Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita
Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, amefanya ziara ya
ukaguzi katika Mahakama za Wilaya za Bukombe, Mbogwe na Nyang’hwale,
kwa lengo la kujionea hali halisi ya uendeshaji wa mashauri pamoja na nidhamu
ya Watumishi.
Katika ziara hiyo,
Jaji Mhina aliwapongeza Watumishi wa Mahakama hizo kwa
kutekeleza maelekezo ya kuhakikisha kasi ya usikilizaji wa mashauri
kwa mwaka 2026 inaongezeka.
Aliwasisitiza kuwa
wahakikishe wanavuka mwaka 2026 bila kuwa na mashauri
kwa Mahakama za Mwanzo kama walivyofanya mwaka 2025 kwa kumaliza mwaka wakiwa
wamemaliza mashauri yote yaliyokuwa yamefunguliwa. Aidha,
alisifu hatua ya kutokuwepo kwa malalamiko ya ukiukwaji wa maadili katika
usikilizaji wa mashauri.
Pamoja na pongezi
hizo, Jaji Mhina alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa
viwanja pamoja na nyumba za Mahakama
zisizotumika ili kuzuia uvamizi na upotevu wa mali za Taasisi.
Aliwahimiza Viongozi na Watumishi kutafuta
matumizi mbadala ya viwanja vilivyo wazi ili kuongeza tija na kuchangia ukuaji
wa uchumi wa Taifa.
Vilevile,
aliwataka Viongozi wa Mahakama kuendelea
kujadili masuala ya maadili katika vikao vya ndani ili kuimarisha utendaji kazi
na kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza wakati wa uendeshaji wa mashauri.
Katika ziara hiyo,
Jaji Mhina aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Fredrick Lukuna,
Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, pamoja na Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mhe. Cleofas Waane na Maofisa
wengine.
Naye Mtendaji
wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwataka watumishi
kuendelea kuzingatia taratibu za ununuzi wa Serikali kupitia
mfumo wa kielektroniki wa ununuzi (NeST) ili kuhakikisha uwazi na ufanisi
katika matumizi ya rasilimali za umma.
Jaji Mhina na wajumbe wake walitembelea pia mradi wa ujenzi wa jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe kwa lengo la kukagua maendeleo yake.
Akizungumza wakati
wa ukaguzi huo, Jaji Mhina alisema kuwa jengo hilo linatarajiwa kuanza kutumika
kabla ya Juni 2026. Alibainisha kuwa kwa sasa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe
inafanya kazi katika mazingira finyu yasiyokidhi mahitaji, hali inayowaweka Watumishi
katika mazingira magumu na hatarishi kiafya na kiutendaji.
Kwa sasa, ujenzi wa jengo hilo umefikia hatua ya mwisho ya umaliziaji, ukiwa katika hatua ya upakaji rangi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda
ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akisaini kitabu
cha wageni katika Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.
Hakimu Mkazi Mfawidhi
wa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe, Mhe. Mashaka
Msonogone, akitoa taarifa ya usikilizaji
wa mashauri na ikama ya Watumishi Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.
Mtendaji wa
Mahakama Geita akisisitiza Watumishi kufuata
taratibu za ununuzi kupitia Mfumo nunuzi (NeST) ili kuongeza uwazi na ufasi kwa
rasilimali za umma.
Hakamu Mkazi
Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe, Mhe. Zawald Nyekelela,
akitoa taarifa ya mashauri Mahakama ya Wilaya ya Bukombe.
Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Geita, Mhe. Kevin Mhina, akijadiliana na
Mtendaji wa Mahakama Geita, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa
Mahakama ya Wilaya Mbogwe namna ya kuweka uzio kwenye jengo la Mahakama ya
Mwanzo Masumbwe.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni