Ijumaa, 13 Juni 2025

JAJI MFAWIDHI ASISITIZA KUKAMILISHWA MIRADI YA UJENZI KWA WAKATI

Na Christopher Msagati - Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza amesisitiza kukamilishwa miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama kwa wakati ambayo yanaendelea kujengwa kwa sasa na Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara.

Mhe. Kahyoza ameyasema hayo wakati akiwa katika ziara ya Ukaguzi wa Mahakama za Wilaya ya Kiteto na Simanjiro iliyofanyika kuanzia tarehe 12 Juni 2025 hadi tarehe 13 Juni 2025.

Katika ziara hiyo Mhe. Kahyoza aliambatana na viongozi mbalimbali waliyoshiriki Ukaguzi wa maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Mahakama ya Wilaya ya Kiteto, Gereza la Wilaya ya Kiteto, Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro pamoja na miradi ya ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro na Mahakama ya Mwanzo Terrat iliyopo Wilayani Simanjiro ambayo inaendelea kwa sasa.

Akiwa katika Ukaguzi wa miradi ya Ujenzi wa Mahakama inayoendelea Wilayani Simanjiro, Mhe. Kahyoza aliwaambia Wakandarasi wahakikishe kuwa miradi hiyo ya Mahakama inakamilika mapema kwa sababu shughuli za kimahakama zinatakiwa kuanza ili wananchi wapate huduma zinazohitajika katika maeneo yao.

“Nawasihi mjitahidi kumaliza ujenzi huu mapema iwezekanavyo kwa sababu tunapaswa kuanza kuwahudumia wananchi wa Wilayani Simanjiro vilevile watumishi wa Mahakama hii wapate jengo bora zaidi kwa sababu sasa wanatumia jengo la kuazima ambalo ni dogo na halitoshi kwa mahitaji ya Mahakama na pia tuwasaidie wananchi wa Terrat waweze kupata huduma za kimahakama ambazo kwa sasa wanachelewa kuzipata kwa sababu inawapasa kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa Hamsini ili kupata huduma hizo” alisema Mhe. Kahyoza.

Naye, Mhandisi Samwel James kutoka Kampuni ya Moladi Tanzania Ltd ambayo inajenga jengo la Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro aliuahidi uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kujitahidi kukamilisha ujenzi huo mapema kwa kuwa wamepata vifaa vya ujenzi ambavyo vitafanya shughuli yao kufika mbali.

“Kwa sasa tuna vifaa vya kutosha pamoja na nguvu kazi ya kutosha, hivyo naahidi kukamilisha ujenzi huu mapema iwezekanavyo” alisema Mhandisi James.

Aidha, katika upande wa Ukaguzi wa Mahakama zinazofanya kazi kwa sasa, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo aliwasihi watumishi kutumia mifumo ya TEHAMA ambayo inatumiwa na Mahakama inarahisisha taarifa kufika kwa haraka kwa wadaawa na pia inasaidia Ofisi kupunguza matumizi ya makaratasi na gharama nyingine za uchapishaji.

“Tukiitumia hii mifumo itatusaidia sana kufikisha taarifa kwa wadaawa wetu mapema zaidi lakini pia na sisi kama Ofisi tunapunguza gharama za uchapishaji wa nyaraka mbalimbali na hivyo kuweza kusaidia kupata fedha za kufanya mambo mengine ya kimaendeleo,” alisema Mhe. Mpepo.

Mahakama Kuu Kanda ya Manyara inaendelea na zoezi la Ukaguzi wa Mahakama za chini kwa Robo Mwaka ya kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni 2025 kwa lengo la kuangalia ufanisi na utendaji kazi pamoja na kutoa maelekezo kwa watumishi wa Mahakama ambayo yatasaidia katika utoaji huduma ya haki kwa wakati.

     Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akisalimiana na Baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto alipofika Mahakamani hapo kwa ajili ya Ukaguzi.

1    Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto Mhe Boniface Lihamwike akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Wilaya hiyo kwa Mhe. John Kahyoza (hayupo pichani) ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

     Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akiwa katika picha ya Pamoja na baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto, aliyekaa upande wa Kushoto Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemed.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (wa pili kulia) akiwa na baadhi ya watu aliombatana nao katika ziara ya Ukaguzi katika Gereza la Wilaya ya Kiteto.

     Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akisalimiana na baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro alipofika Mahakamani hapo kwa ajili ya Ukaguzi.

1. Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (hayupo pichani) wakati akizungumza nao katika ziara ya Ukaguzi katika Wilaya hiyo.

Mhandisi Samwel James (wa kwanza Kulia) kutoka Kampuni ya Moladi Tanzania Ltd akitoa maelezo kuhusu Mradi wa ujenzi wa   Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro mbele ya timu ya Ukaguzi iliyoongozwa na  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara  Mhe John Kahyoza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (kushoto) akizungumza na baadhi wa wawakilishi wa Kampuni ya Pioneer Builders Company Ltd  wanashughulikia ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat iliyopo Wilayani Simanjiro.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni