Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea
Mahakama Kanda ya Songea inaendesha
mafunzo maalum kuwajengea uelewa Mahakimi na Wadau mbalimbali kuhusu kuepuka
kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono.
Mafunzo hayo ya siku tatu
yalifunguliwa jana tarehe 24 Juni, 2025 na Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe.
James Karayemaha, yakikutanisha
Mahakimu Wakazi, Waendesha Mashtaka na Maafisa Ustawi wa Jamii.
Mafunzo hayo ni endelevu,
yakiwa yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Irish Rule of Law International (IRLI),
kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania.
Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea
uwezo washiriki katika kushughulikia mashauri ya ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia athari za kiakili na kihisia
kwa waathirika, sambamba na kuheshimu haki za watuhumiwa.
Katika hotuba yake ya
ufunguzi, Mhe. Karayemaha alisisitiza Wanasheria, Polisi na Mahakama kuwatendea
ubinadamu na heshima waathirika wanapofikishwa mbele yao na kuheshimu
waathirika wa ngono na unyanyasaji kijinsia pale kesi au mashauri
yanapofikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni Jaji
wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe Victoria Nongwa pamoja na Hakimu
Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga. Wapo pia waratibu wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi
Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Goodluck Ndimbo pamoja na Patric Lipiki
kutoka IJA ambao ndio watakaoongoza washiriki kupitia mijadala na mafunzo ya
vitendo yenye kuhusisha uzoefu wa kiutendaji.
Mafunzo haya yatagusa maeneo mbalimbali muhimu ikiwemo: uelewa wa athari za kiakili na kihisia
kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, mbinu rafiki na salama za kuwauliza maswali
mashahidi wa aina hiyo, ushirikiano baina ya Taasisi katika kusaidia
mashahidi waliopo katika mazingira magumu na mizania ya kulinda haki za
waathirika sambamba na zile za watuhumiwa.
Washiriki watapata fursa ya kujadili
matukio halisi, kushiriki mazoezi ya vitendo, na kuibua maeneo yanayohitaji uboreshaji
wa kitaasisi, kujifunza kwa pamoja na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa
maarifa watakayoyapata kazini.
Mafunzo hayo yamekuwa sehemu ya
jitihada za Mahakama ya Tanzania kuboresha mifumo ya utoaji haki ili iwe
jumuishi, yenye huruma na inayowajali wahitaji wa huduma za haki, hasa kutoka
makundi yaliyo hatarini.
Chuo cha IJA na IRLI wanatarajia kufanya tathimini ya
utekelezaji wa mafunzo hayo ili kupima mafanikio yake na kuchangia uboreshaji wa
muda mrefu katika upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na
kingono.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe.
James Karayemaha akitoa hotuba
wakati wa ufunguzi wa mafunzo.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe Victoria Nongwa akiwa katika uwezeshaji wa mafunzo.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga akiwa katika uwezeshaji wa mafunzo.
Sehemu ya wawakilishi wakifuatilia mafunzo hayo.
Picha ya pamoja ya washiriki wa mafunzo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni