Jumatatu, 23 Februari 2026

MAHAKAMA TANZANIA YAJIVUNIA MAFANIKIO YA USIKILIZAJI MASHAURI

  • Zaidi ya asilimia 93 ya mashauri yaliyopangwa yamalizwa
  • Yarejesha kwenye mzunguko wa fedha trioni 13 kwa muda mfupi

 Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, leo tarehe 23 Februari, 2026, amekutana na Waandishi wa Habari katika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma na kuelezea mafanikio makubwa yaliyopatikana, ikiwemo kumaliza mashauri ya kimkakati yanayohusu biashara, uchumi na kodi yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania Trioni 13.1 katika kipindi kifupi.

Mhe. Nkya amebainisha kuwa mashauri hayo 2,973 yalisikilizwa katika ngazi mbalimbali za Mahakama kuanzia tarehe 3 Novemba hadi 15 Desemba, 2025. Amekumbusha kuwa Oktoba 8, 2025, Mahakama iliitisha kikao maalum cha wadau wa masuala ya biashara na uchumi kwa lengo la kuweka mikakati ya kusikiliza mashauri 2,128 ya kiuchumi yaliyokuwa tayari kwa usikilizaji katika ngazi mbalimbali za mahakama.

Kwa mujibu wa Msajili Mkuu, wakati huo Mahakama ya Rufani ilikuwa na mashauri 405, Mahakama Kuu mashauri 1,673, Mahakama za Hakimu Mkazi mashauri 17 na Mahakama za Wilaya mashauri 33. Jumla ya mashauri hayo yalikuwa yameshikilia kiasi cha shilingi trilioni 4.4 za kitanzania.

Amefafanua kuwa usikilizaji wa mashauri hayo ulianza Novemba 3 hadi Desemba 15, 2025, kupitia vikao maalum pamoja na utaratibu wa kawaida wa Mahakama. Kutokana na baadhi ya mashauri kumalizika mapema, Mahakama ilipata fursa ya kuongeza mashauri mengine 1,068, yakiwemo 256 yaliyohusu masuala ya hifadhi ya jamii na kufanya jumla ya mashauri yaliyosikilizwa kufikia 3,196.

“Tuliweza kumaliza mashauri 2,973, sawa na zaidi ya asilimia 93 ya mashauri tuliyokuwa tumepanga kuyasikiliza. Hili ni jambo la kujivunia kwa Mahakama na Wadau wote walioshiriki,” amesema Mhe. Nkya.

Alieleza kuwa thamani ya fedha iliyohusika katika mashauri yaliyomalizika ilifikia shilingi trilioni 13.1, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya kile kilichokuwepo awali. Mafanikio hayo, yanaendana na kaulimbiu ya Siku ya Sheria ya mwaka 2026 iliyosisitiza mchango wa Mahakama katika ustawi wa jamii na maendeleo ya nchi.

Katika kuimarisha utatuzi wa migogoro, Msajili Mkuu ameeleza kuwa Mahakama pia ilitumia njia ya usuluhishi ambapo mashauri 18 yalimalizika kupitia utaratibu huo, huku mashauri 25 yakiombwa na Wadaawa kupelekwa kwenye usuluhishi nje ya Mahakama.

Mhe. Nkya alibainisha kuwa vikao maalum vya Wadau vimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza mlundikano wa mashauri, ambapo hadi kufikia mwisho wa mwaka 2025, mashauri yaliyokuwa yamelundikana yalikuwa asilimia tano ya mashauri yote. Aidha, amesema kuwa wastani wa muda wa usikilizaji ulipungua kutoka siku 96 hadi 30 katika Mahakama za Mwanzo, ambazo hushughulikia zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yote.

Alieleza kuwa vikao hivyo hushirikisha Taasisi mbalimbali za kiserikali na binafsi zikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha, Benki Kuu, Tume ya Mipango, Baraza la Ushindani, Baraza la Rufani la Kodi, Umoja wa Mabenki, Chemba ya Taifa ya Biashara, Mamlaka ya Uwekezaji wa Maeneo Maalum ya Kiuchumi, Chama cha Wanasheria Tanganyika, pamoja na Wadau wengine wanaohusika na masuala ya kiuchumi na biashara.

Msajili Mkuu ameeleza kuwa mkutano wa leo wa Wadau hao ni mwendelezo wa kikao kilichofanyika tarehe 8 Oktoba, 2025, ambapo walikubaliana kukutana mara nne kwa mwaka ili kufuatilia utekelezaji wa mikakati waliyojiwekea.

Aliongeza kuwa mbali na mashauri ya kiuchumi na biashara, Mahakama pia inaendelea kufanya tathmini ya mashauri ya haki jinai, na kikao kingine cha Wadau wa sekta hiyo kinatarajiwa kufanyika ili kupima mafanikio ya mikakati iliyowekwa awali.

Kwa ujumla, Mahakama imeonesha dhamira ya kuendelea kuboresha utoaji haki kwa wakati, kupunguza gharama kwa Wadaawa na kuimarisha mchango wake katika kukuza uchumi na maendeleo ya Taifa.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya [juu na chini] akizungumza na Waandishi wa Habari leo tarehe 23 Februari, 2026, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Katibu wa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Jovin Binshanga [kushoto] pamoja na sehemu ya Waandhi wa Bari [juu na chini] wakichukua kumbukumbu muhimu wakati wa mkutano huo. 




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni