Jumatatu, 23 Februari 2026

TAARIFA YA KITAALAAM YA MAFUNZO KUHUSU FIDIA KWA WAFANYAKAZI YAANDALIWA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), wanakutana mjini Kibaha kuandaa taarifa ya kitaalaam ya mafunzo awamu ya kwanza kuhusu fidia kwa Wafanyakazi yaliyofanyika nchi nzima kwa nyakati tofauti.

Mafunzo hayo yalifanyika mfululizo Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia Bagamoyo tarehe 09-10 Juni 2023, Mwanza tarehe 15-16 Agosti 2023, Arusha tarehe 01-02 Desemba 2023, Songea tarehe 09-12 Februari 2024, Kigoma tarehe 19-20 April 2024, Zanzibar tarehe 19-20 Julai 2024 na Arusha tarehe 07-08 Oktoba 2024.

Akizungumza wakati anafungua kikao kazi hicho cha siku nne leo tarehe 23 Februari, 2026, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, amesema kuwa mafunzo hayo yamekuwa chachu ya kuongeza uelewa miongoni mwa Majaji, Naibu Wasajili, Wasuluhishi, Waamuzi, Watendaji wa Mahakama na Maofisa wengine wa Mahakama nchi nzima, kuhusu namna bora ya kushughulikia masuala ya fidia kwa wafanyakazi kwa mujibu wa sheria.

Huku akinukuu Wanazuoni mbalimbali, Jaji Mfawidhi amebainisha kuwa kukusanya elimu na kuiweka katika mfumo wa compendium si jambo la kawaida, bali ni jukumu la kitaaluma na la hali ya juu na kwamba ni mahali pa kupata taarifa kuhakikisha kuwa Hakimu, Mwanasheria, au mtoa huduma hafanyi kazi kwa njia ya makisio, bali ana rejea thabiti.

Miongoni mwa Wanazuoni hao ni James Boswell katika kitabu cha The Life of Samuel Johnson, Oxford World’s Classics, Ukurasa wa 1071, Blaise Pascal katika Kitabu cha The Provincial Letters, letter 16 na Francis Bacon aliandika katika kitabu cha The Essays of Counsel, Civil and Moral Studies Uk. 50.

‘Naamini itatumika kama rejea mahakamani, kwenye shughuli za WCF na Wizara kwa ajili ya mabadiliko ya sera na sheria, Vyuo na Vyuo Vikuu mbalimbali, Shule ya Sheria, Kikanda ikiwa ni pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Shirika la Kazi Duniani (ILO) na sehemu mbalimbali Duniani kama chachu ya mabadiliko ya sheria,’ Mhe. Dkt. Mlyambina amesema.

Jaji Mfawidhi amebainisha kuwa kuwa juhudi hii ya kuandaa compendium ni sehemu ya kuwapa silaha watumishi wa sheria, wakiwemo Majaji, Manaibu Wasajili, Wasuluhishi, Waamuzi na Watendaji ili waweze kubadilisha dunia ya kazi na kutoa haki kwa ufanisi zaidi kwa wafanyakazi wanaopata madhira au magonjwa wakiwa kazini.

Amemnukuu Rais wa Afrika Kusini na Mshindi wa Tuzo ya Nobel, kwa sasa Marehemu Nelson Mandela kama alivusema: 'Education is the most powerful weapon which you can use to change the world.' (Elimu ni silaha kali unayoweza kuitumia kubadilisha dunia).

Mhe. Dkt. Mlyambina amewakumbusha maneno ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyeasisi umuhimu wa kuandika vitabu kwa ajili ya uhifadhi wa ukweli. Mwalimu alisema: 'What is written is permanent; it can be referred to, ‘akimaanisha kuwa; ‘Kilichoandikwa ni cha kudumu; kinaweza kurejelewa).

‘Kupitia compendium hii, tunajenga uhakika kwamba mafunzo yetu ya fidia hayatapotea kwenye mawazo ya muda mfupi, bali yatakuwa kumbukumbu ya kudumu itakayowalinda wafanyakazi na kuongoza watoa haki kwa miaka ijayo,’ amesema.

Ameendelea kumnukuu Mwalimu Nyerere alipokuwa anaelezea kwa nini aliamua kukusanya na kuichapisha hotuba zake za awali (1952–1965) aliwahi kusema katika kitabu chake cha Freedom and Unity: katika utangulizi (Preface), toleo la Oxford University Press (1966), ukurasa wa xvii.

Mwalimu alisema, "I have put these speeches together... primarily because I want to leave a record of the growth of our nationalist movement... We must write our own history. If we don't, others will write it for us..."

Kwa tafsiri isiyo rasmi ni; ‘Nimekusanya hotuba hizi... hasa kwa sababu nataka kuacha rekodi ya ukuaji wa harakati zetu za kitaifa... Tunapaswa kuandika historia yetu wenyewe. Kama hatutaandika, wengine wataandika kwa ajili yetu...’

‘Kwa msingi huo, kikao hiki kinabeba umuhimu mkubwa katika kuunganisha fikra, uzoefu na ushahidi wa wahanga walioshiriki katika vikao kazi, ili tuweze kuandaa rejea ya kitaalamu yenye ubora, inayostahili hadhi ya Mahakama na WCF kama Taasisi tegemeo katika utoaji wa haki na ustawi wa wafanyakazi nchini,’ Jaji Mfawidhi amesema.

Ameeleza kuwa compendium hiyo itaweka vema kumbukumbu juu ya yote yaliyojiri kabla ya mafunzo (msimamo wa sheria kufika Juni 09-10, 2023), wakati wa mafunzo (mapendekezo ya washiriki ama maamuzi ya kesi mbalimbali yaliyopelekea mabadiliko ya sheria ama kanuni wakati mafunzo yanaendelea) na nini wanapendekeza.

Mhe. Dkt. Mlyambina, kwa niaba ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ametoa shukrani za dhati kwa WCF kwa ufadhili na ushirikiano thabiti uliowezesha kufanyika kwa mafunzo hayo na sasa kikao hiki cha kuandaa compendium.

Amesema kuwa wataanza na compendium ya Kingereza kisha kuaitafsiri kwa Kiswahili kama alivyoagiza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania wakati anafungua Kikao Kazi kati ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mfuko wa Fidia uliofanyika jijini Arusha ili Watanzania wote waweze kufaidika nayo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akizungumza wakati anafungua kikao kazi hicho.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina [katikati] akiwa katika picha ya pamoja na Mtalaam Mwelekezi, Dkt. Cornel Mtaki [kushoto] na Ofisa Sheria Mwandamizi, Bi Francisca Kweka.

Meza Kuu ikiwa kawenye picha ya pamoja na Timu ya watalaam wa kazi husika, Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Enock Matembele [wa tatu kulia], Kaimu Mtendaji, Bi. Joyce Mulugu [katikati], Naibu Msajili, Mhe. Mary Mrio [wa pili kushoto], Naibu Msajili, Mhe. Rita Tarimo [wa tatu kushoto] na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji, Mhe. Jane Masua, Mhe. Baraka Mahenge na Mhe. Suzana Mwiguru.



Kikao kazi kikiendelea [juu na chini].


 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni