- Naibu Msajili Elimo Massawe awa Rais
Na
ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro
Chama
cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) kimefanya uchaguzi na kupata safu mpya
ya uongozi katika ngazi mbalimbali, huku Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Mhe. Elimo Massawe akichaguliwa kuwa Rais wa Chama hicho.
Uchaguzi
huo umefanyika jana usiku tarehe 15 Aprili, 2025 katika ukumbi wa hoteli ya Morena
mkoani hapa, ukishuhudiwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Juma, Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Viongozi
wengine.
Viongozi
waliomaliza muda wao, Jaji John Kahyoza, Rais, Mhe. Shaibu Mzandah, Makamu wa
Rais, Mhe. Lazaro Magai, Katibu. Mhe. Marry Kallomo, Naibu Katibu na Mweka Hazina,
Mhe. Devotha Kasebele, wameshukuru kwa ushirikiano waliopata kwa wanachama.
Kabla
ya kumaliza muda wao, Viongozi hao walipata nafasi ya kuzungumza na wanachama
na kuwashukuru kwa ushirikiano wao kwa muda wote ambao walitumikia katika
kipindi cha miaka minne.
Wakati
wa uchaguzi huo, Mhe. Massawe ameibuka kidedea kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa
chama hicho baada ya kupata kura 111, huku mpinzani wake wa karibu, Jaji wa
Mahakama ya Rufani, Mhe. Latifa Mansoor akijinyakulia kura 82, kati ya kura 280
zilizopigwa na wanachama wa chama hicho.
Mhe.
Mansoor amepitishwa na wanachama wote kwa kura za ndiyo kuwa Makamu wa Rais
mara baada ya kuwa mshindi wa pili katika kinyang`anyiro cha urais na wajumbe
wote kuridhia kumpitisha kushika nafasi hiyo mara baada ya Rais kuwa na sifa ya
Hakimu na mwenza wake kutakiwa kuwa Jaji kwa mujibu wa katiba ya JMAT.
Viongozi
wengine waliochaguliwa ni Mhe. James Mniko aliyechaguliwa kuwa Katibu Mkuu kwa
kura 80, Mhe. Teddy Raphael Mlimba aliyezoa kura 157 kwenye nafasi ya Naibu
Katibu Mkuu na Mhe. Kasebele alifanikiwa kutetea nafasi hiyo baada ya kupata kura
169 kati ya 280.
Akifunga
mkutano huo, Mlezi wa Chama hicho na Jaji Mkuu wa Tanzania aliwapongeza
washindi wote katika nafasi mbalimbali, huku akiwaahidi kuwapa ushirikiano na
kuwaomba wasisite kwenda ofisini kwake kama watakumbana na changamoto yoyote.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni