Na AIDAN ROBERT - Mahakama Kigoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,
Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka Mahakimu pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Kigoma kufanya kazi kwa
kuzingatia mambo sita muhimu ya maadili ambayo ni Uadilifu, kuwa viongozi bora
kwa wengine, kujali stahili za watumishi, Ubunifu katika kazi, Mahusiano mazuri
kazini na mawasiliano ya karibu katika utendaji wa shughuli za kiutawala.
Mhe. Rwizile aliyasema hayo tarehe 28 Machi 2026 wakati
akifungua Kikao cha Uongozi kwa robo ya tatu ya mwaka kilichofanyika kwenye ukumbi
wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe ambapo alitumia fursa hiyo kuwakumbusha kuhusu
majukumu ya kila siku na kubaini mapungufu, changamoto na kuona mapendekezo na
njia sahihi za kutatua changamoto hizo.
“Fanyeni kazi kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma
na nidhamu kama Sheria ya Utawala wa
Mahakama inavyotutaka katika ibara (237), ambapo Sheria hii ina maboresho yake
imeeleza wazi utendaji wa Viongozi wa Mahakama katika mnyororo wa haki na hasa
fungu la (11) ambapo linaeleza wazi jinsi ambavyo utawala katika muhimili wa
Mahakama unapaswa kuwa, ni vema mkaisoma vizuri ili kuongeza weledi katika eneo
la utawala,” alisema Jaji Rwizile.
Aidha, alisisitiza pia kifungu cha (65) cha sheria hiyo
kinachotoa namna ambavyo watendaji wanafanya kazi wakishirikiana na Ofisi ya
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, ikiwataka kushirikiana kwa karibu ili
kuhakikisha shughuli za kiutawala zinasimamiwa vema kwa ajili ya kuhakikisha
mnyororo wa usikilizwaji wa mashauri katika Mahakama zote haukwami kwa namna
yeyote.
Hata hivyo, aliwasisitiza viongozi hao kuongeza kasi
katika umalizaji wa mashauri kwa kuzingatia lengo mama la Mahakama ya Tanzania
ambalo ni kusikiliza mashauri na kuyatolea uamuzi mapema ipasavyo. Vilevile
Mhe.Rwizile aliwaasa Viongozi kuendelea kudumisha ushirikiano mzuri uliopo eneo
la kazi.
Sambamba na hayo Jaji Rwizile, alizindua chumba cha Hakimu
wa Mahakama ya Mwanzo Kasulu Mjini kilichokarabatiwa kwa fedha ya ndani ili
kusaidia kusogeza huduma na kuongeza kasi ya usikilizwaji wa mashauri kwa Mahakama
za Mwanzo.
Aidha, wajumbe wa kikao hicho walipata fursa ya kupanda
miti ya matunda katika eneo la wazi lililopo katika Mahakama ya Wilaya Buhigwe.
Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma
Mhe. John Francis Nkwabi, alitoa pongezi kwa Viongozi wa Mahakama za Wilaya Kanda
ya Kigoma kwa jinsi wanavyoshirikiana kwa karibu na watumishi wa kada zote kuhakikisha
usikilizwaji wa mashauri na kutunza miundombinu ya Majengo na TEHAMA inaendelea
kuboreshwa ili utendaji wa kazi za watumishi uendelee kuwa rahisi, sambamba na
ubunifu unaoleta tija katika shughuli za kila siku.
Katika ziara hiyo iliyoambatana na Kikao cha Uongozi, Jaji
Mfawidhi, Mhe. Rwizile aliambatana na Viongozi wengine wa Mahakama akiwemo Jaji
wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza, Naibu Msajili Mahakama
Kuu, Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya
Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka na Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Singida, Bw.Filbert
Matotay, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo,
Mahakimu Wakazi Wafawidhi kutoka Wilaya za Kigoma, Kasulu, Kibondo, Uvinza,
Buhigwe na Kakongo pamoja na Wakuu wa Vitengo wa Mahakama Kuu Kigoma.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Kasulu (waliosimama) mara baada ya uzinduzi wa chumba cha Hakimu. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni