Jumamosi, 18 Oktoba 2025

MAAGIZO TISA YA MSAJILI MAHAKAMA YA RUFANI KWA MAHAKIMU WAPYA

  • Ahimiza uaminifu, uadilifu kazini, nidhamu ya kazi
  • Asema kupata uhakimu siyo mwisho wa kujifunza

Na FAUSTINE KAPAMA-MAHAKAMA, Dodoma

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, amewataka Mahakimu Wakazi wapya 89 kuzingatia mambo tisa muhimu wanapoanza kutekeleza majukumu yao ya kuwatumikia wananchi na Taifa kwa ujumla.

Mahakimu hao waliapishwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, hivi karibuni na baadaye kushiriki kwenye mafunzo ya siku tisa yaliyoanza kutolewa tarehe 7 Octoba, 2025 na kuhitimishwa tarehe 17 Octoba, 2025.

Mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, yaliandaliwa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.

Akizungumza wakati anahitimisha mafunzo hayo jana tarehe 17 Octoba, 2025, Mhe. Herbert aliwataka Mahakimu hao kuzingatia umuhimu wa kazi yao, uadilifu na uaminifu, nidhamu ya kazi na kuwa na uhusiano mwema kazini.

Mambo mengine waliyohimizwa Mahakimu hao kuyazingatia ni kuendelea kujifunza kila siku, huduma wanazotoa, utunzaji wa rasilimali, kuzingatia maadili na mwenendo mzuri na uwajibikaji.

Umuhimu wa kazi yako

Mhe. Herbert amewaeleza Mahakimu hao kuwa kazi wanayoenda kuifanya ni kazi nyeti na wamepewa dhamana kubwa. Hivyo, wanatakiwa kufanya kazi kwa moyo wa kujitoa, huku wakitambua kwamba wana hudumia watu, Mhimili wa Mahakama na Taifa kwa ujumla.

Uadilifu na uaminifu

Msajili wa Mahakama ya Rufani amesema kuwa kila mmoja wa Mahakimu hao aamini kwamba jina lake na taaluma yake vitajengwa kwa uaminifu na uadilifu. Amewataka kujiepusha na vitendo vya rushwa, upendeleo au matumizi mabaya ya mamlaka. Amewaeleza kuwa wanatakiwa kujua kwamba uadilifu ndiyo nguzo ya mafanikio kwa Hakimu yoyote.

Nidhamu ya kazi

Mhe. Herbery amewaeleza Maheshimiwa hao kuwa kama Mahakimu wanategemewa kuwa na nidhamu ya kazi, kuheshimu ratiba za mashauri, kutengeneza malengo na kutekeleza maagizo na misingi ya utendaji kazi. Ameeleza kuwa nidhamu ndiyo itakayowatofautisha wao na watu wengine.

Uhusiano mwema kazini

Msajili wa Mahakama ya Rufani amewahimiza Mahakimu hao kuheshimu wote wanaofanya kazi kuanzia mkubwa mpaka yule wanayemuona ni mdogo. ‘Mkiheshimina kutakuwa na ushirikiano na mahusiano mazuri kazini na mambo hayo yataleta matokeo chanya sehemu ya kazi,’ amesema.

Tuendelee kujifunza kila siku

Mhe. Herbert amesema kuwa kupata uhakimu siyo mwisho wa kujifunza, hivyo amewahimiza kutambua kwamba kila siku wanapokuwepo kazini, fursa ya kuongeza maarifa na uzoefu zipo na wanatakiwa wasiziache zikawapita.

Aidha, Kiongozi huo mwandamizi wa Mahakama amewaeleza Mahakimu hao kuwa wanapokutana na lolote wasiache kuuliza, wawe wasikivu na tayari kujifunza kwa wengine, hata wale ambao wanadhani ni wadogo kwao, kwamba siyo Mahakimu.

Huduma tunazotoa

Msajili wa Mahakama ya Rufani amewaeleza Mahakimu hao kujua kwamba wanayemhudumia ni mwananchi na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo wahakikishe wanatoa huduma bora ya haki mapema ipasavyo kwa kila mwananchi.

Utunzaji rasilimali

Mhe. Herbert ameeleza pia kuwa katika ofisi zao kuna rasilimali mbalimbali, hivyo ni vizuri wakavitumia vifaa hivyo vizuri kwa malengo yaliyokusudiwa. Amesema kuwa hatua hiyo itawasaidia kulinda na kuvitunza vifaa hivyo.

Tuzingatie maadili na mwenendo mzuri

Msajili wa Mahakama ya Rufani amewakumbusha Mahakimu hao kuwa maadili yao siyo pale wanapokuwa mahakamani tu, bali hata nje ya ofisi zao.

Hivyo wanatakiwa kujua kwamba Hakimu ni mtu ambaye anayeheshimika na anafuatiliwa kwa sababu anaonekana kuwa mfano na taswira kwa wote waliopo katika jamii husika.

Uwajibikaji

‘Kila kazi unayopewa ni jukumu la kutekeleza kwa ufanisi na hivyo unapaswa kuwajibika ipasavyo,’ Mhe. Herbert amewambia Mahakimu hao.

Katika hili, amewakumbusha kwamba kuna Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050. Mhe. Herbert amewaasa kila mmoja wao aisome Dira ile, aielewe na aone inamtakaje yeye kama Hakimu kuwa mwajibikaji.

Katika hafla ya kuhitimisha mafunzo hayo, washiriki wote walipatiwa vyeti pamoja na vitendea kazi, ikiwemo kompyuta mpakato, yaani laptops, huku wengine wakikabidhiwa zawadi mbalimbali kwa ushiriki bora walioutoa wakati wa mafunzo hayo.

Viongozi wengine walioshiriki kwenye hafla ya kuhitimisha mafunzo hayo ni Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick na Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda.

Wengine ni Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Emmanuel Mrangu na Naibu Mkurugenzi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngunguru.

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert akizunguza wakati anafunga mafunzo elekezi yaliyotolewa kwa  Mahakimu Wakazi wapya 89 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akizungumza kwenye hafla hiyo.

Meza Kuu inayoongozwa na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert ikiwa kwenye hafla ya kuhitimisha mafunzo hayo. Kushoto ni Mkrugenzi wa Rasilimaliwatu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Betrice Patric na kulia ni Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda. Picha chini ni Viongozi wengine wakifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Meza Kuu ikijiandaa kutoa vyeti kwa washiriki wa mafunzo. Picha chini, mshiriki mmoja akipokea cheti chake.


Mshiriki mwingine wa mafunzo hayo akionesha heshima kubwa kwa Mgeni Rasmi kabla ya kupokea cheti chake.

Washiriki wa mafunzo hayo [juu na chini] wakipokea zawadi zao kutoka Meza Kuu.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo akipokea kompyuta mpakato kama kitendea kazi ktuka Meza Kuu.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni