Jumatatu, 7 Aprili 2025

MFUMO WA USAJILI WA TAARIFA ZA WATEJA NA MAWAKILI WABORESHA HUDUMA DIVISHENI YA BIASHARA

Na AMINA SAID, Mahakama Kuu-Divisheni ya Biashara

Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara imeendelea kuvuna mafanikio makubwa kupitia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambapo Mfumo wa Usajili wa Taarifa za Wateja na Mawakili umeleta mapinduzi katika utoaji wa huduma kwa wateja wa Mahakama hiyo.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bw. Edward Mbara, alieleza jinsi mfumo huo unavyosaidia katika ufuatiliaji na uboreshaji wa huduma.

"Kwakuwa mfumo huu unarekodi taarifa za wateja zikiwemo namba za simu, siku moja nilipitia takwimu na kupata mteja mmoja aliyekaa mahakamani zaidi ya masaa Matano, nilimpigia simu kutaka kufahamu kwanini alitumia muda mrefu, akanijibu kwamba alikuwa maktaba anajisomea nyaraka mbalimbali," alisema Bw. Mbara.

Aidha, aliongeza kuwa mfumo huo umesaidia kuongeza ufanisi kwa kuwawezesha viongozi wa Mahakama kufahamu kwa undani aina ya wateja wanaohudumiwa, jambo linalorahisisha utoaji wa huduma bora na kwa wakati.

Katika kikao hicho, Mtendaji huyo aliweka bayana vipaumbele vya Mahakama hiyo kwa robo mwaka unaofuata, ambavyo ni pamoja na Kumaliza mashauri ya mlundikano, kuboresha na kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) sambamba na kuwajengea uwezo watumishi juu ya matumizi ya mifumo Teknolojia.

Vipaumbele vingine ni kulipa stahiki za watumishi na watoa huduma pamoja na kufanya vikao vya kusukuma mashauri na vikao vya utawala

Baraza hilo pia lilihusisha uchaguzi wa Naibu Katibu wa Baraza la Wafanyakazi ambapo, Bi. Fullness Katekela na Bi. Tausi Mwambujule walichuana kuwania nafasi hiyo. Katika uchaguzi huo ulioshirikisha jumla ya wajumbe 21, Bi. Fullness alipata kura 11 na Bi. Tausi alipata kura 10. Hivyo, Bi. Fullness Katekela alitangazwa mshindi na kuchukua nafasi ya Naibu Katibu wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama hiyo.

Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Jaji Cyprian Mkeha aliwapongeza Majaji kwa kazi kubwa ya kusikiliza na kuamua mashauri kwa kasi na ufanisi mkubwa, hali iliyosaidia Mahakama hiyo kuendelea kuonesha mafanikio makubwa.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Baishara ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Cyprian Mkeha  (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza jambo wakati wa kikao cha Baraza la Mahakama hiyo kilichofanyika hivi karibuni.


Katibu wa Baraza (katikati), Bw. Justine Kilenza akichangia jambo wakati wa kikao hicho kilichofanyika hivi karibuni.

Afisa Utumishi Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara mmoja wa Wajumbe wa Baraza hilo, Bi. Adventina Kambuga akisisitiza jambo juu ya umuhimu wa kujiunga katika mfumo wa “PSSSF Kiganjani”.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara   Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Cyprian Mkeha  (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama hiyo. Kulia ni Katibu wa Baraza hilo, Bw. Justine Kilenza na kushoto ni Naibu Katibu wa Baraza, Bi. Fullness Katekela. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakiimba wimbo wa mshikamano.


Picha ya juu na chini ni Viongozi wa meza kuu wakiwa katika picha za pamoja na wajumbe wa Baraza hilo.

(Picha na ASHURA YUSUPH, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara)

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni