Jumanne, 8 Aprili 2025

JAJI MFAWIDHI DIVISHENI YA ARDHI AONGOZA KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Ardhi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda, hivi karibuni aliwaongoza Watumishi kufanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi cha mwaka 2025.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Wazi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Luvanda aliwaambia Watumishi hao kuwa Mabaraza hayo ni muhimu kwani yanawapa fursa ya kutoa maoni na ushauri kuhusu nini kinatakiwa kifanyike katika kuboresha mazingira ya mahala pakazi.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi aliwaelezea kuwa vikao vya mabaraza hayo vinafanyika mara chahe kwa mwaka, hivyo ni muhimu kwa Watumishi kuchangia Mawazo chanya ili kuboresha maslahi yao.

Akizungumza na wajumbe katika kuchangia hoja ya utawala na mashauri, Mhe. Luvanda alisisitiza kuwa Chama cha Wafanyakazi ni chombo muhimu kwa ajili ya kusimamia maslahi mapana ya Wafanyakazi.

Pamoja na hilo, Jaji Mfawidhi alisisitiza Viongozi wa TUGHE Tawi kushiriki mafunzo mbalimbali ili kuwa mabalozi wazuri kwa Watumishi wengine kujiunga na Chama hicho kwa maslahi mapana ya kusimamia hoja za Watumishi.

Kiongozi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Bw. Shaibu Kanyochole alisema kuwa miongoni mwa hoja zilizotolewa na Watumishi wa Mahakama ni pamoja na kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara kwa ajili ya kuongeza motisha ili waweze kwenda na mabadiliko ya matumizi ya TEHAMA ambayo yanajitokeza kwa sasa na kuongezewa vitendea kazi.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu wa TUGHE Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Grace Magereli aliwashauri wajumbe kujenga hoja zao vizuri ili zitakapopelekwa katika Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi Taifa ziweze kujibiwa vizuri na Viongozi.

 Aliendelea kufafanua na kushauri Watumishi kujiunga kwenye chama kwa lengo la kuwa na nguvu ya pampoja ili chombo hicho kiweze kuongea kwa nguvu zaidi na kubeba hoja zitakazopelekwa TUGHE Taifa.

Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi wameweza kushiriki katika kikao hicho cha kujadili masuala mbalimbali ya kiutumishi, bajeti na ikiwa ni maandalizi ya Kikao kitakachofanyika Dodoma tarehe 10 na 11 Aprili, 2025.

Kwa upande wake, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Bw. Peter Mbaguli alizitolea ufafanuzi baadhi ya hoja ambazo zinaweza kutatulika ndani ya Divisheni na kuahidi kuwasilisha kwenye Baraza Kuu hoja ambazo zitahitaji majibu ya mwajiri.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi.

Mjumbe wa TUGHE Mkowa wa Dar es Salaam, Bi. Grace Magereli.

Kaimu Mtendaji wa Divisheni ya Ardhi, Bw. Peter  Mbanguli.

Kaimu katibu wa Baraza, Bi. Tumaini Mwalyoga.

Mjumbe wa TUGHE Mahakama ya Tanzania Bw. Kilenza.

Picha za wajumbe wa Baraza la Wafanya Kazi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni