Jumapili, 15 Juni 2025

USHIRIKIANO WA MIHIMILI HAUINGILII UHURU WA MAHAKAMA; JAJI MKUU MSTAAFU

Na INNOCENT KANSHA - Mahakama

Mafanikio ya maboresho yaliyopatikana ndani ya Mahakama ya Tanzania yanatokana na ushirikiano madhubuti baina ya Mhimili ya Serikali na Bunge, ushirikiano ambao unalenga kuimarisha ustawi wa utoaji haki na kujenga misingi imara ya haki kwa wananchi.

Akitoa neno fupi la shukurani wakati wa hafla ya Uapisho wa Jaji Mkuu Mpya wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju leo tarehe 15 Juni, 2025 katika Viunga vya Ikulu Chamwino jijini Dodoma, Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema, mashirikiano ya Mihimili hiyo ya Serikali na Bunge yameleta mapinduzi makubwa ndani ya Mahakama kwani mihimili hiyo ndiyo inayosimamia rasilimali zinazotumiwa na Mahakama kujenga mifumo imara na kuboresha katika nyaja ya utoaji haki.

“Watu wengi wanadhani ule ushirikiano wa mihimili mengine unaingilia uhuru wa Mahakama siyo kweli, kwa sababu Mahakama inachokitafuta katika ushirikiano ni rasilimali ya Taifa ambayo inasimamiwa na mihimili mingine. Siku zote ukipata wasaha wa kukaa na viongozi wa mihimili mingine lazima ujadili mambo yenye maslahi makubwa kwa ajili ya manufaa ya muhimili wa Mahakama,” ameongeza Jaji Mkuu Msataafu.

Aidha, Jaji Mkuu Mstaafu amemshauri Mhe. Masaju kuwa, siku zote afuatilie hotuba za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwasababu kuna ahadi fulani huwa anazitoa zilizojengeka katika msingi wa utoaji haki unaweza kuzitumia kama silaha.

“Mimi nakumbuka tarehe 22 mwezi wa nne mara baada ya kuapishwa kuchukua hatamu ya kuiongoza nchi alihutubia Bunge la 12 na kuna maneno ambayo aliyasema kuhusu Mahakama siku zote huwa natembea nayo mfukoni kwa sababu mara zote nikikutana naye huwa namkubusha juu ya ahadi aliyotoa na ndiyo silaha ambayo Mtendaji Mkuu akienda hazina uonesha Mhe. Rais aliahidi hivi,” amenukuliwa Jaji Mkuu Mstaafu huyo.

Akitoa nukuu ya Mhe. Rais, Mhe. Prof. Juma alisema tutashirikiana pia na Mhimili wa Mahakama katika kuimarisha mifumo ya utoaji haki, ikiwemo kuendelea kujenga miundombinu ya Mahakama, kuongeza idadi ya Majaji na Mahakimu na kukuza matumizi ya TEHAMA ili kuongeza kasi ya usikilizaji wa kesi na uwekaji wa kumbukumbu.

Jaji Mkuu Mstaafu ameongeza kuwa, Mhe. Rais anaweza kuwa na shahuku ya kuiimarisha mfumo wa utoaji kwani anajua kuwa, maendeleo yoyote ya kiuchumi hayawezekani bila ya kuwa na Mahakama huru, bila kuwa na utawala wa sheria. Hivyo Mhe. Rais ni mdau muhimu sana na ndiyo maana ukiangalia programu za maboresho zinajaribu kujiengesha kwenye dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025 kwa sababu dira hiyo ina ahadi ya rasilimali ambazo Mpango Mkakati wa Mahakama ulijiengesha huko ili kunafaika na rasilimali hizo.

Vilevile, Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, Mhe. Rais anatambua kuwa, utoaji wa haki ni sehemu muhimu sana ya maendeleo ya nchi, kwamba ukiwa na Mahakama imara inayofuata sheria na taratibu inaleta utulivu ambao unahitajika katika shughuliza za kujenga uchumi ulioimara na kustawisha Taifa.  

Sheria ya Usimamizi wa Mahakama sheria namba nne (4) imesaidia sana kwani imeimarisha uhuru wa Mahakama kwani Serikali na Bunge ndiyo vyombo vinavyosimamia rasilimali, sasa basi Mahakama inazifikia hizo rasilimali kupitia Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Msajili Mkuu wa Mahakama kwa sababu mara nyingi Jaji au Msajili akionekana anazunguka zunguka Hazina watu wengine wanadhani uhuru wa Mahakama upo mashakani.

Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, lakini akionekana Mtendaji Mkuu wa Mahakama akizunguka hazina na kufanikisha yote aliyokuwa anatafuta utaweza kuona kwamba hiyo sheria ya usimamizi wa Mahakama ni msingi imara sana ambao umeiwezesha Mahakama kuwa huru zaidi, na vilevile kuweza kupata rasilimali kutoka mfuko mkubwa wa Serikali  

“Nakushuru sana Mhe. Rais pamoja na kunipa mazingira ya kufanya kazi kwa utulivu ila uwezeshaji ulikuwa ni mkubwa sana, uwezeshaji ambao ulileta utulivu na utivu wa kipekee katika Mahakama na hilo ni somo ambalo nitamuomba Jaji Mkuu Mpya Mhe. George Mcheche Masaju kwamba usiache kuangalia jicho la Mhe. Rais kwasababu yeye ni mdau mwezeshaji,” amesema Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Prof. Juma.

Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, maboresho yote yaliyopatikana na kuyaona siyo nguvu ya Prof. Juma ya uwezeshaji ama nguvu ya Majaji, ni nguvu ya uwezeshaji kutoka Serikali Kuu chini ya Mhe. Dkt. Samia ambaye amekuwa mara zote akitaka Mahakama kutatua kero za wananchi kupitia Mahakama.

“Nakuhakikishia kwamba, Uongozi mzima wa Mahakama tulikaa tukajadiliana tukasema kwamba tutakupa utiifu, unyenyekevu wa hali ya juu ili kukuwezesha wewe utuongoze ili tuweze kufikia malengo ya utoaji wa haki kwa sababu haya malengo ni endelevu viongozi wote wa Mahakama waliopo mbele yako ni viungo na wako tayari kukupa ushirikiano ukiwa na jambo lolote ambalo ni la nje ya mhimili hawa viungo watakupa ushirikiano mkubwa kulitatua,” ameongeza Mhe. Prof. Juma.

Aidha, Mhe. Prof. Juma akatoa rai kwa Jaji Mkuu mpya Mhe. Masaju kwamba, jicho lake lazima likamate jicho la Mhe. Rais kwa kuangalia anafanya nini na je hicho anachokifanya kitasaidiaje Mahakama kwa sababu Mhe. Rais ni mdau muhimu sana bila uwekezaji wake hakuna chochote Mahakama inaweza kukifanya, kweni ndiye anayeongeza Majaji, Mahakimu, rasilimali fedha za miundombinu na watumishi waoisaidia Mahakama kutenda haki.

Aidha, Itakumbukwa kuwa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania wa sita (6) Mzalendo mnamo mwaka 2017 na aliyekuwa Rais wa Awamu ya tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na kuhudumu katika cheo hicho kuanzia 2017 hadi 2025.

Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa nasaa zake wakati wa hafla ya kumwapisha Jaji Mkuu mpya wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju leo Tarehe 15 Juni, 2025 Ikulu Chamwino jijini Dodoma 

Jaji Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju akila kiapo Ikulu Chamwino jijini Dodoma kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania leo tarehe 15 Juni, 2025 jijini Dodoma mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye hafla ya uapisho wa Jaji Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju Ikulu Chamwino jijini Dodoma akiwa wakati wa uapisho huo.

Sehemu ya Viongozi wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama wakiwa kwenye hafla ya kumwapisha Jaji Mkuu wa Tanzania mpya Mhe. George Mcheche Masaju wakiwa Ikulu Chamwino jijini Dodoma akiwa wakati wa uapisho huo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma Ikulu Chamwino jijini Dodoma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju (kulia) Ikulu Chamwino jijini Dodoma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju (kushoto) na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma Ikulu Chamwino jijini Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na familia ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju mara baada ya kuapishwa kwake Ikulu Chamwino jijini Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na familia ya Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma Ikulu Chamwino jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju na  Majaji wa Mahakama ya Rufani  ya Tanzania.
Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju pamoja Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju (kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma mara ya makabidhiano ya Ofisi kwenye jengo la Makao Makuu jijini Dodoma leo tarehe 15 Juni, 2025.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Mcheche Masaju (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya kuwasili kwenye chumba maalumu cha kupumzikia wageni alipowasili kwenye jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma mara baada ya uapisho wake wa kushika wadhiwa wa Jaji Mkuu wa Tanzania.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)  


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni