Alhamisi, 12 Februari 2026

MAAFISA USAFIRISHAJI WA MAHAKAMA WATAKIWA KUZINGATIA TAHADHARI, USALAMA WA VYOMBO VYA MOTO

Na. Halima Mnete & James Busanya - Mahakama

Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania nchini wamehimizwa kuongeza umakini, nidhamu na kuzingatia kwa kina misingi ya udereva wa kujihami ili kupunguza ajali zinazotokea wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kimahakama.

Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodma katika kikao maalum kilichowakutanisha madereva hao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, kilicholenga kujadili masuala ya usalama barabarani, ustawi wa madereva pamoja na changamoto wanazokumbana nazo katika utendaji wa kazi zao za kila siku.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania , Bw. Shedrack Bambaganya, amesema kuwa, katika kipindi cha hivi karibuni kumekuwepo na ajali kadhaa zilizowakumba madereva wa Mahakama wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hali iliyosababisha madhara ya kibinadamu pamoja na uharibifu mkubwa wa magari ya Taasisi.

Ameeleza kuwa, ajali hizo zimeongeza gharama kubwa kwa Mahakama, zikiwemo gharama za matengenezo ya magari, ucheleweshaji wa ratiba za shughuli za kimahakama na hatari ya kupoteza maisha ya watumishi pamoja na wananchi wanaohudumiwa.

“Haya ni matukio ya bahati mbaya, lakini ni wajibu wetu kuongeza tahadhari zaidi barabarani. Tunapaswa kuzingatia kanuni za usalama, kutumia udereva kwa kujihami na kuwa makini muda wote tunapokuwa barabarani. Usalama wa maisha ya wateja wetu na watumiaji wengine wa barabara ni kipaumbele,” amesisitiza Bw. Bambaganya.

Aidha, ameongeza kuwa, zipo changamoto ambazo madereva hukutana nazo, zikiwemo ajali zinazosababishwa na uzembe au mwendo kasi wa madereva wa Taasisi nyingine na watumiaji wengine wa barabara. Akitolea mfano; ajali iliyotokea Nzega mkoani Tabora katika msafara wa Jaji Kiongozi, alisema kuwa msafara huo ulikuwa katika upande sahihi wa barabara, lakini dereva wa Taasisi nyingine ya Umma aliendesha kwa mwendo kasi bila kuchukua tahadhari, hali iliyomfanya ashindwe kudhibiti gari na kusababisha ajali.

Aidha, Bw. Bambaganya amefafanua kuwa, kutokana na umakini, uzoefu na ustadi wa dereva wa Jaji Kiongozi, aliweza kulidhibiti gari kwa haraka na kuokoa maisha ya waliokuwamo ndani ya gari hilo, licha ya gari kuharibika vibaya na kuhitaji matengenezo ya gharama kubwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick aliwashukuru madereva kwa kuitikia wito wa kikao hicho na kutoa maoni yao kwa uwazi na pia kuwasilisha changamoto mbalimbali wanazokutana nazo kazini. Mkurungenzi huyo ameahidi kuwa, uongozi wa Mahakama unatambua mchango mkubwa wa madereva katika kuhakikisha shughuli za kimahakama zinafanyika kwa wakati na kwa usalama.

Vilevile, miongoni mwa changamoto zilizotajwa na madereva ni suala la kupanda vyeo kwa waliopo katika madaraja ya chini, pamoja na uhitaji wa mafunzo ya mara kwa mara ya usalama barabarani. Bi. Beatrice aliahidi kuwa uongozi utayafanyia kazi masuala hayo kwa kushirikiana na kitengo cha ndani cha malalamiko cha kuwahudumia watumishi (Judiciary Internal Customer Services) ili kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza motisha kwa madereva hao.

Kikao hicho kimetajwa kuwa hatua muhimu ya kuimarisha mawasiliano na ushirikiano kati ya uongozi na madereva kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha usalama barabarani, kulinda rasilimali za Mahakama na kuhakikisha utekelezaji wa majukumu ya kimahakama unafanyika kwa ufanisi, uwajibikaji na weledi.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick akijibu baadhi ya hoja zilizowasilishwa na Maafisa Usafirishaji kwenye mafunzo elekezi yaliyoendeshwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani)

Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania Bw. Shedrack Bambaganya akifafanua jambo wakati wa mafunzo elekezi kwa Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.
Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.


Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mafunzo hayo elekezi yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha)

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni