Ijumaa, 25 Aprili 2025

JAJI MKUU ATANGAZA KUUNDA KAMATI KUHUISHA TARATIBU ZA UENDESHAJI MASHAURI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mkutano wa mwaka wa mapitio ya shughuli za Mahakama ya Rufani 2024 uiliokuwa unafanyika kwenye Ukumbi wa Kimataifa Mikutano wa Julius Nyerere jijini hapa kimehitimishwa leo tarehe 25 Aprili, 2025 na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha Mkutano huo, Mhe. Prof. Juma ametangaza kuunda Kamati ya Kuhuisha Taratibu za Uendeshaji wa Mashauri katika Mahakama ya Rufani -Business process Re-engineering-ili kuboresha utendaji kazi katika utoaji haki kwa Wananchi.

Ameagiza mwenendo wa kikao hicho utayarishwe mapema ili kama kuna mambo ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi yafanyiwe kwa haraka zaidi.

‘Kitu kimoja ambacho naenda kukifanya ni kuwa na Kamati ya Business Process Re-engineering ili ianze kazi mara moja na kutupa taarifa kwa muda mfupi ili tujue tunaweza kufanya nini,’ Jaji Mkuu amesema.

Kabla ya kuhitimisha Mkutano huo, Wajumbe walipitishwa kwenye mada mbalimbali, ikiwemo matumizi ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA-katika usikilizaji wa mashauri iliyowasilishwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Mhandisi Benedict Ndomba na Mkurugenzi wa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kaleghe Enock.

Katika wasilisho lao, wataalam hao waliwaeleza wajumbe wa Mkutano kuwa matumizi ya TEHAMA katika sekta na Taasisi mbalimbali hayaepukiki ili kuboresha   huduma kwa urahisi na ufanisi zaidi.

Mada nyingine ilihusu maandalizi ya kustaafu katika utumishi na uongozi iliyowasilishwa na Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi pamoja na ile inayohusu namna ya kuthibiti msongo wa mawazo iliyowasilishwa na Bi. Zuhura Muro.

Katika mada yake, Dkt Mashillingi amewakumbusha Majaji hao kuwa kustaafu ni fursa ya kuanza maisha mapya yenye utulivu na furaha, hivyo maandalizi mazuri, yanaweza kuwa na mchango mkubwa katika jamii na kufurahia maisha.

‘Panga maisha yako: aina gani ya maisha ungependa uishi? Punguza msongo wa mawazo, usitumie akiba yako kwa mambo ya siasa. Samehe na kusahau: huu siyo muda wa kuwaza wale waliokukosea, waliokudhulumu,’ amesema.

Wakati wa Mkutano huo, wajumbe walipokea na kujadili taarifa mbalimbali zinazohusu mashauri katika Mahakama ya Rufani pamoja na masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na ikama, bajeti, stahiki za Majaji, mabadiliko ya sheria kwenye stahiki za Majaji pamoja na mafunzo kwa watumishi wa Mahakama ya Rufani.

Kadhalika, wajumbe walijadili masuala mbalimbali katika Mahakama ya Rufani na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla, ambayo yanalenga kuboresha utendaji wa kazi ya utoaji haki.

Mkutano huo ulihudhuriwa na Majaji wote wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtandaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Naibu Wasajili, Watendaji na watumishi mbalimbali wa Mahakaka hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati wa kuhitimisha Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani Tanzania.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania-juu na chini-ikiwa kwenye Mkutano huo.


Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Watumishi wengine wa Mahakama-juu na chini-ikiwa kwenye Mkutano huo.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Mhandisi Benedict Ndomba akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo.

Mkurugenzi wa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kaleghe Enock akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo. Picha chini ni Mtaalam wa Saikolojia, Bi. Zuhura Muro.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni