Alhamisi, 17 Julai 2025

JAJI MUGETA ASISITIZA UPENDO NA USHIRIKIANO MIONGONI MWA WATUMISHI

Na. Christopher Msagati- Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta amesisitiza upendo miongoni mwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara. Mhe Mugeta ameyasisitiza hayo alipokuwa katika ziara ya kuzifahamu Mahakama zilizopo katika Mahakama Kuu Kanda ya Manyara hivi karibuni.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mugeta aliambatana na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara ambao ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo, pamoja na Mtendaji wa Mahakama Bi. Nyanzobe Hemed.

Akiongea na watumishi kwa nyakati tofauti katika vituo vyao Mhe. Mugeta aliwakumbusha watumishi waendelee kufanya kazi kwa kupendana na kushirikiana ili kusaidiana kutimiza malengo yaliyokusudiwa.

“Hakuna mtu ambaye ananufaika endapo atamchukia mtumishi mwenzake na kumfanyia visa ambavyo vitamsababisha afukuzwe kazi, naomba mjue kuwa tunaishi kwa kutegemeana kila mmoja. Kwa sababu hizo hatuna haja ya kuchukiana katika hizi kazi. Nawasihi tupendane na kushirikiana vema na malengo yetu yatatimia ipasavyo” alisema Mhe. Mugeta.

Aidha, Mhe. Mugeta alipita katika Mahakama za Wilaya Mbulu, Hanang, Kiteto pamoja na Simanjiro. Vile vile aliweza kupita katika Mahakama za Mwanzo Endagkot, Dongobesh na Haydom zilizopo wilayani Mbulu pamoja na Mahakama za Mwanzo Bassotu na Katesh zilizopo wilayani Hanang. Aidha, Mhe. Mugeta aliweza kukagua miradi ya Ujenzi wa Mahakama zinazojengwa ambazo ni Mahakama za Wilaya Mbulu, Hanang, Simanjiro pamoja na Mahakama ya Mwanzo Terrat iliyopo Wilayani Simanjiro.

Kwa upande mwingine, Mhe. Mugeta aliweza kuwasisitiza watumishi kujikita katika matumizi sahihi ya rasilimali zilizopo kwa ubunifu ili kupata matokeo yanayotarajiwa.

“Ni kweli natambua changamoto ya uhaba wa bajeti pamoja na watumishi kwa kada tofauti. Rasilimali hazijawahi kutosha hata siku moja popote pale, kwa changamoto hii tuliyonayo inatupasa kuwa wabunifu na kutanguliza vipaumbele katika utendaji kazi wetu na hapo ndipo tutafanikiwa” alisema Mhe. Mugeta.

Akisoma Taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro Mhe. Charles alimuomba Mhe. Mugeta kuzungumza uongozi wa ngazi ya juu ili Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro wapate majengo yanayojitosheleza kwa sababu hali ya Majengo iliyopo sasa hairidhishi.

“Mheshimiwa Jaji, Wilaya yetu ya Simanjiro haina jengo hata moja ambalo linamilikiwa na Mahakama, hivyo tunaomba ukatusemee katika ngazi za juu zaidi tupate majengo yetu kwa sababu majengo yote yanayotumika sasa yameazimwa Serikali za Mitaa, tunaona kuna juhudi za kumalizia ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro lakini pia tunaomba Mahakama za Mwanzo pia zitazamwe” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mugeta aliweza kutembelea Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Kiteto ambapo alipokelewa na mwenyeji wake Mkuu wa Wilaya hiyo Mheshimiwa Remidius Mwema Emmanuel, ambaye aliahidi kutoa ushirikiano utakaohitajika na Mahakama ya Wilaya ya Kiteto kwa lengo la kutoa huduma zinazotakiwa kwa wananchi.

Hiyo ni ziara ya kwanza iliyofanywa na Mhe. Mugeta katika kuzifahamu Mahakama zilizopo katika Kanda ya Manyara tangu alipohamishiwa katika Kanda hiyo akitokea Mahakama Kuu Kanda ya Arusha kwa kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Jaji Mfawidhi Mhe. John Kahyoza ambaye alihamishiwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga mwanzoni mwa Mwezi Juni mwaka 2025.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Simanjiro Mhe Charles Uisso akimtambulisha mbele ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta alipofanya ziara Mahakamani hapo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama  Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akipokea maelezo juu ya hatua za mradi wa ujenzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Terrat wilayani Simanjiro kutoka kwa Msimamizi wa mradi huo Mhandisi Magreth Kabepela anayeiwakilisha Kampuni ya Pioneer Builders Company Ltd.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (wa nne kushoto) Pamoja na msafara wake akiwa katika picha ya Pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto alipofanya ziara Mahakamani hapo.




Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Haydom Mhe. Zena Mgalula (aliyenyoosha mikono) akimuonesha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Manyara Mhe. Ilvin Mugeta Mazingira ya Mahakama hiyo katika ziara iliyofanywa Mahakamani hapo. Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe Bernard Mpepo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbulu (hawapo pichani) alipokuwa katika ziara wilayani hapo. Kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe Bernard Mpepo, na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemed 



Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (wa tatu kutoka kushoto) Pamoja na msafara wake akiwa katika picha ya Pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Bassotu iliyopo Wilayani Hanang alipofanya ziara Mahakamani hapo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Hanang Mhe. Arnold Kileo akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Mahakama hiyo mbele ya  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta wakati wa ziara iliyofanywa Wilayani hapo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (wa nne kushoto) Pamoja na msafara wake akiwa katika picha ya Pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto alipofanya ziara Mahakamani hapo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Maoni 1 :

  1. Hongera sana Jaji i/c kwa ziara yako kwani kutembelewa na bosi ni faraja.

    JibuFuta