Ijumaa, 20 Juni 2025

JAJI KAHYOZA AFANYA MAKABIDHIANO YA OFISI MANYARA

Christopher Msagati – Mahakama, Manyara

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza amekabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Ilvin Mugeta jana tarehe 19 Juni, 2025 ikiwa ni baada ya kuhamishiwa Kituo kipya cha kazi cha Mahakama Kuu, Kanda ya Shinyanga.

Mhe. Mugeta ambaye kabla ya kuhamishiwa Manyara alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha. Katika hafla ya makabidhiano, Majaji hao walipata wasaa wa kuzungumza na watumishi pamoja na wadau wa Mahakama, ambapo Mhe. Kahyoza alitumia nafasi hiyo kuagana na Wanamanyara, huku Mhe. Mugeta akatumia wasaa huo pia kujitambulisha na kwa watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo.

Aidha, akitoa shukrani wakati wa kuagana na watumishi, Mhe. Kahyoza alisema kuwa ushirikiano alioupata toka Kanda ya Manyara usiishe mara baada ya kuondoka kwake bali uendelee kwa Kiongozi huyo mpya na hata Viongozi wengine watakaoendelea kuja kwenye Kanda hiyo.

“Leo ni siku yangu ya pekee na adimu, nalazimika kuagana na watumishi niliokuwa nao tangu mwaka 2022 ilipoanzishwa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, watumishi hawa wamenipa heshima kubwa sana. Viongozi hawawezi kufanya kazi peke yao isipokuwa kwa ushirikiano na umoja wetu,” alisema Mhe. Kahyoza.

Naye, Mhe. Mugeta alipokea kwa mikono miwili makaribisho aliyoyapata kwa watumishi wa Kanda hiyo, huku akisisitiza kuwa ofisi yake ipo wazi kwa yeyote mwenye mawazo ya kuboresha jukumu la msingi la utoaji haki. Alisisitiza kuwa yeye ni mtu wa kazi na anavutiwa zaidi na wachapakazi.

“Nashukuru kwa uongozi wa Mahakama kwa kuona kuwa mimi naweza kuendeleza kazi njema iliyoanzishwa na Mhe. Kahyoza katika Kanda hii ya Manyara, kasi ya utendaji kazi iliyokuwepo naamini tutaiendeleza na kushirikiana vema ili tuweze kuwahudumia wananchi kwa namna ambayo inastahili,” alisema Mhe. Mugeta.

Kwa upande wake, akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. Devotha Kamuzora alisema kuwa, wataendelea kutoa ushirikiano kwa Kiongozi wao mpya ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa. Vilevile Mhe. Kamuzora alimtakia majukumu mema Mhe. Kahyoza katika majukumu yake anayokwenda kuyaanza katika Kituo chake Kipya cha Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga.

Kauli hiyo iliungwa mkono Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mhe. Nenelwa Mwihambi pamoja na watumishi ambao waliongeza kuwa wapo tayari kuyapokea maelekezo toka kwa Kiongozi huyo na kuonesha ushirikiano.

Kwa namna ya pekee Wanamanyara watamkumbuka Mhe. Kahyoza kwa kuwa ndiye Jaji Mfawidhi wa Kwanza tangu kuanzishwa kwa huduma za Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara mnamo Mwezi Novemba mwaka 2022. Vilevile atakumbukwa kwa utaratibu aliouweka wa kusikiliza mashauri kwa wakati kuanzia Mahakama Kuu mpaka Mahakama za Mwanzo zilizopo katika kanda ya Manyara.


Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta  (kushoto) wakati wa makabidhiano ya kituo na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. John Kahyoza (kulia) kufuatia uhamisho wa vituo vya kazi.


Mhe. John Kahyoza anayehamia Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga akisoma taarifa ya makabidhiano ya Mahakama Kuu Kanda ya Manyara mbele ya Jaji Mfawidhi Mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta  na kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe Nenelwa Mwihambi pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara (hawapo pichani).

Mhe. Ilvin Mugeta ambaye ni Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara akitoa neno la shukrani kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda hiyo mara baada ya kukaribishwa katika kituo chake kipya cha kazi.


Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akisaini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara. 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara wakiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Ilvin Mugeta ambaye ni Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara (wa sita Kushoto), Wengine ni Jaji Mfawidhi anayeondoka Manyara Mhe. John Kahyoza (wa sita kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora (wa tano kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Nenelwa Mwihambi (wa tano kusho) na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo (wa pili kushoto).

Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Bw. Arthur Swai akitoa Neno la shukrani kwa Majaji wote katika hafla ya Makabidhiano ya Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.
Jaji Mfawidhi anayeondoka Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akimkaribisha Jaji Mfawidhi mpya anayeripoti katika Kanda hiyo Mhe Ilvin Mugeta mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.



Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akisalimiana na baadhi ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara mara baada ya kuwasili Mahakamani hapo.


















Maoni 1 :

  1. Bwana awabariki wote. Mhe, J i/c Kahyoza tunakutakia kila la kheri. Tutadumisha yote kwa weledi mkubwa. Mhe, J i/c Mugeta, karibu sana Kanda ya Manyara. Tunakuhahidi ushirikia mkubwa na kufanya kazi kwa weledi na kutekeleza maelekezo yako yote. Karibu sana .he, Jaji i/c Mugeka.

    JibuFuta