Na DOTTO NKAJA-MAHAKAMA, GEITA
Jaji wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Venance Mwakapeje jana tarehe 16 Juni,
2025 alifanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama kwa Robo ya Nne ya Mwaka 2024/25 kwa
katika Mahakama za Wilaya ya Mbogwe na Bukombe na Mahakama za Mwanzo Masumbwe na
Ushirombo.
Katika ziara hiyo
aliyoifanya kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya
Geita, Mhe. Kevin Mhina, Jaji Mwakapeje aliambatana na Naibu Msajili wa
Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa
Mahakama Kanda hiyo, Bi. Masalu Kisasila na Maofisa wengine.
Akizungumza na watumishi
mara baada ya kumaliza kusikiliza taarifa mbalimbali zilizowasilishwa, kuhusu Mahakama
hizo, Mhe. Mwakapeje aliwataka kuzingatia maadili na uadilifu katika utoaji
haki ili kuimarisha uhusiano na Watu waliopo nje ya Mahakama.
Jaji Mwakapeje
aliwahimiza Watumishi kutumia rasilimali zilizopo kuzalisha zaidi na kuimarisha
misingi ya utoaji haki na kuendelea kuyaenzi na kuyaishi maazimio ya Jaji
Mfawidhi wa Kanda hiyo katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA.
Mhe. Mwakapeje alisema, “Binafsi
sipendi kuona Mtumishi yeyote katika Kanda yetu anakuwa kikwazo katika kukuza
uwezo wa matumizi ya TEHAMA. Rai yangu ni kuiona Geita inazidi kuwa nuru ya
kimataifa katika matumizi ya Mahakama Mtandao.”
Naye Mtendaji wa Mahakama
Kanda hiyo aliwakumbusha Watumishi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa
kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu pamoja na miongozo mbalimbali inayoendelea
kutolea na Viongozi.
Aidha, alikemea vitendo
vya utovu wa nidhamu wakati wa utekelezaji wa majukumu yao na kuwataka Watumishi
wawe na upendo, heshima, hekima na ushirikiano kwani kila mtumshi ni muhimu katika
kukuza Taasisi.
Pia aliwataka kutambua
kwamba kila Mtumishi ana mchango muhimu katika mafanikio ya Kituo chake alipo
na Taasisi kwa ujumla.
“Mtumishi wa Umma hana kwao nyumbani kwake ni pale alipo. Hii ina maana kwamba Mtumishi wa Umma anatumia muda mwingi kuwa kazini, hivyo Watumishi wenzake alionao kazini ndiyo kama ndugu zake. Kwa hiyo, Watumishi tushirikiane na tuchukuliane kama ndugu,” alisema.
Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe, Mhe. Mashaka Msologone akiwasilisha taarifa fupi ya hali ya mashauri ile ya utawala na rasilimaliwatu kwa Jaji Mwakapeje.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akitoa ufafanuzi juu ya changamoto za utumiaji wa mifumo ya Mahakama.
Watumishi wa Mahakama Wilaya ya Bukombe wakiwa katika kikao kifupi na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje baada ya ukaguzi kukamilika.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Venance Mwakapeje akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Bukombe.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni