Alhamisi, 3 Aprili 2025

JAJI MFAWIDHI DAR ES SALAAM HATAKI MZAHA

  • Ahimiza ujenzi wa Mahakama za Mwanzo tano kukamilika haraka
  • Amtaka Mkandarasi kufanya kazi usiku na mchana

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amemtaka Mkandarasi wa Ujenzi wa majengo ya Mahakama za Mwanzo tano zilizopo katika Kanda hiyo, Deep Construction Ltd kufanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha mradi huo kwa wakati.

Mhe. Maghibi alieleza akiwa kwenye zira yake ya ukaguzi wa shughuli za usimamizi wa Mahakama na Magereza kwa robo mwaka ya Jan hadi Machi 2025 kuwa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Msata, Kimanzichana na Bungu Mkoa wa Pwani na Mbagala na Somangila Mkoa wa Dar es Salaam upo nyuma na unatakiwa kukamilika ifikapo mwezi Mei, 2025.

Awali, akiwa katika mradi wa Mahakama ya Mwanzo Mbagala jijini Dar es Salaam, Jaji Maghimbi alipokea taarifa ya utekelezaji wa miradi hiyo mitano kutoka kwa Msanifu Majenzi, Bw.Henry Mwoleka ambaye ni Mwakilishi wa Mtaalamu Mshauri wa miradi hiyo kutoka Kampuni ya Jaji Norman&Dawbarn (T)Ltd.

Taarifa hiyo ilionesha kuwa miradi hiyo ilitakiwa kuwa imekamilika ifikapo mwezi Februari, 2025 lakini kutokana na sababu mbalimbali kubwa ikiwamo Mkandarasi kutotimiza wajibu wake kikamilifu, imesababisha kuwa nyuma ya ratiba, jambo lililosababisha muda wa ujenzi kuongezwa.

 Alisema kwamba Mkandarasi ameweza kukamilisha katika miradi yote ujenzi wa msingi tu (Sub structure) sawa na asilimia 15, sasa ameanza ujenzi wa kuta unaotarajiwa kukamilika ndani ya wiki mbili.

Kufuatia taarifa hiyo na ukaguzi uliofanyika katika miradi yote kati ya tarehe 25-27 Machi,2025, Mhe Maghimbi hakufurahia kasi iliyopo ya ujenzi na pia hali isiyoridhisha ya vifaa vya kufanyia kazi kama matofali,saruji,nondo na mchanga hivyo, kumtaka Mkandarasi kufanya kazi usiku na mchana.

“Nimekagua miradi yote mitano na kukuta kasi ya ujenzi siyo ya kuridhisha ikilinganishwa na muda uliobaki wa kutekeleza mradi huu. Namtaka Mkandarasi kuongeza kasi kwa kufanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha miradi hiyo ifikapo mwezi Mei,2025. Namtaka pia kuongeza wafanyakazi wataalamu na vibarua, kuongeza matofali, saruji, nondo, mchanga na vifaa muhimu hitajiwa haraka.Nitarudi tena kukagua hata kwa ratiba isiyo rasmi” a,lisema Jaji Maghimbi.

Kwa upande mwingine, Jaji Maghimbi alimtaka Mtaalamu Mshauri Kampuni ya  Norman&Dawbarn (T) Ltd kutimiza wajibu waliopewa wa kusimamia kwa karibu miradi hiyo ili ikamilike kwa wakati. Alikumbusha umuhimu wa miradi hiyo kwa Mahakama hususani maeneo ya Mbagala ambako imelazimika kukodi nyumba ya mtu binfsi ili kuendeshea mashauri wakati wakisubiri ujenzi kukamilika.

Mhe Maghimbi alikagua pia shughuli za usimamizi wa Mahakama za Mwanzo Bungu, Kimanzichana,  Mbagala , Msata, Mwambao  Ikerege pamoja na Gereza la Wazo Hill ambako alihimiza matumizi sahihi ya mfumo wa usajili wa mashauri upitia Programu tumizi ya Mahakama za Mwanzo.

Kadhalika, alihimiza uzingatiaji wa taratibu za uendeshaji wa mashauri katika Mahakama za Mwanzo, miongozo mbalimbali ya usimamaizi wa Mahakama na kuondoa mlundikano wa mashauri na Mahabusu magerezeni, hususani wanaotokana na mashauri ya Mahakama za Mwanzo.

Katika ziara hiyo, Jaji Maghimbi aliongozana na Viongozi wengine, akiwepo Naibu Msajili Mfawidhi Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Mary Moyo na Mtendaji wa Mahakama, Bw.Moses Mashaka.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya  Dar es Salaam, Mhe, Salma Maghimbi akiwa kwenye ukaguzi Bungu.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa kwenye ukaguzi Bungu.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa kwenye ukaguzi Msata-juu na chini.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa kwenye ukaguzi Bungu.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni