Jumatano, 16 Julai 2025

UWEKAJI MAZINGIRA SALAMA KWA WAFANYAKAZI SI HIARI BALI NI LAZIMA; JAJI KIONGOZI

Na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ametoa ushauri kwa waajiri wote nchini kuhakikisha wanaweka mazingira salama kwa wafanyakazi wao ili kuepusha hatari za kiafya mahali pa kazi.

 

Akizungumza leo tarehe 16 Julai, 2025 jijini Mwanza wakati akifungua Mafunzo kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Mhe. Dkt. Siyani amesema, usalama na afya kazini si suala la hiari bali ni haki ya msingi kwa kila mfanyakazi.

 

Ili kusema kwamba mfanyakazi ana mazingira salama, ni lazima mazingira hayo yawe na mguso chanya kwa mwili, akili na hisia zake. Mazingira ya kazi yanayogusa sehemu hizi humfanya mfanyakazi aweze kutoa huduma bora, kuwa na morali ya juu na kuchangia kwa ufanisi zaidi maendeleo ya taasisi na taifa kwa ujumla,” amesema Jaji Kiongozi.

 

Amesema kuwa, mazingira salama ya kazi si tu yanamlinda mfanyakazi dhidi ya ajali na magonjwa, bali pia yanachangia katika kuongeza tija, ubunifu na mshikamano miongoni mwa watumishi hivyo ni muhimu pia kuhakikisha wafanyakazi wanaelewa kwa mapana mantiki na umuhimu wa afya na usalama kazini.

 

Akizungumzia kuhusu Sekta ya Haki, Mhe. Dkt. Siyani ameongeza kwamba, Dhana ya Haki Kazi haiwezi kutenganishwa na dhana ya usalama na afya mahala pa kazi (Occupational Safety and Health).

“Hizi ni dhana mbili zinazoshikamana na hakuwezi kuwa na dhana moja bila nyingine. Dhana ya Haki Kazi ni pana, na inajumuisha ujira wa haki, usawa kazini, ushiriki wa wafanyakazi katika uamuzi, fursa za maendeleo, pamoja na mazingira salama na yenye afya. Mazingira salama ya kazi yanampa mtumishi hali ya utulivu, ujasiri wa kufanya kazi kwa bidii na uwezo wa kutoa huduma zenye viwango vya juu,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Kwa upande mwingine, Jaji Kiongozi amesema, mazingira hatarishi huzaa hofu, huzuni, magonjwa, ajali, changamoto za afya ya akili na hata vifo, mambo ambayo huvunja misingi ya haki kazi.

Kama nilivyotangulia kusema, suala la usalama na afya mahala pa kazi sio hiari, bali ni wajibu wa waajiri. Hivyo basi, waajiri, ikiwemo serikali wanapaswa kuhakikisha uwepo wa mazingira salama ya kazi na kuelimisha wafanyakazi juu ya namna wanavyoweza kushiriki ili kufaidika na kudumisha mazingira hayo,” ameeleza Mhe. Dkt. Siyani.

Kwa upande mwingine, Jaji Kiongozi amewakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa, katika dunia inayoendelea kubadilika kwa kasi, ni vema kuendana na maendeleo yanayoletwa na Mapinduzi ya Nne ya Viwanda (Fourth Industrial Revolution) yanayoendeshwa na teknolojia kama Intaneti ya Vitu, Akili Unde, Ukusanyaji wa taarifa na vitu kujiendesha vyenyewe (Automation).

 

Ninaamini kuwa, uelewa wa teknolojia hizi si anasa, bali ni hitaji la msingi kwa taasisi yoyote inayotaka kusalia hai na yenye ushindani katika enzi hizi za kidigitali,” amesema Mhe. Dkt. Siyani.

 

Ameongeza kwa kusema kuwa, “pamoja na mambo mengine, kwa siku mbili hizi mtapata wasaa wa kujifunza namna ya kulinda faragha ya taarifa za kazi, matumizi ya TEHAMA kwa ajili ya kurahisisha kazi na kuwa na uelewa juu ya athari za kijamii na kisaikolojia zinazotokana na matumizi ya mifumo ya kidijitali mahala pa kazi. Hili ni jambo la muhimu sana katika zama hizi.”

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina amesema, nguzo ya tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania unaoishia mwaka huu 2025, katika utekelezaji wake inalenga pamoja na mambo mengine ushirikishwaji wa wadau. 

“Katika kutekeleza hayo, Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali wa haki kazi.  Wakati huu, tumeshirikiana na OSHA katika kuhakikisha watumishi wa Mahakama na wadau wetu wengine wanapata elimu juu ya haki kazi na usalama mahali pa kazi,” amesema Mhe. Dkt. Mlyambina.

Jaji Mfawidhi huyo amesema, wamefanya hivyo kwa kutambua kuwa bila usalama mahali pa kazi hakuna maendeleo endelevu kwa watumishi kutokana na vihatarishi mbalimbali mahali pa kazi vinavyoweza kuhatarisha maisha ya wafanyakazi na kupunguza au kudhoofisha nguvu kazi ya taifa na kufanya taifa lisifikie maendeleo endelevu.

“Nipende kuwashukuru kwa kipekee OSHA kwa kuonyesha utayari kufanya kazi na sisi katika kusimamia haki kazi ikiwemo usalama mahali pa kazi, mafunzo hayo ni ya tatu kufanya, tulianza mafunzo ya kwanza kwa watumishi wenye ulemavu kutoka ndani na nje ya mahakama mwezi Desemba, 2024 Jijini Dodoma,” amesema Mhe. Dkt. Mlyambina.

Ameongeza kuwa, mafunzo ya pili yalifanyika Jijini Dodoma mwezi Aprili mwaka huu na yalihusisha watumishi kutoka Kanda za Dodoma, Kigoma Tabora na Singida. Mafunzo hayo yalihudhuriwa na jumla ya watumishi 70 walinufaika na mafunzo hayo.

Aidha, Jaji Mfawidhi amesema kwamba, mafunzo ya awamu hii yanayofanyika jijini Mwanza yamegawanywa katika makundi mawili yaani kundi la viongozi washiriki 110 na kundi la watumishi wasaidizi wa viongozi washiriki 90.  

Baada ya hafla ya uzinduzi wa mafunzo hayo kumefanyika tukio la utiaji saini kwa Hati ya Ushirikiano (Memorandum of Understanding) kati ya Mahakama ya Tanzania na OSHA yenye lengo la kufanya mafunzo kwa pamoja kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka miwili.

Makubaliano hayo yanalenga kuimarisha uelewa wa Sheria ya Afya na Usalama Kazini na kanuni zake, kuongeza uwezo wa kushughulikia migogoro ya kazi, kuendeleza utekelezaji wa Sheria na Kanuni za Kazi na kutilia mkazo sheria zinazosimamia ustawi wa wafanyakazi.

Amesema, Hati hiyo ya mashirikiano imegawanya mafunzo hayo kwa kanda mbalimbali. Mafunzo hayo pia yatajumuisha mafunzo ya watumishi wenye ulemavu mara moja kwa mwaka.

Mhe. Dkt. Mlyambina ameongeza kuwa, utekelezaji wa makubaliano hayo utatimizwa na wadau wengine wa Haki Kazi kama Kamishna wa kazi, Wakili Mkuu wa Serikali, Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali, Shirika la Kazi Duniani (ILO), CMA, LESCO, TUCTA, ATE na mifuko ya hifadhi ya jamii katika majukumu mbalimbali yaliyoainishwa kwenye makubaliano hayo.

Naye, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko amesema, OSHA kwa kushirikiana na Mahakama imeona ni vyema kuwa na mashirikiano rasmi katika maeneo manne ambayo ni pamoja na kuimarisha uelewa wa Sheria ya Afya na Usalama mahali pa kazi, kuongeza uwezo wa kushughulikia migogoro ya kazi, kuboresha utekelezaji wa sheria za kazi na kanuni zake na mengine.

 Katika Mafunzo hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo Nafasi ya Haki Kazi: Afya na Usalama Kazini kwa Maendeleo Endelevu zitatolewa mada mbalimbali ikiwa ni pamoja na Itifaki na maadili (Protocol and Etiquette), Sheria Mpya za Usafiri Zinazoendana na Teknolojia, Ujuzi wa Kidigitali wa Msingi, Data na Mifumo ya Ufuatiliaji (Telematics), Ufahamu wa Teknolojia ya Magari ya Kisasa na nyingine.

Washiriki wa mafunzo hayo ni pamoja na Majaji, Naibu Wasajili, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji, Watendaji wa Mahakama kutoka Mwanza, Shinyanga, Geita, Bukoba na Musoma, Kamishna wa Kazi, Mkurugenzi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Wakili Mkuu wa Serikali, Madereva na Walinzi wa Viongozi hao.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama leo tarehe 16 Julai, 2025 kwenye Hoteli ya Malaika jijini Mwanza.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiendelea na hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Majaji, Naibu Wasajili, Watendaji na Wadau wa Mahakama leo tarehe 16 Julai, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Malaika jijini Mwanza.




Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mafunzo hayo iliyokuwa ikitolewa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo katika picha).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akizungumza jambo wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo hayo.

Mkurugenzi wa Mafunzo, Utafiti, Takwimu na Uhamasishaji kutoka Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa OSHA leo tarehe 16 Julai, 2025 wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama ya Kazi.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa neno la shukrani wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama yanayofanyika katika Hoteli ya Malaika jijini Mwanza.


Mkurugenzi wa Mafunzo, Utafiti, Takwimu na Uhamasishaji kutoka Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) akisaini hati ya makubaliano ya ushirikiano na Mahakama kwa niaba ya Mkurugenzi wa OSHA.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) na Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko kwa pamoja wakionesha hati za makubaliano ya ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na OSHA mara baada ya kuzisaini.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko katika picha ya pamoja baada ya kusaini hati za makubaliano ya ushirikiano kati ya Taasisi hizo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akipokea tuzo kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika eneo la Haki Kazi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kushoto) akipokea 
tuzo kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika eneo la Haki Kazi.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) 
akipokea tuzo kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika eneo la Haki Kazi.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (kushoto) 
akipokea tuzo kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bw. Joshua Matiko ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika eneo la Haki Kazi.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakiwa katika picha za pamoja na sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.


(Picha na MARY GWERA-Mahakama)
 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni