Jumatano, 11 Februari 2026

WATUMISHI MBEYA WAPATIWA ELIMU YA AFYA YA KINYWA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wamepata elimu muhimu ya afya ya kinywa na meno tarehe 9 Februari, 2026. Elimu hiyo ilitolewa na Daktari Melkzedeck Japhet kutoka kliniki ya Confort Dental Care iliyopo Mwanjelwa, Jijini Mbeya.

Akitoa elimu hiyo Daktari Japhet alisisitiza mambo muhimu yakuzingatia ikiwemo, usafi wa kinywa ambapo Daktari alisisitiza kuhusu kusafisha meno angalau mara mbili kwa siku hasa usiku kabla ya kulala, kupunguza ulaji wa vyakula vyenye sukari nyingi ili kuzuia kuoza kwa meno na afya ya fizi ambapo daktari alisema dalili za magonjwa ya fizi, namna ya kuyatambua na matibabu yake.

Aidha Daktari Japhet aliongezea kwa kuwaasa watumishi hao kuvunja dhana potofu kuhusiana na magonjwa ya meno na matibabu ya meno kwa mama mjamzito na kueleza kuwa Mama mjamzito anaweza kupata matibabu ya meno inapohitajika, hakuna “mdudu mtoboa jino” bali ni bakteria na asidi zinazotokana na sukari na kwamba kung’oa jino si lazima kufanyika asubuhi pekee na chakula kinaweza kuliwa kabla ya kung’oa jino kulingana na ushauri wa daktari, mambo ambayo walio wengi huwa na dhana potofu.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, alitoa shukrani kwa daktari kwa kutenga muda na kutoa elimu hiyo, alisisitiza kuwa elimu hiyo imewafanya watumishi wa mahakama kutambua zaidi umuhimu wa kujali afya ya kinywa na meno kwa maisha bora na ufanisi kazini.

Daktari Melkzedeck Japhet (aliyesimama) akitoa elimu ya Afya ya kinywa na meno mbele ya watumishi wa Mahakama kuu Mbeya. 

Afisa Utumishi kutoka Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Sarah Rossi (wa pili kushoto) akiuliza swali kwenda kwa mtaalamu wa afya wakati wa utoaji elimu ya afya ya kinywa na meno.


Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa pili kulia) akiuliza swali Kwenda kwa mtaalamu wa afya wakati wa utoaji elimu ya afya ya kinywa na meno.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza Kulia), Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (Katikati), na wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakipata elimu ya afya ya kinywa na meno.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Mbeya wakipata elimu kutoka kwa Mtaalamu wa Afya 



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni