Na NAOMI KITONKA, Kituo Jumuishi Temeke
Jaji
Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa amefungua mafunzo kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika
na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV) yanayotolewa kwa Mahakimu
Wakazi, Waendesha Mashtaka, na Maafisa Ustawi wa Jamii.
Akifungua
mafunzo hayo tarehe 14 Aprili, 2025 yaliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama
hiyo, Mhe. Mnyukwa alisisitiza umuhimu wa kuboresha mifumo ya utoaji haki ili
iwe jumuishi, yenye huruma na inayowajali wahitaji wa huduma za haki hasa
kutoka makundi yaliyo hatarini kama sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania
katika kukamilisha majukumu yake.
“Ukatili
wa kijinsia umekuwa suala kubwa katika jamii yetu, hivyo ipo haja ya
kuhakikisha haki inatendeka pale mashauri ya jinsi hiyo yanapoletwa mahakamani
kwa kuzingatia hali walizo nazo wahanga wa ukatili huo na kama Mahakama na watu
tuliopewa dhamana tunatambua umuhimu wa kutumia lugha yenye huruma, staha na
weledi mkubwa pamoja na kujenga mazingira yenye usalama kwa waathirika wa
ukatili tunaposikiliza mashauri mahakamani” alisema Mhe. Mnyukwa.
Jaji
Mnyukwa alihimiza washiriki kuwa makini na mbinu wanazotumia katika
kushughulikia mashahidi walio katika mazingira magumu ili wasiwajengee hali ya
woga au kukumbuka majeraha yao ya awali.
Aidha,
imeelezwa kuwa, mafunzo hayo yanatolewa kwa lengo la kuwajengea washiriki uwezo
wa kuzuia na kuepusha kurejesha majeraha yatokanayo na ukatili wa kingono na
kijinsia kwa ujumla wake na yamekusudiwa pia kubadilisha namna ya kuwachukulia
na kuwalinda wale ambao wako hatarini katika michakato ya kisheria sambamba na
usikivu wa Mahakama, kuchunguza mienendo tata ya unyanyasaji wa kijinsia na
kuelewa jukumu muhimu ambalo Mahakama inatekeleza katika usimamizi wa haki.
Washiriki hao wamepata nafasi ya kujifunza kwa vitendo na kujadili matukio halisi yanayotokea mahakamani wakati wa kusikiliza mashauri pamoja na kujifunza mbinu salama za kuwauliza maswali mashahidi walio katika mazingira magumu na kulinda haki na utu wa waathirika na jinsi ya kuwa na mikakati ya pamoja ya utekelezaji wa maarifa hayo muhimu katika kufanikisha zoezi la utoaji haki na pia kuwaepushia waathirika maumivu.
Wawezeshaji
wa mafunzo hayo ni Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa
Mahakama (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda na Mratibu wa Mafunzo wa Chuo cha
Uongozi wa Mahakama IJA. Mhe. Husna Rweikiza.
Mafunzo
hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa
kushirikiana na ‘Irish Rule of Law International’ (IRLI) na kwa ufadhili wa
Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania yatafanyika kwa muda wa siku tatu. Yamehudhuriwa
na washiriki mbalimbali wakiwemo Mahakimu Wakazi, Waendesha Mashtaka na Maafisa
Ustawi wa Jamii.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa (aliyesimama) akitoa neno la ufunguzi mbele ya Washiriki wa mafunzo kuhusu Kuepuka Kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) yaliyofanyika tarehe 14 Aprili, 2025 kituoni hapo. Kulia ni Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe Husna Rweikiza, (kulia) na kushoto ni Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda.
Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akisisitiza jambo mbele ya washiriki wa mafunzo maalum kuhusu kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) yaliyofanyika tarehe 14 Aprili 2025 katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke.
Washiriki wa
mafunzo maalum kuhusu kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa
ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV), Mhe. Magdalena Malaba (kushoto) na Mhe. Juliana Nankoma (kulia) wakifuatilia kinachojiri katika mafunzo hayo.
Mratibu wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Mhe. Husna Rweikiza akiwasilisha mada mbele ya washiriki wa mafunzo maalum kuhusu kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) yaliyofanyika jana tarehe 14 Aprili 2025 kituoni hapo.
Wajumbe wa
Sekretarieti, Mhe. Edna Mollel na Mhe. Gloria Shuma wakifuatilia wasilisho la Mratibu wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA), Mhe.
Husna Rweikiza (hayupo katika picha) katika mafunzo maalum kuhusu kuepuka kutonesha majeraha kwa
waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) yaliyofanyika tarehe 14 Aprili, 2025 kituoni hapo.
Washiriki wa mafunzo maalum kuhusu kuepuka utonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda (Hayupo pichani) yaliyofanyika jana tarehe 14 Aprili 2025 kituoni hapo.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa akiwa katika
picha ya pamoja washiriki wa mafunzo kutoka Ofisi ya Waendesha Mashtaka (NPS)
waliohudhuria katika wa mafunzo hayo yaliyofanyika tarehe 14 Aprili, 2025 kituoni hapo.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa akiwa katika picha ya pamoja na Washiriki wa mafunzo yanayohusu Kuepuka Kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono (SGBV) yaliyofanyika tarehe 14 Aprili, 2025 katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni