Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga ameshiriki mazishi ya aliyekuwa
Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese, Kanda ya Morogoro, Mhe. Asajile Joshua
Mhando. Mazishi hayo yamefanyika tarehe 20 Februari 2026 katika Kijiji cha
Vwawa, Wilaya ya Mbozi, Mkoa wa Songwe, ambako ndiko nyumbani kwa familia ya
marehemu Asajile Mhando.
Awali, mwili wa marehemu
uliagwa na viongozi pamoja na watumishi mbalimbali wa Mahakama Kuu Kanda ya
Mbeya katika viunga vya Mahakama hiyo, wakiwemo Waheshimiwa Majaji wa Mahakama
ya Rufani Tanzania waliokuwa wakiendelea na vikao vya mashauri ya rufani katika
Kanda hiyo na baadaye mwili wa marehemu ulisafirishwa kwenda Kijiji cha Vwawa,
Mkoa wa Songwe, kwa ajili ya kupumzishwa kwenye nyumba yake ya milele.
Akizungumza wakati wa
mazishi hayo, Mhe. Tiganga, alitoa salamu za pole kwa mjane, familia na ndugu
wa marehemu, pamoja na kutoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya
Morogoro na Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe kwa mchango wao mkubwa katika
kufanikisha kumpumzisha aliyekuwa mtumishi hodari wa Mahakama ya Tanzania.
“Ninafahamu hiki ni
kipindi kigumu kwa mjane, familia na hata watumishi wenzake, lakini hatuna budi
kukubali kwani ni mapenzi ya Mwenyezi Mungu; aliyemtoa ndiye aliyemtwaa. Wajibu
wetu sisi ni kumuombea ili Mwenyezi Mungu ampumzishe kwa amani,” alisema Mhe.
Tiganga.
Aidha, Mhe. Tiganga
aliwasisitiza wanafamilia kufuatilia stahiki za marehemu kutoka kwa mwajiri
mara baada ya kumaliza msiba, ikiwemo kukaa kikao cha familia na kumteua
msimamizi na mfuatiliaji wa stahiki hizo.
Kwa upande wa Uongozi wa
Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro ulitoa shukrani zao kwa Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, pamoja na Uongozi wa
Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, kwa ushirikiano mkubwa waliouonesha katika
kumpumzisha aliyekuwa mtumishi mwenzao kutoka Kanda ya Morogoro.
Mhe. Asajile Joshua
Mhando alifariki Dunia mchana wa tarehe 17 Februari 2026 katika Hospitali ya
Platinum, mjini Morogoro, alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kujisikia
vibaya akiwa kazini. Marehemu atakumbukwa kwa ucheshi wake, busara, unyenyekevu
na ari ya kuchapa kazi, kwani hadi umauti unamfikia hakuwa na shauri lolote la
mlundikano; alikamilisha mashauri yote aliyopangiwa kwa wakati.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe.
Joachim Tiganga akizungumza machache katika mazishi hayo.
Viongozi, Majaji wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya
watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wakitoa pole kwa wafiwa na kuaga
mwili wa Marehemu Mhe. Asajile Mhando katika viunga vya Mahakama Kuu Kanda
Mbeya walipopita katika Kanda hiyo wakitokea Mkoani Morogoro
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi
Songwe Mhe. Francis Kishenyi (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika
Mazishi hayo.
Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama kutoka
Morogoro, Mbeya na Songwe walioshiriki mazishi hayo wakiongozwa na Jaji
Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wapili kushoto waliosimama mbele)
Sehemu ya waombolezaji katika mazishi hayo.
Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama kutoka
Morogoro, Mbeya na Songwe walioshiriki mazishi hayo wakiongozwa na Jaji
Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wapili kushoto
kwa waliokaa mbele)
Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wakitoa pole kwa wafiwa na kuaga mwili wa Marehemu Mhe. Asajile Mhando katika viunga vya Mahakama Kuu Kanda Mbeya walipopita katika Kanda hiyo wakitokea Mkoani Morogoro
Mwili wa aliyekuwa hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese
Kanda ya Morogoro Mhe. Asajile Joshua Mhando ukiagwa huko kijijini kwao Vwawa
wilaya ya Mbozi mkoa wa Songwe.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni