Alhamisi, 12 Juni 2025

MAHAKAMA SPORTS YAKABIDHI MAKOMBE 15 KWA MTENDAJI MKUU

  • Yale iliyozoa SHIMIWI, Mei Mosi baada ya kuibuka washindi kwenye michezo mbalimbali

Na GODFREY KUSOLWA-Mahakama, Dodoma

Timu ya Michezo ya Mahakama ya Tanzania, Mahakama Sports, jana Jumatano tarehe 11 Juni, 2025 ilikabidhi kwa Uongozi wa Mahakama vikombe 15 ilivyokusanya kwa vipindi vitatu baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali iliyofanyika kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali-SHIMIWI-na Mei Mosi kuanzia mwaka 2023.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, ambaye alikuwa mgeni rasmi, alipokea vikombe hivyo na kutoa medali na vyeti kwa washindi wa michezo mbalimbali katika mashindano hayo. hafla hiyo ilifanyika kwenye moja ya Kumbi za Mikutano katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma,

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Ole Gabriel aliwapongeza wanamichezo hao walioweza kushiriki na kuibuka washindi kwenye michezo ya SHIMIWI iliyofanyika katika Mikoa ya Iringa na Morogoro na mashindano ya Mei Mosi yaliyofanyika katika Mikoa ya Arusha na Morogoro na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kukuza michezo hapa nchini.

Akizungumzia mipango ya kuwekeza katika kutambua vipaji vya michezo ndani ya Mahakama ya Tanzania, Mtendaji Mkuu aliuliza, “Hivi hatuwezi siku moja tukacheza na Timu za Simba au Yanga pale kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa?”

Aliongeza, “Maono yangu, ni kuona siku moja tunapata timu bora za kushiriki kwenye michuano mbalimbali mikubwa ikiwemo mchezo wa riadha, na mimi mwenyewe napenda kucheza mchezo wa vishale, yaani (Darts).”

Prof. Ole Gabriel aliwaambia wanamichezo hao kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahimu Hamis Juma, siku zote amekuwa muumini wa michezo kwani anaamini michezo ni uchumi na inaweza kumuongezea mtu kipato binafsi na kuchangia katika pato la Taifa kwa ujumla.

MtendajiMkuu alitumia fursa hiyo kutoa pongezi za Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya kwa mafanikio makubwa ambayo wanamichezo hao wameyapata.

“Uongozi wote wa Mahakama ya Tanzania unatambua umuhimu wa mashindano hayo kwa Watumishi wa Umma, ikiwemo wa Mahakama. Nakubali kutoa wiki moja kwa washiriki kujiandaa kabla ya mashindano, maana hilo naliweza,” alisema.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede, akizungumza katika hafla hiyo, aliushukuru uongozi kwa hatua inazochukua kuhakikisha wanashiriki kwenye mashindano mbalimbali.

Baadhi ya Washindi katika mashindano hayo walielezea siri ya mafanikio kwenye michezo kama hiyo kama vile kuzingatia nidhamu, programu ya mazoezi na kujituma kupambania Taasisi wakati wote.

Makombe 15 yaliyonyakuliwa na Mahakama Sports kwenye Mashindano ya SHIMIWI na Mei Mosi kuanzia mwaka 2023 katika Mikoa ya Iringa, Morogoro, Arusha na Singida.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akinyanyua juu moja ya makombe hayo.

Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akimkabidhi Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel moja ya makombe hayo. Kulia ni Mkurugenzi Msaididi-Utawala- wa Mahakama ya Tanzania, Steven Magoha akishuhudia tukio hilo.

'Hongera Mama' alisikika Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akimpongeza Mfukuza Upepo hatari wa Mahakama ya Tanzania, Justus Tibendelane baada ya kumvalisha nishani alizonyakua kwenye mashindano hayo. Picha chini ni Mfukuza Upepo mwingine wa Mahakama ya Tanzania, Mwajabu Mohamed Bwire

 

'Striker' refu kuliko goli, John Mapinduzi akipongezwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.


Mshindi wa Kwanza katika mchezo wa Karata, Malkia Nondo akipokea cheti cha pongezi kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.


Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akipongezwa kwa kazi nzuri ya kusimamia Timu yake.


Mchezaji mahiri wa mchezo wa Karata, Hashim Mtomondela akipokea cheti cha pongezi kutoka kwa Mgeni Rasmi.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza kwenye hafla hiyo. Picha chini ni Afisa Michezo wa Mahakama ya Tanzania Peter Macharo akimwaga sera na mipango ya ushindi.
\


Katibu wa Mahakama Sports Donald Tende akiwasilisha taarifa ya ushiriki wa mashindano kwenye hafla hiyo.


Mkurugenzi Msaidizi wa Mipango na Uchumi Gladys Quambaita akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya Mlezi wa Timu, ambaye ni Mkurugezi wa Mipango na Uchumi, Erasmus Uisso.

Wazee wa kazi kazi, wakiwa ukumbini kufuatilia yaliyokuwa yanajiri.

Kwani wewe unasemaje sasa.


Sehemu ya washindi wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa hafla hiyo-juu na picha mbili chini.



Washindi na makombe yao.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.





















 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni