Ijumaa, 17 Oktoba 2025

WIKI YA USULUHISHI KUFANYIKA NOVEMBA 2025

  • Vikao vya maandalizi vikihusisha wadau vyaanza

Na EUNICE LUGIANA-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, jana tarehe 16 Octoba, 2025 imefanya kikao na Watendaji Wakuu wa Taasisi mbalimbali kujadili namna bora ya kushiriki kwenye Wiki ya Usuluhishi itakayofunguliwa tarehe 20 Novemba, 2025 jijini Dodoma.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Banki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kilifunguliwa na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud, ambaye alimwakilisha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Akizungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Aboud alisema kuwa japokuwa jukumu kubwa la Mahakama ni kutenda haki mapema ipasavyo, lazima kuzingatia njia mbadala au utatuzi mbadala wa migogoro ambao umesisitizwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977, Ibara ya 107 (d).

Alisema kuwa kwakuwa Mahakama imedhamiria kwa dhati kuona masuala ya utoaji wa haki yanapaswa kufanywa mapema ipaswavyo, hatua hiyo ni mwendelezo katika kukamilisha jukumu kubwa iliyopewa kikatiba la kutoa haki.

Mhe. Aboud alieleza kuwa kikao hicho kina lengo la kujadili utatuzi mbadala wa migogoro, njia ambayo itasaidia kwa upande wa Mahakama kupunguza mashauri ambayo yasingekuwa na ulazima wa kufika mahakamani iwapo wadau husika kwenye Taasisi au Ofisi zao wangeitumia.

Alisisistiza kwamba njia mbadala ya utatuzi wa migogoro ni rahisi, haina gharama na huwafanya pande zote mbili kuwa na mahusiano mazuri. “Hii ni njia ambayo inatakiwa tuienzi na kuhakikisha tunaitafutia mikakati bora ya kuitumia,” alisema Jaji Abood.

Kadhalika, alibainisha kuwa njia hiyo itawavutia wawekezaji kuja kuwekeza Tanzania maana watajua migogoro ya kibishara haichukui muda mrefu kuisha na baadaye kuendelea na biashara kwa amani kwakuwa wafanyabishara wengi hawapendi migogoro.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma alisema kuwa mkutano huo unaweka historia ya safari ya kuhamasisha matumizi ya njia ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro nchini Tanzania.

Alisema kuwa lengo kuu la Mahakama na wadau wake ni kupata uelewa wa pamoja juu ya kuhamasisha usuluhishi wenye kuleta ufanisi na tija, siyo tu kama inavyotajwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bali hata kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025- 2050.

Alibainisha kuwa nchi nyingi duniani hivi sasa zimekuwa zikitumia njia za usuluhishi na kuondokana na dhana ya kuendesha mashauri mahakamani kwa muda mrefu na hii ni kutokana na faida nyingi zinazotokana na njia hiyo.

Akitoa takwimu za migogoro katika Kituo hicho, Mhe. Maruma alisema wameshudia ongezeko kubwa katika kutatua migogoro. ‘Takwimu zinaashiria nia njema kwamba tukiendelea kwa juhudi za pamoja tunaweza kufanikisha sana migogoro mingi ikaishia kwenye hatua za usuluhishi,’ alisema.

Alisema kuwa mwaka 2023 migogoro 82 ilifanikiwa kupitia njia ya usuluhishi, kwa mwaka 2024 migogoro 109 na mpaka Oktoba 2025, migogoro 70 imemalizika kwa njia hiyo.

Naye Prof. Zakayo Lukumai, akitoa taarifa ya hali ya usuluhishi Tanzania, alisema kuwa usuluhishi uliingizwa mahakamani kama kiambata (court annex mediation) na kuanzia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na baadaye Mahakama Kuu na sasa imeenea Mahakama zote.

Alieleza kuwa kwa sasa somo la usuluhishi limeingizwa kwenye mitaala ya Shule ya Sheria kwa Vitendo na linafundishwa kwa vitendo. Mhe. Lukumau alisema kuwa kuanzishwa kwa Kituo cha Usuluhishi kumeongeza kasi kwa njia mbadala kuweza kukubalika katika utatuzi wa migogoro.

Prof Lukumai alitoa wito kwa Vyuo Vikuu nchi kulifanya somo hilo kuwa la lazima ili kuanza kujenga misingi tangu mwanzo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Viongozi wa Mabenki, Taasisi za Usuluhishi na vitengo vyote vinavyoshughulika na usuluhishi.

Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud [juu na chini] akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akizungumza kwenye hafla hiyo.

Mhadhiri kutoka Shule ya Sheria kwa Vitendo, Mhe. Prof. Zakayo Lukumai akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao hicho.




Sehemu ya washiriki wa kikao hicho [picha mbili juu na moja chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud [kulia] akiwasili kwenye ukumbi wa kikao akiwa ameongozana na wenyeji wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma [katikati], Naibu Msajili, Mhe. Augustina Mmbando [wa pili kutoka kushoto] na Mtendaji, Bi. Hellen Mkumbwa [wa kwanza kushoto].
[Picha na Bakari Mtaullah-Dar es Salaam]
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni