Na ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro
Mahakama
imeendelea kuchukua hatua madhubuti katika kuimarisha utoaji wa haki kwa watoto
kwa kuandaa kikao kazi maalum, kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa
Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), ili kupitia kanuni za Mahakama za Watoto za mwaka 2016 kwa ajili ya kuziboresha.
Uboreshaji huo unalenga kuzifanya kanuni hizo ziendane na mabadiliko ya sheria yaliyotokea, kuongeza
ufanisi, tija na weledi katika usikilizaji na uamuzi wa mashauri ya watoto.
Kikao kazi hicho
cha siku tano kilianza
tarehe 9 Februari, 2026 kikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Nyigulila
Mwaseba, kikihusisha mijadala ya kina, mapendekezo ya kitaalamu pamoja na
kubadilishana uzoefu juu ya utekelezaji wa sheria na kanuni hizo.
Aidha, kikao
hicho kinafanyika
katika ukumbi wa mkutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC)
Morogoro na kimewakutanisha wataalamu
mbalimbali wa haki za mtoto, wakiwemo Naibu Wasajili, Mahakimu,Wizara za
Kisekta, Taasisi za Kiserikali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Maafisa
Ustawi wa Jamii, Maafisa wa Jeshi la Polisi, pamoja na Mawakili na Wanasheria
kutoka Taasisi mbalimbali za kisheria.
Mwenyekiti wa
kikao hicho, alieleza kuwa Kanuni za
Mahakama ya Watoto hazijawahi kufanyiwa mapitio tangu kuanza kutumika mwaka
2016. Alibainisha kuwa hali hii imezua changamoto katika utekelezaji wake
kutokana na mabadiliko ya kisheria yaliyotokea baada ya kipindi hicho. Aliweka
msisitizo mkubwa katika umuhimu wa kuzingatia ulinganifu wa kanuni hizi na
sheria mama pamoja na misingi ya maslahi bora ya mtoto.
“Nadhani sheria
hizi hazijawahi kufanyiwa marekebisho tangu mwaka 2016, nimekua nikiona changamoto mbalimbali haswa kutokana
na mabadiliko ya teknolojia na sheria mbalimbali,”
alisema Mhe. Mwaseba.
Kwa ujumla, kikao
kazi hiki kinatarajiwa kuwa chachu ya maboresho makubwa katika mfumo wa utoaji
haki kwa watoto nchini, kwa kuhakikisha kuwa sheria zinazotumika zinaendana na
mahitaji ya sasa ya kijamii, kisheria na kiteknolojia, huku maslahi ya mtoto
yakiendelea kuwa kipaumbele cha juu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni