Jumatatu, 23 Machi 2026

ZINGATIENI MAADILI NA TARATIBU ZA UTUMISHI WA UMMA; JAJI TIGANGA

Na MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga amewataka Mahakimu pamoja na watumishi wengine wa Mahakama kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na taratibu za utumishi wa umma.

Ameyasema hayo hivi karibuni wakati akifanya ukaguzi wa Mahakama Mkoa wa Songwe pamoja na Wilaya ya Mbarali unaolenga kukumbushana kuhusu majukumu ya kila siku na kubaini mapungufu, changamoto na kuona mapendekezo na njia sahihi za kutatua changamoto hizo.

“Fanyeni kazi kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma na nidhamu kama njia ya kuelekea kuhitimisha utumishi katika hali inayofaa” alisema Mhe. Tiganga

Mhe. Tiganga aliwasisitiza watumishi hao kuongeza kasi katika umalizaji wa mashauri kwa kuzingatia lengo mama la Mahakama ya Tanzania ambalo ni kusikiliza mashauri na kuyatolea maamuzi mapema ipasavyo. Vilevile Mhe. Tiganga aliwaasa watumishi kuendelea kudumisha ushirikiano mzuri uliopo eneo la kazi.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mavis Francis Miti, alitoa pongezi kwa uongozi wa Mahakama ya wilaya ya Mbarali kwenye kufuatilia suala la viwanja kwa haraka kama ilivyoelekezwa kuelekea lengo la Mahakama ya Tanzania kuwa na Mahakama katika kila Kata.

Katika ziara hiyo, Mhe. Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu kanda ya Mbeya Mhe. Tiganga aliambatana na viongozi wengine wa Mahakama akiwemo Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Emily Temu, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer na Afisa Utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Bi. Paulina Kaaya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) akiwa kwenye pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Songwe.wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mavis Francis Miti, wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama kuu Masijala ndogo ya Songwe Bw. Sostenes Mayoka, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Emily Temu, (wa pili kulia) Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Emily Temu na wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu masjala ndogo  Songwe Mhe. Joyce Mark Minde.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akipokea maelezo maalum wakati wa alipokuwa akikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Kituo Chumuishi Songwe.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Kituo Chumuishi Songwe.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami akiwasilisha taarifa mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Hayuipo pichani) katika ziara hiyo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni