- Asema kila mmoja atapimwa mfumo upi ametumia, kwa kiasi gani
Na FAUSTINE KAPAMA na
ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro
Jaji Mkuu wa Tanzania,
Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewahimiza Majaji na Mahakimu kote nchini
kuongeza kasi ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA- kwenye
usikilizaji wa mashauri ili kufanya vizuri zaidi katika utekelezaji wa jukumu la
utoaji haki kwa Wananchi.
Mhe. Prof. Juma ametoa
wito huo leo tarehe 15 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Mkutano Mkuu wa Mwaka
2024 wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT), ambao umefanyika mwaka
huu 2025 katika Hoteli ya Morena mjini hapa.
‘Taarifa ya Msajili Mkuu
katika Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi inaonesha kuwa mwaka jana 2024, sisi
wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania, tuliweza kumaliza mashauri
mengi (mashauri 245,310) zaidi ya yale yaliyopokelewa (mashauri 242, 284),’
amesema.
Jaji Mkuu amewapongeza wanachama
hao kwa mafaniko hayo makubwa katika kutimiza wajibu wao wa kikatiba kama
Mamlaka yenye Kauli ya Mwisho ya Utoaji Haki katika Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Hata hivyo, Mhe. Prof.
Juma amebainisha kuwa Majaji na Mahakimu bado wanayo nafasi ya kufanya vyema zaidi
endapo watajikita katika matumizi ya TEHAMA kwenye usikilizaji wa mashauri.
Amewakumbusha kuzingatia Waraka
No. 1 wa Jaji Mkuu, ambao unaeleza kuwa uongozi utaanza kupima matumizi ya
uwekezaji mkubwa ambao umefanyika kwenye mifumo mbalimbali ya TEHAMA.
‘Ni jambo moja kuwekeza
kwenye mifumo ya TEHAMA na ni jambo tofauti kabisa kama hatutumii kikamilifu. Fedha
nyingi sana zimetumika katika kuwekeza kwenye mifumo hiyo. Sasa umefika wakati
tuweze mwisho wa mwaka kujua nani ametumia mfumo upi na kwa kiasi gani ili
tuone mapungufu yapo wapi tuweze kuboresha,’ Jaji Mkuu amesema.
Mhe. Prof. Juma
amebainisha pia kuwa, kwa kutumia mifumo ya TEHAMA wanaweza kuhifadhi data
kubwa ambayo imesheheni mambo mengi yanayoweza kuwasaiduia kujua
kinachoendelea.
Amesema kuwa wamefika
katika wakati ambao ni tofauti kabisa na wakati mwengine na kwamba uwepo wa
Kituo cha Kutolea Taarifa ambacho kinapokea data zote, utasaidia kuchakata taarifa
na kuweza kujua ni maeneo gani yanahitaji maboresho.
‘Ninawaomba sana tuongeze
nguvu katika matumizi ya TEHAMA, kwa sababu ule Waraka utakuwa unatupima kama Mahakama
na mtu mmoja mmoja ili tuweze kujua uwekezaji mkubwa ambao tumefanya kwenye
mifumo kama unatoa matunda makubwa. Ninaamini tukijipima tutakuwa na sifa zaidi
ya hizi tulizo nazo sasa,’ amesema.
Jaji Mkuu amewapongeza na
kuwashukuru wanachama wote wa Chama cha Majaji na Mahakimu wa Tanzania kwa
kuendelea kutimiza wajibu wao wa kutekeleza Dira ya Mahakama ya Tanzania ambayo
ni “Haki
Sawa kwa Wote kwa Wakati.”
Awali, akizungumza wakati
wa ufunguzi wa Mkutano huo, Rais wa JMAT na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza aliupongeza uongozi wa Mahakama
kwa kurejesha mahusiano mazuri ya Chama hicho na Mahakama ya Tanzania.
‘Sote ni mashahidi wa
mahusiano mabaya ambayo yalikuwepo huko nyuma. Wimbi la mahusiano mabaya hayo
halikuikumba Tanzania pekee yake, liliikumba Afrika Mashariki, wengine
walidiriki kupelekana mahakamani, sisi tusifikie huko,’ alisema.
Aliwaambia wanachama wa
JMAT kuwa ni muhimu mahusiano yao na Mahakama kuyalinda na kuyaheshimu kwa
manufaa ya wote. Kadhalika, Mhe. Kahyoza aliupongeza uongozi wa Mahakama kwa
kuboresha mazingira ya kufanyia kazi, hususan majengo na maslahi kwa ujumla ya
wanachama.
Viongozi wakuu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-katikati-juu na chini. Wengine kutoka kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.
Sehemu ya wajumbe wa mkutano huu-juu na chini- ikifuatilia yanayojiri.
Sehemu nyingine ya wajumbe wa mkutano huu-juu na picha mbili chini- ikifuatilia yanayojiri.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni