Jumatano, 5 Machi 2025

MAHAKIMU WAKAZI WAPYA WATANO GEITA WAKABIDHIWA VITENDEA KAZI

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin David Mhina jana tarehe 4 Machi, 2025 alikabidhi Kompyuta Mpakato (Laptop) kwa Mahakimu Wakazi watano wa Mahakama za Mwanzo walioajiriwa hivi karibuni na Mahakama ya Tanzania.

Makabidhiano hayo yalikuwa na lengo la kuboresha na kurahisisha utendaji kazi katika uendeshaji wa mashauri, ikiwa ni pamoja na kwenda na kasi ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Kanda hiyo.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita ni kinara wa matumizi ya TEHAMA katika uendeshaji wa ofisi na usikilizaji wa mashauri.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mhe. Mhina aliwaeleza Mahakimu hao kuwa ili kwenda na kasi ya usikilizaji wa mashauri, ikiwemo utoaji wa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri kwa wakati, ni vyema wakazitumia kompyuta hizo kwa maslahi mapana ya Taasisi.

Kwa upande wao, Mahakimu hao waliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuwapatia vitendea kazi ambavyo vitawawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha na kwa wakati.

Walisema kuwa kabla ya kukabidhiwa vitendea kazi hivyo walikuwa wanakumbana na changamoto wakati wa uendeshaji wa mashauri, kwani walikuwa wakitumia komputa za kuazima na nyingine walizokuwa wanazitumia hazikuwa na ubora,

Jumla ya kompyuta mpakato tano zilikabiziwa kwa Mahakimu Wakazi ambao ni Mhe. Eliaman Litahinge Ayoub wa Mahakama ya Mwanzo Ushirombo, Mhe. Jacob Elinami Shayo wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Rashid Yakweli Khalfan wa Mahakama ya Mwanzo Bugando, Mhe. Bahati Sultani Omary wa Mahakama ya Mwanzo Chato Mjini na Mhe. William Greyson Msuya wa Mahakama ya Mwanzo Kharumwa.

Wengine waliohudhuria makabidhiano hayo ni pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kanda ya Geita, Mhe. Fedrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila na wengine.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin David Mhina akikabidhi Kompyuta Mpakato (Laptop) Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Chato Mjini, Mhe. Bahati Sultani Omary.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin David Mhina akizungumza baada ya kukabidhi vitendea kazi kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo walioajiliwa hivi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni