Ijumaa, 27 Machi 2026

JAJI NONGWA AAGWA MBEYA KWA TAFRIJA KABAMBE

Na. MUKSINI NAKUVAMBA- Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, ameongoza viongozi na watumishi wa Mahakama katika hafla maalum ya kumtakia kheri na baraka, Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Victoria Mlonganile Nongwa kufuatia uteuzi wake wa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe.

Hafla hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, ilihudhuriwa na Viongozi na Watumishi mbalimbali wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Njombe, Songwe na Iringa. Vilevile watumishi walipata wasaa wa kutoa shukrani, pongezi na kumbukumbu za namna Mhe. Nongwa alivyogusa maisha ya wengi kupitia uongozi wake.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga alimpongeza Mhe. Nongwa kwa utendaji wake uliotukuka na uwezo wake wa kujenga mshikamano miongoni mwa watumishi, akibainisha kuwa ameacha alama isiyofutika katika utumishi wa Mahakama hiyo.

“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuteuliwa kwako kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, tumeshuhudia uongozi wenye busara, upendo na ushirikiano kutoka kwako. Umeweza kuunganisha watumishi na kujenga mazingira ya kazi yenye kuheshimiana na kusaidiana,” alisema Mhe. Tiganga.

Naye, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu alisema, Uongozi bora wa Mhe. Nongwa ulipekea kutunukiwa tuzo mbalimbali za uchapakazi bora kwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

“Umekuwa kiongozi na mshauri mzuri katika kutekeleza majukumu ya utumishi wako hapa Mbeya, umekuwa na utayari wa kipekee sana mpaka kutunukiwa tuzo mapema Februari 2026 na Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya kwa kutambua na kuthamini utayari wako wakati wote katika kutekeleza majukumu ya kimahakama hata pale uliposhtukizwa wewe ulikuwa tayari kupokea majukumu hayo ya usikilizaji wa mashauri ambalo ni jukumu mama la Mahakama ya Tanzania,” alisema Naibu Msajili huyo.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi mteule wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe Mhe. Victoria Nongwa alitoa shukrani kwa watumishi wenzake kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote cha utumishi wake katika Kanda ya Mbeya, akieleza kuwa mafanikio aliyoyapata yametokana na mshikamano na moyo wa pamoja kazini.

“Naondoka nikiwa na kumbukumbu nzuri ya kufanya kazi na timu yenye upendo na mshikamano. Nitaendelea kuthamini mahusiano haya hata ninapoanza majukumu yangu mapya mkoani Njombe na nayabeba mazuri yote ya Mbeya,” alisema Mhe. Nongwa.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa, Mhe. Nongwa alikuwa kiongozi aliyesikiliza, aliyejali ustawi wa watumishi na aliyehamasisha utendaji kazi wa pamoja, hali iliyochangia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za haki.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama) akitoa nasaa zake kwa Viongozi na watumishi wa Mahakama (hawapo pichani) wakati wa hafla hiyo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama) akizungumza machache na Viongozi na Watumishi wa Mahakama katika hafla ya kuagwa kwake.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Marvis Miti (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya na Njombe wakiwa wameshikana mikono kwa pamoja ikiwa ni ishara ya upendo na mshikamano.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (aliyesimama) akitoa shukurani kwa niaba ya Mahakimu wa Kanda ya Mbeya na Songwe waliohudhuria katika hafla hiyo.

Mmoja wa watumishi (aliyesimama) akitoa neno la shukurani kwa niaba ya watumishi wengine katika hafla hiyo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya na Njombe wakiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo mbele ya Jengo la Mahakama Kuu Kanda ya mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)









Hakuna maoni:

Chapisha Maoni