Alhamisi, 24 Aprili 2025

MAHAKAMA YA RUFANI NA KASI YA UONDOSHWAJI MASHAURI YA MLUNDIKANO

Na MWANAIDI MSEKWA na NAOMI KITONKA- Mahakama, Dar es Salaam.

  • Kiwango uondoshaji mashauri kimepanda mwaka 2024.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma leo tarehe 24 Aprili 2025 ameongoza kikao kazi cha tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024.

Kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano Julius Kambarage Nyerere, Dar-es Salaam kiliambatana na uwasilishaji wa Taarifa ya Mashauri kwa kipindi cha Januari hadi Disemba 2024 iliyowasilishwa na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert pamoja na taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya kiutawala na kiutumishi kwa mwaka 2024/2025 iliyowasilishwa na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor Kategere.

Akiongea katika taarifa hiyo, Mhe. Herbert alisema takwimu zinaonyesha idadi ya mashauri yanayoondolewa ni kubwa katika kipindi cha mwaka mmoja kulinganisha na kipindi kilichopita cha mwaka 2023, japokuwa mzigo wa mashauri umeongezeka kwa mwaka 2024.

Alisema pia kuwa Mahakama ya Rufani imeendelea kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao kwenye vikao vya majopo, maombi ya faragha, usomaji wa maamuzi na usikilizaji wa maombi ya madai ya gharama za kesi (taxations).

Kadhalika, Mahakama imeendelea kupandisha kwa wakati maamuzi yote yanayopaswa katika tovuti ya TanzLII na kuanzia mwezi Februari mwaka 2025 Mahakama ya Rufani imeanza rasmi matumizi ya mfumo wa eCMS kuanzia kufungua shauri hadi kusomwa hukumu.

Pia taarifa iliyowasilishwa na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani iligusia maeneo muhimu ya vipaumbele vilivyowekwa na Mahakama hiyo, yakiwemo mkakati wa kuharakisha utatuzi wa mashauri ya kawaida, uendeshaji wa vikao vya Mahakama (Session), matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano -TEHAMA Pamoja na kuongeza ushirikiano na wadau wa haki jinai.

“Pamoja na mafanikio haya, Mahakama ya Rufani imedhamiria kuharakisha utatuzi wa mashauri ya kawaida na mkakati wa kumaliza mashauri ya muda mrefu, kuboresha mifumo na matumizi ya TEHAMA, kuimarisha uwezo katika ukaguzi na usimamizi wa shughuli za Mahakama, kuendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama, kuongeza ushirikiano na wadau wa haki jinai pamoja na kuimarisha maendeleo ya rasilimali watu ikijumuisha mafunzo na nidhamu ya watumishi wetu,” aliongeza Bw. Kategere.

Aidha, alihitimisha kwa kusisitiza kuwa Mahakama ya Rufani itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje ili kuhakikisha haki inaendelea kutolewa kwa wakati. Aidha, ili kuwafikia wananchi kwa wakati, Mahakama itaendelea kuimarisha na kuboresha matumizi ya TEHAMA katika huduma mbalimbali zitolewazo na Mahakama.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi, Msajili Mkuu, Mtendaji Mkuu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Wasaidizi wa Sheria na Watumishi wa kada mbalimbali za Mahakama.

Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akitoa wasilisho katika kikao kazi cha tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024 kilichofanyika leo tarehe 24 Aprili 2025.

Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor F. Kategere akitoa wasilisho katika kikao kazi cha Tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024 kilichofanyika leo tarehe 24 Aprili 2025.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzani,a Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na picha mbili chini.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Jaji wa Mahakama Kuu na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wanaohudumu katika Mahakama ya Rufani.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Menejimenti wa Mahakama ya Tanzania.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni