Ijumaa, 11 Aprili 2025

KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI TAIFA CHAHITIMISHWA

  • Chatoka na maazimio kadhaa kuimarisha utendaji kazi

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Kikao cha siku mbili cha Baraza la Wafanyakazi Taifa cha Mahakama ya Tanzania kilichokuwa kinafanyika katika Ukumbi wa PSSSF jijini hapa kimehitimishwa leo tarehe 11 Aprili, 2025, huku wajumbe wakitoka na maazimio kadhaa yanayolenga kuimarisha utendaji wa kazi.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha Kikao hicho, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Baraza hilo amewataka Viongozi kuanza mara moja kutekeleza yale waliyojifunza wakati wa Kikao hicho.

Mhe. Prof. Juma amesisitiza umuhimu wa Watumishi wa Mahakama kujiona kama sehemu ya Mahakama licha ya kila mmoja kuwa na majukumu tofauti.

‘Tuna majukumu mbalimbali, lakini wote tunafanya majukumu ya pamoja. Naomba Wafanyakazi wanaosaidia au kufanikisha jukumu mama wasijione Watoto yatima kwa sababu wanafanya kazi kubwa sana. Mahakama haiwezi kufanya kazi bila uwezeshaji unaofanywa na kada ya Watumishi wengine,’ amesema.

Ameshukuru kwa maandalizi mazuri ya shughuli mbalimbali za maandalizi zilizofanikisha Kikao hicho pamoja na taarifa za utendaji kwenye maeneo kadhaa zilizowasilishwa na Viongozi wa Mahakama.

Kadhalika, Jaji Mkuu ameshukuru kwa mada nzuri zilizowasilishwa na wataalam kwenye maeneo mbalimbali ambazo zimekuwa na manufaa makubwa kwa Watumishi wa umma.  

Kabla ya kuhitimishwa kwa Kikao hicho, wajumbe walipitishwa kwenye mada tatu muhimu, ikiwemo utaratibu na maandalizi ya nyaraka kwa ajili ya mafao iliyowasilishwa na Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa PSSSF, Bw. Victor Kikoti.

Bw. Kikoti aliwaomba wajumbe wa Baraza hilo kujaza kwa usahihi kumbukumbu za mafao na kuwasilisha kwenye mamlaka husika madeni mapema, jambo litakalosaidia Mfuko kulipa mafao kwa wakati.

Wajumbe pia walipokea mada inayohusu maandalizi ya kustaafu katika utumishi wa umma iliyowasilishwa na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi.

Dkt. Shilingi aliwakumbusha wajumbe wa Baraza kuwa wasitegemee chanzo kimoja cha mapato na kujiepusha na matumizi yasiyofaa ya fedha.

Kadhalika, wajumbe wa Baraza walipokea mada inayohusu ulinganifu wa staili ya maisha namna mtumishi anavyotakiwa kuishi kabla na baada ya kustaafu iliyowasilishwa na Mwanasaikolojia maarufu, Bi. Sadaka Ahmed Gandi.

Maazimio yaliyofikiwa na wajumbe wakati wa Kikao hicho yalikuwa nafasi ya Mahakama katika maandalizi ya Dira ya Taifa 2050, kuwa Watumishi wote washiriki kikamilifu katika kutayarisha mpango mkakati mpya wa Mahakama ambao utaendana na Dira hiyo.

Wajumbe pia wameazimia kuwa kutokana na takwimu za mashauri za hivi karibuni kuonesha kuwa Mahakama za Mwanzo zina asilimia 70 ya mashauri yote nchini, ipo haja ya kuweka mkazo zaidi katika kuimarisha usimamizi wa utoaji haki katika Mahakama hizo ili kuongeza ubora wa huduma ya utoaji haki katika ngazi hiyo.

Azimio jingine ni Viongozi wa Mahakama kuendelea kufuatilia maslahi ya Watumishi na kwamba Kanda za Mahakama ambazo hazijalipa posho ya mavazi kwa Wasaidizi wa Kumbukumbu, Waandishi Waendesha Ofisi, Walinzi na Madereva zihakikishe zinalipa posho hizo ifikapo Juni, 2025.

Wajumbe pia wameazimia kuwa Mwajiri aangalie uwezekano wa kuongeza fedha katika michango ya Watumishi ili waweze kupata huduma bora ya kiafya kupitia huduma za Bima ya Afya-NIHF.

Kadhalika, wajumbe wameazimia kuwa changamoto za kimfumo zinazoendelea kujitokeza na kubainishwa katika matumizi ya Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA-zitengenezewe rejesta maalum inayoainisha changamoto, ufuatiliaji na utatuzi ili kuleta ufanisi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-katikati, akihitimisha Kikao cha Baraza la Wafanyakazi Taifa cha Mahakama ya Tanzania. Kushoto ni Katibu wa Baraza, Bw. Ezra Kyando na kulia ni Katibu Msaidizi wa Baraza, Mhe. Christina Mlwilo.


Sehemu ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- ikiwa kwenye kikao hicho.


Sehemu nyingine ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- ikiwa kwenye kikao hicho.



Sehemu nyingine ya tatu ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- ikiwa kwenye kikao hicho.



Sehemu nyingine ya nne ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- ikiwa kwenye kikao hicho.



Sehemu nyingine ya tano ya Wajumbe wa Baraza-juu na picha mbili chini- ikiwa kwenye kikao hicho.




Meneja kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ya PSSSF, Bw. Victor Kikoti akiwasilisha mada kwenye Kikao cha Baraza hilo. Picha chini ni Mwanasaikolojia Maarufu, Bi. Sadaka Ahmed Gandi.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni