Jumanne, 15 Aprili 2025

HOTUBA YA KUSISIMUA YA JAJI MKUU MOROGORO

  • Akipa kazi Chama cha Majaji na Mahakimu kuhusu upotoshaji
  • Ataka upotoshaji mitandaoni ujibiwe kikamilifu
  • Asema hakuna sehemu iliyo na haki kama Mahakama

Na FAUSTINE KAPAMA na ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amekitaka Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) kuandaa utaratibu wa kutoa ufafanuzi wa kweli kunapotokea upotoshaji wowote kwenye mitandao ya kijamii kuhusu Mahakama na maamuzi yanayotolewa.

Mhe. Prof. Juma ametoa wito huo leo tarehe 15 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2024 wa JMAT, ambao unafanyika mwaka huu 2025 katika Hoteli ya Morena mjini hapa.

‘Hili ni eneo ambalo tunatakiwa tuliangalie kwa makini sana, kama JMAT tuwe na utayari wa kutoa ufafanuzi wa kweli kama kuna upotoshaji wowote kuhusu Mahakama na maamuzi yanayotolewa…

‘Tuwe na utaratibu wa kujitokeza kama Chama, siyo kupotosha na sisi, bali kuelimisha. Kwa bahati mbaya Wananchi wanategemea sana mitandao ya kijamii, wengine wanaamini. Kuna upotoshaji mwingi sana,’ Jaji Mkuu amesema.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa moja ya upotoshwaji ambao unazunguka ni kwamba Majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani wakiteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanakuwa hawana uhuru wa kufanya maamuzi kwa mujibu wa Katiba na Sheria.

‘Sote tunafahamu hali siyo hivyo kwani mara baada ya kuteuliwa huwa kuna kuapa kutekeleza majukumu yako kwa mujibu wa Katiba na Sheria, bila chuki wala upendeleo…

‘Lakini ukisoma kwenye mitandao, Wananchi wanaamimishwa kwamba unapoteuliwa na Rais unakuwa huna uhuru. Hili jambo ni vizuri muwe mnalisemea mara kwa mara,’ amewaambia wanachama wa JMAT.

Jaji Mkuu amefafanua kuwa bahati nzuri hoja hiyo ilipelekwa kwenye Mahakama moja kule Canada na hoja kama hizo zikatolewa kwenye kesi ya Matiko dhidi ya Barric Gold Cooperation na uamuzi ulitolewa mwezi Oktoba 2024.

Mhe. Prof. Juma ameeleza kuwa katika uamuzi wake, Jaji wa Canada alitetea mfumo wa Sheria wa Tanzania na kusema kuwa siyo kweli kuwa Rais anapoteua Majaji hachukui mamlaka yao waliyopewa na kutoa maamuzi kwa mujibu wa Katiba ana Sheria.

‘Katika maamuzi hayo, mfumo wa Katiba ya Tanzania umeweka kinga nyingi zaidi kuliko Katiba ya Canada katika uteuzi wa Majaji. Hivyo, uhuru wetu wa kutoa maamuzi usiteteleshwe na yale yanayoendelea kwenye mitandao, ni jukumu letu kuwaelimisha Wananchi, amesema.

Ameeleza pia kuwa bahati mbaya huwezi kukuta kwenye mitandao ya kijamii watu wakijadili uamuzi huo kwa sababu wapotoshaji hawataki Wananchi wajue ukweli.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa hakuna sehemu iliyo na haki kama Mahakama kwani Majaji na Mahakimu mara nyingi wamekuwa wakiwaongoza Wadaawa wanaofika mahakamani, ambao hawafahamu taratibu, sheria na hawana Mawakili, namna ya kufanya wanapotafuta haki.

‘Nadhani, Msajili Mkuu tuweke takwimu ya Wananchi wangapi wanakuja mahakamani hawana msaada wowote wa kisheria, lakini wanashinda na pengine wanashinda upande ule ambao wana Mawakili,’ amesema.

Jaji Mkuu amesema kuwa mambo kama hayo mazuri yanayofanyika mahakamani huwa hayatangazwi na Mahakama inaonekana kama sehemu ambayo haina haki.

Akizungumzia uhuru wa Mahakama, Mhe. Prof. Juma ameeleza kuwa JMAT wana mchango mkubwa na moja ya jukumu lao kwa mujibu wa Katiba yao ni kutetea uhuru wa Mahakama.

Amewakumbusha pia kwamba maendeleo ya Teknolojia ya Habari yameongeza uwazi wa majukumu ya Majaji na Mahakimu na maendeleo hayo makubwa yamekuja na changamoto dhidi ya Uhuru wa Mahakama.

‘Uhuru wa Majaji na Mahakimu kuamua bila shinikizo hutikiswa sana katika zama hizi za Mapinduzi ya Nne ya Viwanda kupitia mitandao ya kijamii,’Jaji Mkuu amesema.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa wapo watumiaji wa mitandao ya kijamii ambao wamejijengea umaarufu wa kuweza kumshambulia Jaji au Hakimu yeyote kwa jina na kwa picha, na wafuasi wake wakajazia maneno ambayo huwashushia heshima.

‘Ukiingia kwenye mitandao ya kijamii unaweza kushangaa kama hii ni Tanzania ninayoifahamu au Tanzania ya kufikirika. Ukweli mnaufahamu na nafikiri huu ukweli tuendeleaa kuutaja,’ Jaji Mkuu amewaeleza wanachama wa JMAT.

 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisisitiza jambo alipokuwa anafungua Mkutano wa Mwaka wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania mjini Morogoro leo tarehe 15 Aprili, 2025.


Sehemu ya wajumbe wa Mkutano huo-juu na chini-ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.



Sehemu nyingine ya wajumbe wa Mkutano huo-juu na chini-ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.



 Sehemu nyingine ya tatu ya wajumbe wa Mkutano huo-juu na chini-ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Sehemu nyingine ya nne ya wajumbe wa Mkutano huo-juu na chini-ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.



Sehemu nyingine ya tano ya wajumbe wa Mkutano huo-juu na chini-ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni