- Ni wa tisa katika historia ya Mahakama tangu kupata uhuru wa Tanzania
- Aahidi
kuendelea kusimamia utoaji haki
Leo
tarehe 15 Juni, 2025 majira ya saa 4:10 asubuhi kwa mara nyingine historia ya Mahakama
ya Tanzania imeandikwa kufuatia kuapishwa kwa Jaji Mkuu wa saba Mzalendo na wa
tisa tangu kupata uhuru wa Tanzania ambaye ni Mhe. George Mcheche Masaju anayechukua
nafasi ya mtangulizi wake, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliyestaafu utumishi
wa umma.
Mhe.
Masaju ameapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan katika hafla ya uapisho iliyofanyika Ikulu- Chamwino jijini
Dodoma.
Akizungumza
mara baada ya kumuapisha Jaji Mkuu mpya, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa,
matarajio ya Watanzania ni kuona kuwa Mahakama inaendelea zaidi ya ilipo kwa sasa.
“Majengo,
watenda kazi, mifumo na yote yaliyopo mahakamani yanahitaji kuendelezwa na Jaji
Mkuu Mstaafu amesema vizuri kwamba, bado kuna miradi inaendelea, mingine fedha
zake zipo, mingine fedha zake za kutafutwa lakini nikuhakikishie ushirikiano wa
Serikali kwenye kukamilisha miradi hii,” amesema Rais Samia.
Mhe.
Dkt. Samia ameeleza kuwa, matarajio ya Watanzania pia ni kuona Mahakama
inaendelea kusimamia haki ndani ya nchi na nje ya nchi, hivyo anatarajia kuwa
jukumu hilo kubwa litasimamiwa vyema na Jaji Mkuu huyo.
“Katika
kusimamia haki, Siku ya Sheria ya mwaka huu nilisema kuwa kazi yenu ni
kusimamia haki. Kazi ya kutoa haki ni kazi ya Mungu lakini kwa duniani kazi ya
haki ni kazi ya Majaji, hivyo ni muhimu kusimamia haki kwa misingi
tuliyojiwekea,” amesisitiza Rais Samia.
Ameongeza
kuwa, Serikali itafanya kila linalowezekana kuendeleza ufanyaji kazi wa
Mahakama kama alivyoahidi wakati analihutubia Bunge kwa mara ya kwanza tarehe
22 Aprili, 2021 ambapo alisisitiza kuwa, Serikali itaendelea kufanya hivyo ili
Mahakama ya Tanzania isimame vizuri na iwe ni moja katika Mihimili yenye hadhi
duniani.
Kadhalika,
Mhe. Dkt. Samia ametoa rai kwa Jaji Mkuu mpya kuendelea na utekelezaji wa
mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Haki Jinai ili kuendelea na maboresho ya sekta ya sheria nchini.
“Nenda
kaangalie ni maeneo gani tumetekeleza na ambayo bado hatujatekeleza na tuone
jinsi tutakavyoendelea kuyatekeleza ili haki isimame vyema ndani ya nchi yetu,”
amesema Rais Samia huku akiongeza kwa kumpongeza Jaji Mkuu Mstaafu kwa
kuhitimisha kazi hiyo bila makandokando.
Akizungumza
baada ya uapisho, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju amemshukuru
Rais Samia kwa kumuamini na kumuona anafaa kushika nafasi hiyo ya kuongoza
Mhimili wa Mahakama ya Tanzania.
“Ninachoweza
kusema tu mbele yako Mheshimiwa ni kwamba, sisi kazi yetu Mhimili wa Mahakama
ni kutoa haki na Katiba katika Ibara ya 107A na B imetueleza kanuni
zinazotuongoza na sheria zote zinazotungwa huwa zina mambo matatu zinazungumza
maslahi ya haki, maslahi ya umma na maslahi ya Taifa,” amesema Mhe. Masaju.
Jaji Mkuu amesema kuwa, katika kutoa haki kuna
kanuni ambazo ni mwongozo na mojawapo ya kanuni hizo ni kutenda haki kwa watu wote
bila kujali hali ya mtu kiuchumi na kijamii lakini pia kuharakisha utoaji haki
isipokuwa kama kuna sababu ya msingi lakini pia kutofungwa na masharti ya
kiufundi yanayoweza kusababisha haki kutotendeka kwa wakati.
Mhe. Masaju ameeleza kuwa, ataenda kushauriana na viongozi wenzake wa Mahakama
ili kuona ni namna gani zaidi ya kuwafikia wananchi kwa kuwa Mahakama imelenga
kuwasaidia wananchi (Citizen Centric Justice Service Delivery).
Amesema
kuwa, ili kuendelea kutoa huduma kwa wananchi, atajadiliana na wenzake kuona
uwezekano wa kuwa na huduma za Mahakama ya Rufani kwa kila mkoa ili kurahisisha
upatikanaji wa haki.
Hafla hiyo imehudhuriwa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Majaji wa Mahakama ya Rufani, Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Dkt. Moses Kusiluka, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro.
Wengine waliohudhuria ni pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher
Mohamed Siyani, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah, Mawaziri,
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante ole Gabriel, Msajili Mkuu
wa Mahakama, Mhe. Eva Kiaki Nkya pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama na
Serikali.
Aidha,
baada ya hafla ya uapisho, Jaji Mkuu mpya aliambatana na Jaji Mkuu Mstaafu hadi
Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania iliyopo Mtaa wa Tambukareli jijini Dodoma
ambapo alikaribishwa na watumishi wa Mahakama wakiongozwa na Mtendaji Mkuu na Msajili Mkuu wa Mahakama.
Kadhalika,
Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amemkabidhi rasmi Ofisi Jaji
Mkuu mpya ambapo ameahidi kumpatia ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu
yake.
Jaji Mkuu mpya wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju.
Viongozi wa Serikali, Bunge na Mahakama pamoja na wageni wengine mbalimbali waliohudhuria katika hafla ya uapisho wa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. George Mcheche Masaju.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na familia ya Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma. Wa pili kulia ni Mwenza wa Mhe. Prof. Juma, Bi. Marina Juma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni