Na. Rehema Awet – Mahakama, Mwanza
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Nimilwa Kilekamajenga amesema kuwa, Siku ya
Sheria ni fursa muhimu ya kutathmini na kutafakari upya dhamira ya Mahakama
katika kulinda haki za wananchi na kusimamia utawala wa sheria nchini.
Aliongeza kuwa Mahakama ina nafasi ya kipekee katika kujenga jamii yenye haki,
amani na maendeleo endelevu.
Aidha,
alibainisha maeneo makuu ya mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya
taifa kuwa ni pamoja na ulinzi wa haki
za binadamu na kuimarisha utawala wa sheria, kuchochea ukuaji wa uchumi na uwekezaji, pamoja na kudumisha amani na utulivu wa kijamii.
Mhe. Kilekamajenga, alibainisha
kuwa, maeneo mengine kuwa ni kuimarisha Demokrasia, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi. Pia
alieleza kuwa maboresho ya miundombinu
na matumizi ya TEHAMA katika usikilizwaji na uendeshaji wa mashauri,
jambo ambalo limeongeza ufanisi na uwazi katika utoaji wa haki.
Kwa upande
wake, Bw. Kabyemela S.
Lushagara akizungumza kwa niaba ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, alisema
Mahakama ni Mhimili
muhimu wa Dola
unaochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia ulinzi
wa haki, utawala wa sheria na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji. Alioneza kuwa, Mahakama
huru, yenye weledi na uadilifu huongeza imani ya wananchi na wawekezaji, hivyo
kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Aidha,
mwakilishi huyo kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali alisema, mafanikio
mbalimbali yaliyopatikana katika sekta ya haki, ikiwemo kupungua kwa msongamano
wa mashauri, ongezeko la Majaji na Mahakimu, matumizi ya mifumo ya TEHAMA kama
e-filing, pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na Taasisi za
utoaji haki. Pia alisisitiza kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo
2050 unahitaji mfumo imara wa utoaji haki unaofanya kazi kwa ufanisi na kwa
wakati
Akizungumza
kwa niaba ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Kanda ya Mwanza, Wakili Erick
Mutta alisisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa uhuru wa Mahakama na ulinzi wa
Mawakili wa Kujitegemea kama nguzo ya Utawala wa Sheria. Wakili Mutta alieleza
kuwa Mahakama inayofanya kazi kwa haki na bila upendeleo hujenga imani ya
wananchi na kuleta utulivu wa kijamii na kisiasa unaohitajika kwa maendeleo
endelevu.
Chama cha
Mawakili wa Kujitegemea kanda ya Mwanza ilitumia jukwaa hilo kueleza mchango
wake katika utoaji wa msaada wa kisheria kwa wananchi wasio na uwezo, elimu ya
kisheria kwa umma, pamoja na ushiriki wake katika utatuzi wa migogoro kwa njia
mbadala nje ya Mahakama.
Mgeni rasmi ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi Kanda
ya Mwanza Mhe. Kilekamajenga alihitimisha kwa kutoa wito kwa wadau wote wa haki kushirikiana kwa karibu na
Mahakama ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati kwa usawa na kwa mujibu wa
sheria, kwa lengo la kuimarisha ustawi wa wananchi na maendeleo ya Taifa kwa
ujumla.
Maadhimisho hayo ya Siku ya
Sheria nchini yaliyofanyika mkoani
Mwanza kwa yakibeba kauli mbiu isemayo “Mchango
wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.” yalihudhuriwa na Viongozi
mbalimbali wa Serikali,
vyombo vya Dola,
wataalamu wa sheria pamoja na wananchi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akiwa tayari kwa
ukaguzi wa Gwaride maalum kuashiria uzinduzi wa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama kwenye Maadhimisho ya Siku ya
Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026. Waliosimama nyuma ni
Majaji, Mawakili na sehemu ya Wadau wengine wa Mahakama Kanda ya Mwanza.
Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt Ntemi Kilekamajenga wakiwa
katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kanda ya Mwanza.
Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu
ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt. Ntemi Kilekamajenga (katikati), Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda (wa tatu
kushoto) na Majaji wa
Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza wakati wa
Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya
Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akihutubia wananchi katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki
kanda ya Mwanza kwenye Maadhimisho ya
Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Ntanda akihutubia katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji
Haki Mwanza kwenye maadhimisho ya siku ya sheria nchini.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya
Mwanza Mhe. Dkt Ntemi Kilekamajenga
akikagua Gwaride maalum lililoandaliwa kuashiria kuanza kwa mwaka mpya wa
Mahakama, 2026.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni