Jumanne, 28 Oktoba 2025

FEDHA ZA MATUMIZI ZIELEKEZWE KWENYE MABORESHO YA MIUNDOMBINU NA USIKILIZWAJI WA MASHAURI; JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwenendo wa matumizi ya fedha za kuendeshea shughuli za Mahakama imeelezwa kuwa, zitumike vema katika shughuli za Mahakama Kanda ya Kigoma kupitia vipaumbele muhimu vilivyowekwa katika Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania (2020/2021-2024/2025) kwenye Nguzo ya Pili ya Mpango huo inayosema ‘Upatikanaji na Utoaji Haki kwa wakati.’

Hayo yalibainishwa hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma wakati wa Kikao cha Bajeti ya Kanda ya Kigoma kilichoongozwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay.

Akitoa neno la ufunguzi wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile alisema kuwa, “Viongozi na Maafisa Bajeti wa Mahakama zote muhakikishe usikilizwaji wa mashauri na vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) pamoja ukarabati wa Mahakama za mwanzo vinapewa kipaumbele zaidi katika bajeti zao ili kuendana na Mpango wa maboresho ya Mahakama na usikilizwaji wa mashauri sambamba na usimamizi wa haki za watumishi pamoja na kutunza samani za ofisi zilizopo.”

Bw. Matotay aliwasisitiza wajumbe wa Kamati ya Bajeti kuwa wabunifu katika kutekeleza bajeti zao zinazopatikana bila kutoka nje ya utaratibu sahihi uliowekwa katika matumizi ya fedha za Serikali ili kuhakikisha kazi za Mahakama yeyote hazikwami kwa namna yeyote ile.

Aidha, aliwasisitiza wajumbe wa kikao hicho kuhakikisha fedha za mirathi zilizopo katika akaunti ya Mahakama zinalipwa kwa wadaawa na kwamba imebainishwa kwamba zoezi la utambuzi wa fedha za mirathi unaendelea ili kumaliza kabisa fedha za mirathi zilizopo katika akaunti ya Mahakama Kanda ya Kigoma.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa aliwapongeza Maafisa Bajeti wa Mahakama za Wilaya kwa taarifa nzuri za utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 kwani imegusa vipaumbele vya Mahakam,  imetekelezwa kwa ufanisi mkubwa kwa usikilizwaji wa mashauri na utatuzi wa changamoto kutumia rasilimali fedha  inayopatikana.

Mhe. Mbelwa alitumia fursa hiyo kuwasisitiza Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Wilaya zote ndani ya Mkoa huo kuendelea kusimamia vema bajeti zao ili zifanye shughuli muhimu za Mahakama kama Mpango Mkakati wa Mahakama huo unavyoelekeza.

Wajumbe wa kikao hicho walikuwa Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Wilaya, Wakuu wa Idara za Mahakama Kuu Kigoma na Maafisa Tawala kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mahakama za Wilaya Kigoma, Kibondo,  Uvinza, Kasulu, Buhigwe na  Kakonko.


Wajumbe Kikao cha Bajeti ya Kanda ya Kigoma kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma wakifuatilia kwa makini maneno ya ufunguzi kutoka kwa  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akisisitiza jambo wakati akitoa neno la ufunguzi wa kikao cha Kamati ya Bajeti Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.

Mtendaji wa Mahakama Kuu  ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay akisisitiza jambo kwa wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Bajeti ya Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika jengo la Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibondo, Mhe. Maira Makonya akichangia mjadala wa bajeti ya Mahakama ya Wilaya Kibondo wakati wa kikao cha 
Kamati ya Bajeti ya Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma kilichofanyika hivi karibuni.

Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga akifafanua jambo wakati wa kikao cha Kamati ya Bajeti ya Mahakama Kanda ya Kigoma kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano -Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 
wajumbe wa kikao cha Kamati ya Bajeti ya Mahakama Kanda ya Kigoma kilichofanyika hivi karibuni. Wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe.Fadhili Mbelwa, wa pili kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay, wa kwanza kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Eva Mushi na wa kwanza kulia ni Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni