Jumatatu, 27 Oktoba 2025

KAMATI YA KITAIFA YA KUSUKUMA MASHAURI YA JINAI YAKUTANA DODOMA

  • Msajili Mahakama Kuu aeleza umuhimu wa wajumbe kwenye kikao hicho

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Kamati ya Kitaifa ya Kusukuma Mashauri ya Jinai leo tarehe 27 Octoba, 2025 imefanya kikao kujadili mambo mbalimbali yanayolenga kuharakisha usikilizaji na utoaji haki kwa wakati kwenye mashauri ya jinai.

Kikao hicho ambacho kimefanyika katika moja ya kumbi za mikutano katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma kimeongozwa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa.

Wajumbe kutoka Taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama ya Tanzania, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, Magereza, Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Chama cha Mawakili Tanganyika na nyingine zinazounda Kamati hiyo wamehudhuria kikako hicho muhimu.

Wakati wa Kikao hicho, wajumbe hao wamejadili mambo mbalimbali, ikiwemo taarifa ya hali ya mashauri ya mlundikano mpaka kufikia mwezi Septemba, 2025, hali ya Mahabusu magerezani na mkakati wa kupunguza mlundikano.

Akizungunza wakati wa kufungua kikao hicho, Mhe. Tengwa, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, aliwaeleza wajumbe hao kuwa ni muhimu katika kuhakikisha haki jinai inasimamiwana inatekelezwa na kwamba kila mmoja wao ana jukumu ambalo utekelezaji wake unategemea mwenzake.

Amesema kuwa vikao hivyo vya kusukuma mashauri ambavyo vinafanyika mara kwa mara ni zaidi ya jukwaa na lengo lake kuu ni kubaini changamoto ambazo zinaweza kuathiri utendaji kazi wao.

‘Iwapo mmoja wetu kwenye mnyororo huu atapatwa na changamoto, utendaji wa mwenzake utaathirika. Ni ukweli usiopingika kwamba kila mmoja ana jukumu lake, lakini hii haimaanishi kwamba kila mwenye jukumu anajua maarifa na ukweli wote...

‘Tunapokuwa tunakuta hivi tunapata wasaa wa kusikiliza changamoto mbalimbali zinazomkabili kila mmoja na wote kwa pamoja tunaweka mikakati ya pamoja ya namna gani ya kuitatua kwa sababu wote tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba haki inatendeka,’ Mhe. Tengwa amesema.


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa akizungumza wakati anafungua Kikao cha Kamati ya Kitaifa ya Kusukuma Mashauri ya Jinai leo tarehe 27 Octoba, 2025 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma. 

Katibu wa Kamati ya Kitaifa ya Kusukuma Mashauri ya Jinai, Mhe. Elimo Masawe [kulia] akiwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo wakati wa kikao.

 Kikao kikiendelea.

Wajumbe wa Kamati hiyo wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

Sehemu nyingine ya wajumbe wa Kamati wakiwa katika ukumbi wa mkutano.

 

Wajumbe wa Kamati-juu na chini- wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ufunguzi wa kikao.


 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni