· Aziagiza Tanesco, Mamlaka ya Maji kutatua changamoto za Maji na Umeme
Na ALLY RAMADHANI – Mahakama
Katavi
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko, ameitaka Mamlaka
ya Maji na Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) mkoani humo kutatua changamoto za
maji na umeme kwenye eneo la mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha
Utoaji Haki Mkoa wa Katavi ili mradi huo ukamilike kwa wakati.
Akizungumza wakati alipotembelea mradi wa ujenzi wa jengo
hilo la Mahakama, Mkuu huyo wa Mkoa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya
Maadili ya Maafisa Mahakama mkoa wa Katavi alisema jengo hilo linalojengwa na Kampuni
ya M/s AZHAR Construction Co. Ltd. linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi
mitatu mpaka minne ijayo.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa alisema ujenzi wa Kituo hicho hauna
budi kukamilishwa kwa kwa wakati na kwa
viwango na ubora uliokusudiwa kwa mujibu wa mkataba wa ujenzi wa jengo hilo.
“Kukamilika kwa Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Katavi, kutasogeza
huduma za Mahakama karibu zaidi na wananchi na kupunguza kwa kiasi kikubwa adha
wanayopata ya kutoka Mkoa wa Katavi Kwenda Sumbawanga mkoani Rukwa kufuata
Huduma za Mahakama Kuu, ”alisema Mkuu wa Mkoa.
Akitoa taarifa ya maendeleo ya mradi wa ujenzi wa jengo hilo kwa
Mkuu wa mkoa, Msimamizi wa Mradi huo Mhandisi Victor Vedasto Ntungamo, alisema
mradi huo umefikia asilimia 57 na kwa upande wa jengo umefikia asilimia 60. Aliongeza kuwa mradi huo unahusisha
sehemu tatu ambazo ni jengo Kuu, eneo la nje (uzio, mgahawa, chumba cha ulinzi)
pamoja na Manzari ( Landscaping).
Aidha, Mhandisi huyo alimweleza Mkuu wa Mkoa wa Katavi
kuwa mradi huo unakabiliwa na changamoto ya kukosekana kwa umeme na maji ambazo
kwa kiasi kikubwa zinachangia kupunguza kasi ya ujenzi wa jengo hilo.
Nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa
Mahakama ya Tanzania inasisitiza Utoaji Haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania
inatekeleza mpango huu kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza
huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi
itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hii.

Mhandisi Victor Ntungamo, akitoa maelezo kuhusu maendeleo
ya mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Katavi
kwa Mkuu wa mkoa huo Mhe. Mwanamvua Mrindoko.
(Habari hii Imehaririwa na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni