- Msajili Mahakama Kuu atoa ujumbe mzito kwa wajumbe
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Dodoma
Kamati ya Kitaifa ya
Kusukuma Mashauri ya Jinai leo tarehe 6 Februari, 2025 imefanya kikao kujadili
mambo mbalimbali yanayolenga kuharakisha usikilizaji na utoaji haki kwa wakati
kwenye mashauri ya jinai.
Kikao hicho ambacho
kimefanyika katika moja ya kumbi za mikutano katika jengo la Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma kimeongozwa na Msajili wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa.
Wajumbe kutoka Taasisi
mbalimbali, ikiwemo Mahakama ya Tanzania, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka,
Magereza, Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Chama cha
Mawakili Tanganyika na nyingine zinazounda Kamati hiyo wamehudhuria kikako
hicho muhimu.
Wakati wa Kikao hicho,
wajumbe hao wamejadili mambo mbalimbali, ikiwemo taarifa ya hali ya mashauri ya
mlundikano mpaka kufikia mwezi Desemba, 2024, hali ya Mahabusu magerezani na
mkakati wa kupunguza mlundikano na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
TEHAMA- kwenye usikilizaji wa rufaa na maombi.
Akizungunza wakati wa
kufungua kikao hicho, Mhe. Tengwa, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo,
aliwaeleza wajumbe kuwa matumizi ya TEHAMA kwa sasa siyo anasa, bali ni nyenzo
muhimu inayohitajika katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
‘Hili ni jambo
lisiloepukika. Mahakama ya Tanzania, kwa kutambua hilo, kwa kiwango kikubwa
ilijipanga na kuhakikisha kwamba inaachana na tabia za awali na mfumo wa zamani
wa kutumia karatasi. Kwa sasa ipo katika mfumo wa kidijitali,’ amesema.
Mhe. Tengwa aliwakumbusha
wajumbe wito uliotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdu Kagomba
alipokuwa anafungua kikao kama hicho tarehe 9 Februari, 2024 ambapo alisisitiza
mambo mbalimbali, ikiwemo uwekezaji mkubwa kwenye mfumo wa TEHAMA.
Mambo mengine
yaliyosisitizwa ni kila Taasisi kuajiri watalaam wa TEHAMA, ushirikiano baina
ya Taasisi moja na nyingine na kuhakikisha mifumo inasomana na pia Watumishi wa
Taasisi hizo kuwa na vifaa stahiki vya TEHAMA ili kuongeza ufanisi katika kazi.
‘Tunaendelea kutoa
msisitizo na ushirikiano kwenye dhamira ya dhati ya kutumia TEHAMA. Mahakama ya
Tanzania, hususan Mahakama ya Rufani, imekuwa mstari wa mbele katika matumizi
ya TEHAMA. Kwa takwimu tulizonazo, asilimia 90 ya vikao vya Mahakama ya Rufani
kwa mwezi wa Machi vilifanyika kwa njia ya mtandao. Huko tunakoelekea
hakutakuwa na matumizi ya karatasi mahakamani,’ amesema.
Ameelezea matumaini yake
kuwa kikao hicho kitatoa mwelekeo na kuwa na maazimio yaliyoshiba
yatakayoonesha dhamira ya matumizi ya TEHAMA kwa zaidi ya asilimia 90.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni