Jumatatu, 16 Februari 2026

MAHAKAMA KITUO CHA USULUHISHI YAENDESHA MAFUNZO YA UPATANISHI KWA MAHAKIMU, NAIBU WASAJILI

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], hivi karibuni kiliendesha mafunzo ya siku tatu yanayohusu ya upataniishi wa Mahakama ili kuimarisha uwezo wa kutumia njia ya upatanishi ambayo ni rafiki katika utatuzi wa migogoro.

Mafunzo hayo ya siku tatu yaliyoanza tarehe 11 Februari, 2026, yakiwaleta pamoja Mahakimu wa ngazi zote pamoja na Naibu Wasajili kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Divisheni, yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma.

Akizunzungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Maruma alieleza kuwa mafunzo hayo yamefanyika katika wakati muafaka na muhimu wakati dira ya 2050 inahimiza usuluhishi kama nyenzo muhimu ya msingi mkuu katika kuleta amani, umoja na utulivu katika taifa letu.

‘Hii inaendana na mikakati ya Mahakama katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo kama inavyosistizwa katika ibara ya 107A (2) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,’ alisema.  

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa mafunzo hayo pia ni moja ya maandalizi ya Wiki ya Usuliuhishi ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi 2026 nchini kote, hivyo, ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelewa kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia hiyo ya upatanishi katika kuharakisha upatikanaji wa haki.

Mhe. Maruma alibainisha kuwa Mahakama zinaendelea kukabiliwa na ongezeko la mashauri, ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa gharama nafuu, na kwa maridhiano, bila kupitia mchakato mrefu wa mashauri, hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alieleza kuwa upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kila mmoja ni mashuhuda wa ongozeko la migogoro inayomalizika katika hatua ya upatanishi ambayo kwa sasa inazidi asilimia 50, tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.

Hali hii inatupa matumaini na chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na Wadau wa usuluhishi ili kuongeza ufanisi katika kutatua migororo kupitia upatanishi na kufikia malengo yaliyopo katika dira ya 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta amani na utulivi katika jamii zetu pamoja na kuchangia katika uchumi endelevu,’ alisema.    

Jaji Mfawidhi alieleza pia kuwa upatanishi unaofanyika nje na ndani ya Mahakama hauondoi mamlaka ya Mahakama, bali unaikamilisha na kusaidia upatikanaji wa haki, kuondoa mrundikano wa mashauri, kuokoa muda na rasilimali, kulinda mahusiano ya kijamii na kibiashara, na kuwapa wahusika nafasi ya kushiriki kikamilifu katika kupata suluhu ya migogoro.

Alisema kuwa mafunzo hayo, siyo ya kiutaratibu pekee, bali ni uwekezaji katika kujenga uwezo, maadili, na taaluma ya wapatanishi wa Mahakama na wadau wa usuluhishi.  

Mhe. Maruma alitumia fursa hiyo kutoa shukrani za dhati kwa chuo cha IJA kwa kubali ombi lao la kushirikiana nao katika kuendesha mafunzo hayo ambayo ni muendelezo wa juhudi za Mahakama katika kuwajengea uwezo wa watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Natambua kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mafunzo ya upatanishi tayari yameshafanyika kwa Majaji na Mahakimu zaidi ya mia moja na baadhi yao ndio wamekuwa wakufunzi wa mafunzo haya ambayo ni endelevu,’ alisema.

Jaji Mfawidhi alitumia fursa hiyo pia kuwashukuru Wadau muhimu kwa kushirikiana na Kituo katika kuwezesha mafunzo hayo bila kusita pale walipowafikia.

Alieleza kuwa hatua hiyo inaashiria mwanzo wa ushirikiano ambao utakuwa endelevu na kutaleta faida kubwa katika kukuza, kuongeza ufanisi na kuhamasisha si tu matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro bali hata katika kuibua changamoto zinazokwamisha na kuzifanyia kazi kwa pamoja.

Awali, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbando, alieleza kuwa ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Naibu Wasajili na Wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa usuluhishi si jukumu la mtu mmoja, bali ni juhudi ya pamoja zinazohusika na utoaji haki.

‘Majaji na Mahakimu, ingawa si wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa mchakato wa usuluhishi, na hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa misingi, taratibu na falsafa ya mediation.

Aidha, Mhe. Mmbando alielezea kutambua kwa heshima uwepo wa Mratibu wa Mafunzo kutoka IJA, ambaye mchango wake ni muhimu katika kujenga uwezo wa Mahakama kupitia mafunzo endelevu na ya vitendo.

Alieleza pia kuwa uwepo wa TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwani bima ni miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimkataba, ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.

‘Ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi za udhibiti kama TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki, na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo wa haki,’ alisema.

Picha ya Meza Kuu, katikati ni Mhe. Zahra Maruma, kulia ni Mhe. Angela Bahati na kushoto ni Bi. Magreth Magumi.

Mgeni Rasmi akifungua mafunzo.

Meza Kuu na Wakufunzi wa usuluhishi.

Meza Kuu na Naibu Wasajili.

Meza Kuu na Mahakimu wa ngazi zote [juu na chini].


Washiriki wote wakiwa kwenye mafunzo [juu na chini].


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma







 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni