Jumatatu, 23 Machi 2026

‘ZINGATIENI MAELEKEZO YA VIONGOZI YANABORESHA, KULETA UFANISI KATIKA UTENDAJI KAZI’

Na FRANCISCA SWAI - Mahakama Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, amewaasa Watumishi kufanya kazi kwa weledi, kuzingatia na kutekeleza maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama.

Mhe. Mtulya alitoa wito huo hivi karibuni katika ziara ya ukaguzi wa Mahakama ndani ya Kanda ya Musoma, huku akisisitiza maelekezo ya Viongozi yanapaswa kuzingatiwa ili kuhakikisha utoaji wa haki unafikiwa kama inavyokusudiwa.

Aidha, aliwapongeza Watumishi kwa mafanikio mbalimbali yaliyofikiwa ndani ya Kanda kutokana na kuzingatia maelekezo ya Viongozi yliyosababisha kutokuwa na Mahabusu wa Mahakama za Mwanzo kwenye Magereza yote.

Alisema kuwa jambo hilo limesaidia kupunguza msongamano gerezani, lakini pia kuwaruhusu Washtakiwa ambao wangelazimika kukaa Mahabusu kuendelea na shughuli zao za kiuchumi, huku wakiendelea pia na mashauri yao mahakamani.

Pamoja na pongezi hizo, Mhe. Mtulya na Viongozi alioambatana nao katika ukaguzi huo, ambao ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora na Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi, walisisitiza umuhimu wa kuzingatia ufungaji wa mirathi kwa mujibu wa taratibu.

Viongozi hao waliwekeana mikakati mbalimbali ya kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa ufanisi na ndani ya muda waliojiwekea.

Vilevile, Mhe. Mtulya aliwapongeza Watumishi kwa namna wanavyojitoa kushiriki matukio mbalimbali ya kijamii pamoja na safari za utalii wa ndani zinazopangwa ndani ya Kanda.

‘Pamoja na kuwa tunatumia muda wetu mwingi kazini, ni muhimu kushiriki matukio hayo ili kujenga umoja na mshikamano, kutunza kumbukumbu nzuri za pamoja, kuongeza ari, tija na mahusiano bora kati ya Watumishi,’ alisema.

Katika ukaguzi huo, Mhe. Mtulya alitembelea ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Serengeti pamoja na kukagua maeneo na mipaka ya Mahakama mbalimbali ndani ya Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma, Naibu Msajili, Mhe. Monica Ndyekobora (wa tatu kushoto), Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi (wa tatu kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Rorya, Mhe. Tumaini Marwa (wa pili kulia), pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Shirati iliyoko Wilayani Rorya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akisistiza jambo wakati wa kikao na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tarime na Mhakama ya Mwanzo Tarime Mjini (hawako pichani). Kushoto ni Naibu Msajili, Mhe. Monica Ndyekobora na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Tarime, Mhe. Veronica Selemani (aliyesimama) akisoma taarifa ya utendaji kazi wa kituo hicho mbele ya Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma (hawako pichani) na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tarime na Mya Mwanzo Tarime Mjini.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Musoma, Mahakama ya Mwanzo Musoma Mjini na Mahakama ya Mwanzo Mukendo wakisikiliza kwa makini maelekezo yanayotolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya na Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma (hawako pichani).

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (mbele) akisikiliza kwa makini maelezo yanayotolewa na Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi (aliyesimama) wakati wa kikao na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Butiama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (wa tatu kulia) akiwa pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Serengeti na Mahakama ya Mwanzo Mugumu Mjini.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma, Naibu Msajili, Mhe. Monica Ndyekobora (wa tatu kushoto), Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi (wa tatu kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Musoma, Mhe. Hadija Masala (wa kwanza kushoto mstari wa nyuma), pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Bukwaya iliyoko Wilayani Musoma.

Muonekano wa jengo linalojengwa la Mahakama ya Wilaya Serengeti.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni