- Ataka mashauri ya rushwa, uhujumu uchumi kupewa kipaumbele
Na HABIBA MBARUKU-
Mahakama Dodoma
Jaji Kiongozi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustepher Mohamed Siyani, amewasisitiza Majaji, Mahakimu na
Wakurugenzi wa Mahakama ya Tanzania kuhakikisha wanatekeleza mikakati inayowekwa
na vikao mbalimbali pamoja na kuwasilisha utekelezaji wake kwa wakati.
Mhe. Dkt. Siyani ametoa rai
hiyo leo tarehe 25 Februari, 2026 kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu wa Mahakama
ya Tanzania, Mhe. George Masaju, kufungua kikao cha mwaka cha Majaji Wafawidhi
wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwa mwaka 2026, kinachofanyika katika ukumbi wa
Mahakama, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Kiongozi amesema
kuwa lengo na shabaha ya vikao hivyo ambavyo hufanyika walau mara moja kila
mwaka ni kupata fursa ya kujipima na kujitathmini juu ya utendaji kazi wa
Mahakama, sambamba na utekelezaji wa Dira na Dhima ya Mahakama.
“Kwa hiyo, lengo la vikao
hivi ni kujitathmini wapi tumefanya vizuri lakini pia maeneo gani hatukufanya
vizuri, matokeo ya tathmini hii ni kuboresha mchakato mzima wa utoaji haki
nchini, jukumu ambalo Mahakama imekasimiwa na umma kupitia Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania,” amesema Mhe. Dkt. Siyani.
Ameeleza kuwa siyo vema
hata kidogo kwa Viongozi kusubiri maelekezo ili kutekeleza mikakati inayowekwa.
Amemtambua kwa namna ya pekee Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara,
Mhe. Alvin Mgeta, ambaye amekua akitekeleza mikakati ya vikao mbalimbali bila
kusubiri barua au maelekezo kutoka Mahakama Kuu.
“Ninalolisema kwa Waheshimiwa
Majaji nalisema pia kwa Wakurugenzi wengine ambao kwa nafasi zao wanahudhuria
vikao hivi na hivyo wana wajibu wa kutekeleza mikakati na yale ambayo
yanaelekezwa, siyo vema hata kidogo kwa Viongozi kusubiri maelekezo ili
kutekeleza mikakati inayowekwa,’amesisitiza Jaji Kiongozi.
Akitoa taswira ya
utendaji kazi wa Mahakama Kuu na Mahakama zilizopo chini yake, Mhe. Dkt. Siyani
amesema kuwa Mahakama ya Tanzania ilivuka mwaka 2024 kukiwa na mashauri
yaliyobaki 38,121.
Jaji Kiongozi amebainisha
kuwa mwaka 2025, jumla ya mashauri 240,607 yalipokelewa na mashauri 250,388
yalimalizika, huku kiwango cha uondoshaji wa mashauri kikiongezeka kutoka asilimia
83 mwaka 2024, hadi kufikia asilimia 88 mwaka 2025.
Mhe. Dkt. Siyani ameeleza
kuwa mafanikio hayo ni sawa na ongezeko la asilimia 5.4 kwa Mahakama Kuu na
Mahakama za chini. Ameeleza pia kuwa wastani wa muda wa shauri kukaa mahakamani
umeendelea kupungua kutoka siku 78 mwaka 2024 hadi siku 66 mwaka 2025.
Ameongeza kuwa pamoja na
ongezeko la mashauri yaliyopokelewa mwaka 2025, mzigo wa mashauri kwa kila Jaji
au Hakimu umeendelea kupungua, ambapo wastani kwa mwaka 2024 ulikuwa mashauri
228 kwa kila Jaji au Hakimu na umepungua hadi kufikia 222 kwa mwaka 2025.
Kadhalika, Jaji Kiongozi
amebainisha kuwa uimarishaji wa Mahakama Inayotembea umeendelea, ambapo kwa
mwaka 2025 Mahakama hiyo imewafikia wananchi 9,069 na hivyo kuvuka shabaha ya
mwaka 2024 ambayo ilikuwa kufikia watu 5,833.
Ameongeza kuwa kwa mwaka
2025 mchakato wa uchaguzi mkuu ulisababisha kufunguliwa kwa mashauri 15 kabla
ya uchaguzi, na kwamba ni shauri moja pekee ambalo limesalia Mahakama Kuu kwa
sababu ya uwepo wa shauri la marejeo katika Mahakama ya Rufani.
Aidha, Mhe. Dkt. Siyani
amesema kuwa baada ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi, jumla ya mashauri 12
ya kupinga matokeo ya ubunge na mashauri madogo 11 yanayotokana na mchakato huo
yalifunguliwa kwenye Masjala mbalimbali za Mahakama Kuu, huku Mahakama za
Hakimu Mkazi zikipokea mashauri 29 ya kupinga matokeo ya udiwani na mashauri ya
maombi madogo 24 yanayohusiana na mashauri hayo, hiyo kufanya jumla ya mashauri
yote yaliyotokana na matokeo ya uchaguzi kuwa mashauri 76.
Jaji Kiongozi amesema kuwa
usikilizaji wa mashauri hayo unaendelea na hadi kufikia tarehe 25 Februari,
2026, mashauri matatu ya msingi na madogo mawili pekee yamebaki kati ya
mashauri 23 ya Mahakama Kuu, huku upande
wa Mahakama ya Hakimu Mkazi yakiwa yamesalia mashauri matatu peke kati ya
mashauri 53 yaliyofunguliwa.
Sambamba na hayo, Mhe. Dkt.
Siyani ameeleza kuwa mkakati wa kusikiliza mashauri yanayochochea ukuaji wa
uchumi, uliwekwa katika vikao vilivyofanyika mwezi Septemba na Oktoba, 2025 na
utekelezaji wake ulifanyika, ambapo Mahakama Kuu na Mahakama za Hakimu Mkazi
zilifanikiwa kusikiliza mashauri 2,675 yaliyowezesha kuachilia kiasi cha
shilingi za Kitanzania 11,940,395,000,000.
Vilevile, ameeleza kuwa, ugatuzi
uliofanywa kwa wasimamizi wa mashauri ya uhujumu uchumi,kupitia uteuzi wa Majaji
wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa kwenda kwa Majaji wote wa
Mahakama Kuu, umechangia kufanikisha usikilizaji wa mashauri 28 chini ya
usimamizi wa Masjala mbalimbali nchini.
Jaji Kiongozi ameeleza kuwa
Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ikimaliza mashauri 16 kati ya
88 yaliyokuwepo wakati hati hiyo inatolewa. Ameongeza kuwa pamoja na uwepo wa
hati hiyo, bado kuna wastani wa mashauri 133 yanayoendelea kwenye Masjala
mbalimbali za Mahakama Kuu.
Katika hatua nyingine,
Mhe. Dkt. Siyani amewataka Majaji kuyapa kipaumbele mashauri ya rushwa na
uhujumu uchumi kama ambavyo wanayapa kipaumbele mashauri mengine ambayo yapo
katika Masjala zao.
“Nichukue fursa hii
kuwataka Waheshimiwa Majaji kuyapa kipaumbele mashauri haya kama mnavyoyapa
mashauri mengine yaliyopo katika Masjala zao” amesisitiza Jaji Kiongozi.
Mhe. Dkt. Siyani amesema
kuwa hatua imepigwa katika eneo la usimamizi wa mashauri ya mirathi, hususan
ulipaji wa fedha za mirathi na utekelezaji wa kanuni mpya za mirathi.
Amesema kuwa kumbukumbu
zilizopo zinaonesha kati ya tarehe 01 Oktoba, 2025 na tarehe 17 Februari, 2026,
fedha za mirathi zilizokuwa kwenye akaunti za Mahakama zimepungua kutoka
wastani wa shilingi Kitanzania 53 bilioni hadi bilioni 36.
Jaji Kiongozi amesisitiza
kuwa takwimu hizo zinaonesha kuwa bado Mahakama ina kazi kubwa ya kufanya
katika eneo hilo, huku akiwasihi Majaji kutumia kikao hicho kama fursa ya
kubadilishana uzoefu ili kuimarisha usimamizi wa mashauri.
“Takwimu hizi zinaonesha
kuwa bado tuna kazi ya kufanya katika eneo hili, ni matumaini yangu kuwa
Waheshimiwa Majaji watapata fursa ya kubadilishana uzoefu na hivyo kuimarisha
usimamizi wa mashauri haya, hususan ulipaji wa fedha za mirathi zilizopo kwenye
akaunti za Mahakama,” amesema Jaji Kiongozi.
Akizungumza kuhusu matumizi
ya mifumo mbalimbali ya kieletroniki mahakamani, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa Mahakama
inaendelea kutilia mkazo matumizi hayo kwa lengo la kurahisisha na kuharakisha
upatikanaji wa haki mapema ipasavyo, pamoja na matumzi ya mifumo mingine ya
TEHAMA kama Mfumo wa Kuratibu na Kusikiliza Mashauri (ESMS).
Jaji Kiongozi ameongeza
kuwa mwaka 2025, Mahakama ilianza rasmi kutumia mfumo wa kieletroniki wa
upimaji na utendaji kazi kwa Maofisa wa Mahakama.
Kadhalika, amesema kuwa
Mahakama imeendelea kuimarisha ukaguzi wa Mahakama na Magereza kama sehemu ya
kupima na kupata mrejesho wa ubora, ufanisi pamoja na kubaini changamoto za
utoaji haki.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani [juu na chini], akizungumza kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 25 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.







Hakuna maoni:
Chapisha Maoni