Alhamisi, 24 Aprili 2025

JAJI MKUU ATAKA MKAKATI MADHUBUTI KUKABILI ONGEZEKO LA MASHAURI MAHAKAMA YA RUFANI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ametoa wito kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania kubuni mbinu mpya zitakazosaidia kukabiliana na ongezeko la mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya.

Mhe. Prof. Juma ametoa wito huo leo tarehe 24 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Mkutano wa Mwaka 2024 unaofanyika kwa siku mbili kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, kujadili masuala mbalimbali katika Mahakama ya Rufani na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.

‘Hiki ni kikao cha kupanga mikakati juu wajibu wetu katika kukabiliana na ongezeko la mashauri baada ya kukamilika ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tisa na Mahakama za Mahakimu 60 zinazoendelea kujengwa…

‘…Katika kikao hiki tutakaribisha majadilino yatakayotusaidia kuendelea kubaini maeneo muhimu ambayo bado yanaleta changamoto katika utekelezaji wa majukumu yetu na kutafuta mbinu za kuondokana na changamoto hizo.’ Jaji Mkuu amesema.

Amebainisha kuwa takwimu zinaonyesha idadi ya mashauri yanayofunguliwa Mahakama ya Rufani kwa mwaka imeendelea kuongezeka na kwamba Mkuu wa Idara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA- amefanya makisio ya mzigo ambao Majaji 39 wataubeba kuanzia mwaka 2026 hadi 2030.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa kila Jaji wa Mahakama ya Rufani amekadiriwa uwezo wa kushughulikia rufaa 99 kwa mwaka, hivyo uwezo wa Majaji wa Mahakama ya Rufani 39 ni kushughulikia rufaa 3,861 kwa mwaka.

Amesema kuwa makisio ya ongezeko la rufani kuanzia 2026 hadi 2030 yatakuwa mashauri 10,434 kwa mwaka 2026, mashauri 11,248 mwaka 2027, mwaka 2028 mashauri 12,061, mwaka 2029 mashauri 12,875 na mwaka 2030 ni mashauri 13,690, huku kila mwaka Majaji hao wakiwa na wastani wa kushughulikia mashauri 3,861.

‘Hatuwezi kukabiliana na wingi na ongezeko la mashauri yanayotiririka kupitia ngazi na vituo mbalimbali hadi kuishia katika Mahakama ya Rufani kwa kutegemea tu mpangilio wa kisheria, kanuni na idadi ya Majaji wa Rufani na Majopo yaliyopo,’ Jaji Mkuu amesema.

Amebainisha kuwa Mkutano huo wa Majaji wa Rufani, uwe mwanzo wa kujiwekea mikakati ya kuziangalia sheria, kanuni na kuzichakata upya taratibu za Mahakama ya Rufani na zile za Mahakama za ngazi za chini ili kumudu ongezeko kubwa la mashauri.

Akizungumzia mlundikano wa mashauri, Jaji Mkuu amebainisha kuwa mwaka 2024, Mahakama ya Rufani ilikuwa na mashauri ya mlundikano 1,273, sawa na asilimia 21 ya mashauri yake na kuchangia asilimia 74 ya mlundikano wa mashauri ulioko mahakamani katika ngazi zote, huku ngazi zingine za Mahakama zikiweza kudhibiti changamoto hiyo.

Ameeleza pia kuwa kati ya Januari na Desemba 2024, wakati Mahakama ya Rufani ilikuwa na asilimia 21 ya mashauri ya mlundikano, Mahakama Kuu haikuwa na tatizo hilo kwani mwaka 2024, mlundikano ulikuwa ni asilimia 2 tu, Mahakama za Hakimu Mkazi ulikuwa asilimia 6 pekee na Mahakama za Wilaya zilikuwa asilimia 1 na Mahakama za Mwanzo hazikuwa na mlundikano mwaka 2024.

‘Kwa ulinganifu wa ngazi zote za Mahakama, hali yetu Mahakama ya Rufani sio nzuri katika mlundikano, tunachangia asilimia 74 ya mzigo wa mlundikano katika ngazi zote za Mahakama ya Tanzania,’ Mhe. Prof. Juma amesema.

Jaji Mkuu amesisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji huduma za kimahakama kwani ni njia bora ya kupambana na changamoto hiyo na amewapongeza Majaji wote kwa kuanza utekelezaji wa jambo hilo.

‘Tunaomba tusirudi nyumba, tuendelee kusikiliza mashauri yote kwa njia ya mfumo na tuendelea kubaini changamoto na kuziwasilisha kwa wajenzi wa mfumo ili tuendelee kuboresha zaidi mfumo na kurahisisha utendaji kazi,’amesema.

Ametumia fursa hiyo kuwapongeza Majaji na Watumishi wote wa Mahakama ya Rufani kwa kuendelea na jitihada za kuamua mashauri kwa mafanikio makubwa, licha ya changamoto mbalimbali mnazokabiliana nazo.

Wakati wa Mkutano huo, wajumbe watapokea na kujadili taarifa mbalimbali zinazohusu mashauri katika Mahakama ya Rufani pamoja na masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na ikama, bajeti, stahiki za Majaji, mabadiliko ya sheria kwenye stahiki za Majaji pamoja na mafunzo kwa watumishi wa Mahakama ya Rufani.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-akizungumza wakati anafungua Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 24 Aprili, 2025 jijini Dar es Salaam.

Amidi wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija akimkaribisha Jaji Mkuu wa Tanzania kufungua Mkutano huo. Picha chini ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akitoa maelezo ya awali kuhusu Mkutano huo.

Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na chini-wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa Mkutano huo.

Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na picha mbili chini-wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa Mkutano huo.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani-wa kwanza kulia-pamoja na Viongozi wengine waandamizi wa Mahakama ya Tanzania-juu na chini-wakiwa kwenye Mkutano huo.

Naibu Wasajili na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.

Sehemu nyingine ya Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani pamoja na Watumishi katika Mahakama hiyo-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.


Sehemu nyingine ya tatu ya Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani pamoja na Watumishi katika Mahakama hiyo-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni