Jumamosi, 5 Aprili 2025

HISTORIA YAANDIKWA, JENGO LA KWANZA LA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA YA TANZANIA LAZINDULIWA

·        Rais Samia akiri kuwa jengo hilo lina hadhi na sifa ya kuwa Makao Makuu ya Mahakama

·        Aipa kongole Mahakama kwakuwa na Mifumo ya TEHAMA inayosomana na kuzitaka Taasisi nyingine za Serikali kuiga

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 05 Aprili, 2025 ameweka historia kwa Mhimili wa Mahakama kwa kuzindua rasmi Jengo la kwanza la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na kukiri kuwa jengo hilo la kisasa na la Kimataifa lina kila sifa na hadhi ya kuwa Makao Makuu ya Mhimili huo.

Uzinduzi wa jengo hilo ni hatua kubwa kwa historia ya Mahakama nchini kufuatia ukweli kwamba, Mhimili huo haukuwahi kuwa na jengo la makao makuu kwa kipindi cha miaka 104 tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza wakati akitoa hotuba yake kwenye hafla ya uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa, hatua ya upatikanaji wa jengo hilo ni moja ya maboresho makubwa yaliyofanyika ndani ya Mhimili wa Mahakama lengo likiwa ni kuboresha huduma ya upatikanaji haki.

“Leo tumeandika historia nyingine kubwa zaidi kwa upande wa Mahakama na Nchi, ni zaidi ya ile ya awali ya uzinduzi wa majengo ya Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs) sita. Nimelikagua jengo hili kwenye baadhi ya Ofisi zikiwemo Vyumba vya Magereza, Chumba maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama, Ofisi za Mawakili Watoto na nikiri kuwa lina kila sifa la kuwa Makao Makuu ya Mahakama,” amesema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia hakusita kuipongeza Mahakama ya Tanzania chini ya Uongozi wa Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kuendelea kuwa mfano mzuri wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ambapo ameonesha kufurahishwa na Chumba maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama (Judiciary Visual Situation Room).

“Nimeona Chumba maalum cha Mifumo ya utoaji taarifa mbalimbali (Judiciary Situation Room) ambayo nimeambiwa ni ya pili kwa ukubwa duniani, kwakweli nimeshangazwa na yaliyomo ndani, tunayoyashuhudia leo ni matokeo ya tuliyashuhudia kwenye nchi za wenzetu,” amesema Mhe. Samia.

Ameongeza kuwa, Serikali inachukua suala la utoaji wa haki kwa uzito wa pekee na kwamba mpaka sasa jumla ya miradi 144 ya ujenzi na ukarabati wa majengo ya ngazi mbalimbali za Mahakama unaendelea na kuahidi kuwa, miradi itakamilika kwa wakati.

Rais Samia, amebainisha kuwa kazi iliyofanywa na Mahakama ni zaidi ya kile kilichoahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na Dira ya Taifa ya Maendeleo.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa, “Serikali itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi wake kadri uwezo wa kibajeti utakavyoruhusu.”

Kwa upande mwingine, amewakumbusha watumishi wa Mahakama kuimarisha utoaji wa huduma ya haki kwa wananchi na kugusia juu ya umuhimu wa Mahakama za Mwanzo kutofungwa na masharti ya kiufundi yanayozuia haki kutendeka kwa wakati.

Katika hotuba yake, Rais Samia amewasisitiza pia watumishi wa Mahakama kuhusu utunzaji wa miundombinu ya majengo ya Mahakama ambapo amekazia kwa kusema kwamba, “Jengo hili la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na mengine niliyoyazindua nikipita hata baada ya miaka mitatu yawe hivihivi kwakuwa gharama za ukarabati ni kubwa.”

Ameikumbusha pia Mahakama kufanya maboresho ambayo pia yanazingatia Mahakama maalum mfano Mahakama ya Ardhi, Mahakama ya Masuala ya Familia na kadhalika.

Miradi mitatu iliyozinduliwa leo imegharimu kiasi ya fedha za kitanzania bilioni 185.4. Kupatikana kwa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama kunafanya Mihimili yote mitatu ya Dola ikiwemo Serikali na Bunge kuwepo Makao Makuu ya Nchi jijini Dodoma.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania sambamba na Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji, hafla hiyo imefanyika leo tarehe 05 Aprili, 2025 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama Mtaa wa Tambukareli jijini Dodoma. Wa nne kushoto ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa tatu kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa nne kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro, wa tatu kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitoa hotuba yake leo tarehe 05 Aprili, 2025 wakati wa uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.


Muonekano wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililozinduliwa leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Muonekano wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na Tume ya Utumishi wa Mahakama yaliyozinduliwa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Nyumba 48 za Makazi ya Majaji ambazo zimezinduliwa leo pia na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimkabidhi Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma mfano wa ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililozinduliwa leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia) pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 05 Aprili, 2025 wakati wa hafla ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.

Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya Maandalizi ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.





Kwaya ya Mahakama ikitumbuiza katika hafla hiyo.

Mtendaji Mkuu wa kwanza wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga (kushoto) pamoja na Mtendaji Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru pamoja na wageni wengine wakiwa katika uzinduzi wa majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba za Makazi ya Majaji iliyofanyika leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Serikali, Watumishi wa Mahakama ya Tanzania pamoja na wageni waalikwa wakiwa katika hafla ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Nyumba za Makazi ya Majaji.














 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni