Alhamisi, 17 Aprili 2025

JAJI BARTHY AFUNGA MAFUNZO YA UKATILI WA KINGONO

Na NAOMI KITONKA-Mahakama, Kituo Jumuishi Temeke.

Mafunzo ya siku tatu kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV) kwa Mahakimu Wakazi, Waendesha Mashtaka, na Maafisa Ustawi wa Jamii yamefungwa jana tarehe 16 Aprili 2025 na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Famila – Temeke, Mhe. Gladys Barthy.

Katika kuhitimisha mafunzo hayo yaliyokuwa yanafanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho, Mhe. Barthy alisisitiza umuhimu wa kila mshiriki wa mafunzo kuwa chachu ya kuyatenda yale waliyojifunza kwa vitendo na pia kubadilishana uwezo na Watumishi wengine, hasa linapokuja suala la kuwahudumia wahanga na waathirika wa ukatili.

“Siku hizi chache zenye mafunzo mengi na kubadilishana uzoefu kusiwe bure, kwa uchache wetu tujitahidi kama W,atumishi wa Mahakama kuhakikisha tunakuwa watu wa kwanza kuwalinda walio hatarini na kuepusha kuwarejeshea majeraha yatokanayo na ukatili wa kingono na kijinsia ili tuwe mfano bora wa kuigwa” aliongea Mhe. Barthy.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya washiriki wengine, Mhe. Mhangwa Yunge alisema kuwa mafunzo hayo yamewabadilisha mtazamo na kuweka alama ya namna ambavyo, kama watu wenye dhamana ya kutoa haki, wanapaswa kuwasaidia waathirika wa unyanyasaji na mchango mkubwa walionao katika kuwaondolea woga wa taratibu za kimahakama.

Naye Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda, akizungumza katika hafla hiyo, alisema, “Tunawashukuru wote kwa kushiriki na mafunzo haya yamekuwa ya vitendo zaidi na tumeona mafanikio ya yale mengi ambayo tumefundishwa mahali hapa na sisi tukawe mabalozi wazuri katika vituo vyetu vya kazi, kuhakikisha ujuzi na maarifa haya adhimu yanaleta matokea chanya katika utendaji wetu na jamii kwa ujumla.”

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Gladys Barthy akizungumza mbele ya Washiriki wakati wa kufunga mafunzo maalum kuhusu kuepuka utonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono yaliyofanyika kwa siku tatu.

Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA), Mhe. Dr. Patricia Kisinda akisisitiza jambo mbele ya washiriki wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Afisa Ustawi wa Jamii, Bi. Asha Mbaruku akitoa wasilisho la ukatili wa kijinsia mbele ya washiriki wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi, Mhe. Mohamed Burhan akitoa wasilisho mbele ya washiriki hao.

Hakimu Mkazi, Mhe. Mhangwa Yunge (aliyesimama) akitoa neno la shukrani kwa niaba ya washiriki wa mafunzo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Gladys Barthy akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Sekretarieti wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kituo Jumuishicha Masuala ya Familia- Temeke, Mhe. Gladys Barthy akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Gladys Barthy akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni