·
Ni wakati akiwasilisha mada katika
Mkutano wa Majaji Wanawake Duniani (IAWJ) Cape Town
·
Abainisha faida zitokanazo na matumizi
ya TEHAMA, mapambano dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia
·
Alionesha Jengo la Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania na miundombinu ya TEHAMA iliyopo, washiriki wastaajabishwa
Na MARY GWERA,
Mahakama-Cape Town
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mwambao Bagamoyo, Mhe. Edith Mwalukasa ametoa rai kwa Wanachama wa Chama cha Majaji Wanawake Duniani (IAWJ) kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kama zana za kulinda haki, kukuza usawa wa kijinsia, kuwezesha upatikanaji wa haki badala ya kuleta madhara.
Mhe. Mwalukasa aliyasema hayo jana tarehe 11 Aprili, 2025 alipokuwa akiwasilisha mada inayohusu Athari za teknolojia kwenye Ukatili wa Kijinsia katika Mkutano wa 17 Chama hicho unaofanyika katika Mji wa Cape Town nchini Afrika Kusini, ambapo ametoa mfano wa Mahakama ya Tanzania kutumia TEHAMA ipasavyo katika jukumu la utoaji haki ikiwemo upatikanaji wa taarifa za kijinsia .
Alisema kuwa, matumizi ya Akili unde yanaweza kuchanganua mkusanyiko mkubwa wa data na kutambua vipengele vya hatari na mienendo inayohusishwa na vurugu pamoja na kusaidia katika maendeleo ya sera yenye msingi wa ushahidi.
Aliongeza kwamba, Teknolojia inaruhusu upatikanaji wa elimu ambayo inaweza
kupinga kanuni hatari za kijinsia na kukuza usawa.
“Matumizi ya TEHAMA huwezesha utaratibu wa kutoa taarifa kwa mamlaka katika mashauri ya kugundua vurugu, ushahidi wa kielektroniki unaotumika kuthibitisha au kukanusha madai, utoaji wa jumbe chanya za kukomesha ukatili wa kijinsia,” alieleza Hakimu huyo.
Alisema kuwa, matumizi ya akili unde huwezesha kutoa taarifa kwa mamlaka katika kesi ya kugundua vurugu; ushahidi wa kielektroniki unaotumika kuthibitisha au kukanusha madai, jumbe chanya wa kukomesha ukatili wa kijinsia
Aliwaeleza washiriki wa Mkutano huo jinsi Mahakama ya Tanzania ilivyopiga hatua katika matumizi ya TEHAMA, ambapo alitaja baadhi ya mifumo ambayo inatumika katika Mhimili huo ambayo ni pamoja na Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS), TanzLII na mingine.
Akizungumzia kuhusu Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mwalukasa
alisema jengo hilo lina Chumba maalum cha Kutolea Taarifa mbalimbali za
Kimahakama (Judiciary Situation Room).
Aliongeza kuwa, katika kuhakikisha kuwa Mahakama ya Tanzaia inaendelea
kutoa haki kwa wananchi ilianzisha Kituo maalum cha Masuala ya Familia Temeke
lengo likiwa ni kushughulikia migogoro ya kifamilia ikiwa ni pamoja na masuala
yanayohusu wanawake.
“Vilevile Mahakama ya Tanzania tunatumia Mahakama Mtandao ‘Virtual Court”, Mfumo
wa Unukuzi na Tafsiri (TTS) na kadhalika vyote ni katika kuhakikisha haki
inapatikana kwa wakati,” alisema Mhe. Mwalukasa.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mwambao Bagamoyo, Mhe. Edith Mwalukasa akitoa mada kuhusu Athari za teknolojia kwenye Ukatili wa Kijinsia jana tarehe 11 Aprili, 2025 katika Mkutano wa 17 Chama hicho unaofanyika katika Mji wa Cape Town nchini Afrika Kusini.
Washiriki wa Mkutano wakifuatilia wasilisho lililokuwa likitolewa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mwambao Bagamoyo, Mhe. Edith Mwalukasa (hayupo katika picha).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni