Jumatatu, 14 Julai 2025

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA, MKURUGENZI WA KAMPUNI YA MASUALA YA MIFUMO WAKUTANA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mkurugenzi wa Biashara wa Kampuni ya Masuala ya Mifumo kutoka Italia, Bw. Franco Martino leo tarehe 14 Julai, 2025 amemtembelea Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na kufanya naye mazungumzo mafupi yenye lengo la kuendeleza ushirikiano kwenye maeneo yanayohusu mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA].

Bw. Franco amekutana na Prof. Ole Gabriel katika ofisi ndogo iliyopo kwenye jengo la Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri, Mhe. Desdery Kamugusha, Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Enoc Kaleghe na Wataalam wengine kutoka Mahakama ya Tanzania na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Mkurugenzi huyo kutoka Kampuni ya Almawave amekutana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ili kuendelea kukubaliana kuhusu namna gani ya kuweza kuendeleza mahusiano ya kibiashara kuhusu Mfumo wa Tafsiri na Unukuzi [Translation and Transcription Software-TTS].

Mfumo wa TTS unasaidia kupunguza jukumu kubwa la Majaji na Mahakimu kuandika mienendo ya mashauri au hata kutayarisha nakala za hukumu kwa mkono.

Ikumbukwe kuwa Mei 2022, Mahakama ya Tanzania iliingia mkataba na kampuni hiyo kwa ajili ya kuuziwa mifumo ya tafsiri na unukuzi.

Hivyo Bw. Franco amekutana na Prof. Ole Gabriel ili kupitia kwa pamoja muhtasari wa mambo gani mahsusi na muhimu kwa ajili ya kuendelea kuboresha.

Kadhalika, Mkurgenzi huyo amekuja kuiomba Mahakama ya Tanzania kuona jinsi gani inaweza kuendelea kuhabarisha Taasisi nyingine ambazo zinaweza kuhitaji kutumia mifumo kama hiyo ili waweze kuitumia.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania amemhakikishia Mkurugenzi huyo ushirikiano wa kutosha na kuomba mafunzo endelevu kwa Wataalam wa ndani na pia watumiaji wa mfumo wa TTS, hususan Majaji, Naibu Wasajili na Mahakimu ili matumizi ya mfumo huo yaende sambamba na mabadiliko yanayofanyika mahakamani.

‘Tungetamani siku za mbele watalaam wetu wa ndani hususan wale wa TEHAMA chini ya Mkurugenzi wao, Bw. Enoc Kaleghe waweze kuelewa na kutambua jinsi gani ya kusimamia na kubuni uboreshaji katika mifumo hii,’ amesema.

Prof. Ole Gabriel amemshukuru kwa kipekee Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye kwa hakika ameridhia na amekuwa akitoa fedha za kutosha kwa ajili ya kuboresha mifumo ya TEHAMA.

Ameeleza kuwa mifumo ya TEHAMA ikiboreshwa hushajiisha kasi na ubora wa utoaji wa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Kadhalika, Mtendaji Mkuu amemshuku Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju kwa usimamizi wake anaoendeleza matumizi ya TEHAMA kwenye shughuli za kimahakama.

Ametoa wito kwa Watanzania kuwa tayari kuendana na mabadiliko yanayoendelea ndani ya Mahakama ya Tanzania kwa ajili ya matumizi ya TEHAMA kwani zama za kutuma karatasi na mifumo ya zamani, imepitwa na wakati na Mahakama inazidi kwenda na teknolojia ya kisasa.

Mkurugenzi wa Biashara wa Kampuni ya Masuala ya Mifumo kutoka Italia, Bw. Franco Martino [kushoto] akisalimiana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel walipokutana leo tarehe 14 Julai, 2025 jijini Dar es Salaam.



Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [kushoto] akimkaribisha ofisini kwakeMkurugenzi wa Biashara wa Kampuni ya Masuala ya Mifumo kutoka Italia, Bw. Franco Martino. Picha chini ni Ofisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Athman Kikwete.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [juu na chini] akizungumza na wageni wake [picha ya pili chini].


Mkurugenzi wa Biashara wa Kampuni ya Masuala ya Mifumo kutoka Italia, Bw. Franco Martino [katikati] akisisitiza jambo kwenye mazungumzo hayo. Wengine ni Ofisa kutoka Wizara ya Mambo ya  Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Athuman Kikwete [kulia] na Bw. Abdi Zagar ambaye aliambatana na Mkurugenzi huyo.

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri, Mhe. Desdery Kamugusha [kulia] na Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Enoc Kaleghe [kushoto] na Wataalam wengine kutoka Mahakama ya Tanzania wakifuatilia kwa karibu mazungumzo hayo. Picha chini mazungumzo yakiendelea.




Picha ya pamoja baada ya mazungumzo.

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni