Jumatano, 11 Februari 2026

MAHAKAMA KANDA YA SONGEA YAFANYA KIKAO KUJADILI MPANGO MKAKATI WA MASHAURI, UTAWALA

Na NOEL SYLIVESTER - Mahakama Kuu, Songea

Uongozi wa Mahakama Kanda ya Songea, hivi karibuni ulikutana na  Mahakimu wote kujadili mpango mkakati wa kimahakama na kiutawala kwa mwaka 2026 ili kuboresha utendaji kazi, uadilifu na ushilikiano.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Taasisi ya Kupamba na Kuzuia Rushwa (PCCB) wilayani Songea mkoani Ruvuma, kiliongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. James Karayemaha na kuhudhuriwa na Viongozi wengine wa Mahakama kwenye Kanda hiyo.

Viongozi hao ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Naibu Msajili, Mhe. Elizabeth Nyembele pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Bw. Allan Mwela.

katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi alielezxa kuwa wamekutana kujadili mpango huo kuhusu mashauri na masuala ya kiutawala kwa mwaka 2026, ambao unalenga kuimarisha utoaji wa haki kwa wakati, kwa uwazi, kwa usawa na kwa kuzingatia misingi ya sheria.

‘Tunatarajia mpango huu utatusaidia kupunguza mlundikano wa mashauri, kuboresha usimamizi wa mashauri, kuimarisha nidhamu ya kazi na kuongeza ufanisi katika utawala wa Mahakama zetu. Tukifanya mipango yetu vizuri hatutakuwa na msongo wa mawazo, tutajijengea uaminifu, tutaboresha namna ya kutoa uamuzi na tutapata matunda tunayoyatamani,’ alisema.

Mhe. Karayemaha aliongeza kuwa wakati wa kutekeleza jukumu la utoaji haki lazima kukumbuka viapo vyao vya kutoa uamuzi wa haki kwa kuzingatia matakwa ya Ibara ya 4, 107A na 107B ya Katiba.

‘Msingi wake ni kuimarisha amani na udugu wa wananchi. Kwa hiyo, sisi waamuzi inatupasa kuzingatia sheria na maadili ya utumishi wetu. Tukifanya kazi yetu ipasavyo bila woga tutadumisha utawala wa sheria, ambalo ni jukumu letu pia. Hii sio hiari, tumeelekezwa na Ibara ya 26 ya Katiba kuwaadhibu na kuwawajibisha ipasavyo wanaokiuka masharti ya Katiba na sheria zetu,’ alisema.

Aliwakumbusha Mahakimu hao kuwa wanalo pia jukumu la kulinda uhuru wa Mahakama unaolindwa na kuhifadhiwa katika Ibara ya 30(2)(d) ya Katiba ikichagizwa na Kifungu cha 114 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu.

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa pale inapotokea uhuru wa Mahakama umechokonolewa au kupakwa matope kwa kauli au vitendo, wanapaswa kumama imara kuwakumbusha hao kuhusu heshima na uhuru wa Mahakama.

‘Woga ni sumu ya mafanikio na mabadiliko na inakinzana na malengo ya Mwenyezi Mungu, ni matarajio yangu kuwa katika kikao hiki tutajadili kwa uwazi changamoto zilizopo katika mashauri na utawala, tutoe mapendekezo ya vitendo na kujenga mikakati itakayotekelezeka kwa ufanisi katika mwaka 2026 na kuendelea,’ Mhe. Karayemaha alisema.

 









Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mbeya.


 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni