Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu
Mtulya, amewapogeza Watumishi
wa Mahakama Kanda ya Musoma kwa uwajibikaji mzuri uliowezesha Mahakama hiyo
kuwa ya pili kitaifa kwa kasi nzuri ya umalizaji wa mashauri.
Mhe. Mtulya alitoa
pongezi hizo katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma kilichofanyika hivi
karibuni wilayani Serengeti katika ukumbi wa Ofisi ya Mashtaka.
Alisisitiza umuhimu
wa vikao vya menejimenti ambavyo vinatumika kuweka mikakati mbalimbali ya
kiutendaji pamoja na kusisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa juu,
jambo lililodhihirishwa kwa matokea mazuri ya usikilizaji na umalizaji wa
mashauri.
Aidha, katika kikao
hicho kinachoundwa na wajumbe kutoka Mahakama Kuu Musoma, Mahakama ya Hakimu
Mkazi Musoma na Mahakama za Wilaya za Musoma, Butiama, Bunda, Serengeti, Tarime
na Rorya, ziliwasilishwa taarifa mbalimbali za utendaji kazi kwa robo ya tatu
ya mwaka wa fedha 2025/26.
Kuliwasilishwa pia taarifa
za Mkaguzi wa Ndani, Ofisa TEHAMA, miradi inayoendelea ndani ya Kanda na ushiriki
katika matukio ya kijamii.
Akizungumza katika
kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora,
alisisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa Mahakama, ikiwemo ufungaji
wa mirathi, kuendelea na utoaji wa adhabu mbadala pamoja na usikilizaji wa
mashauri kwa wakati ili kuepuka kuzalisha mlundikano.
Naye Mtendaji wa
Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi, alielezea mikakati mbalimbali ya Kanda,
ikiwemo uboreshaji wa miundombinu. Alisema kwa mwaka wa fedha, Kanda inaendelea
na ukarabati mkubwa wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Nyaburongo iliyoko Wilayani
Rorya kwa kutumia fedha za ndani.
Pia alielezea hatua
iliyofikiwa katika miradi inayoendelea ya ujenzi wa Mahakama za Wilaya
Serengeti na Tarime. Aidha, aliwaasa Watumishi kuendelea kuzingatia kanuni,
taratibu na miongozo ya utumishi wa umma.
Akihitimisha kikao
hicho, Mhe. Mtulya aliwakumbusha wajumbe mafanikio yaliyopatikana ndani ya
Kanda, ikiwemo kutovuka mwaka na mashauri mlundikano kwa miaka mitatu mfululizo
na ukarabati wa majengo ya Mahakama, hasa za Mwanzo.
Alitaja mafanikio
mengine kama ulinzi wa mipaka ya maeneo ya Mahakama, upatikanaji wa hati, umoja
na ushirikiano wa kikanda kwenye kazi na matukio ya kijamii kma kushiriki matukio
ya huzuni na furaha.
Hivyo aliwaasa
wajumbe hao kwenda kuwasimamia vyema Watumishi katika maeneo yao ili, kwa pamoja
waweze kufikia malengo ya Kanda yaliyowekwa.
Wajumbe wa kikao cha Menejiment Kanda ya Musoma kutoka Wilaya mbalimbali wakiwasilisha taarifa za utendaji kazi katika vituo vyao vya kazi.
Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mhe. Veronica Mugendi (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa kituo chake katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.
Afisa Tawala wa Mahakama
Kuu Musoma, Bw. Kandana Lucas (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji
kazi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na taarifa ya miradi inayotekelezwa ndani, huku
wajumbe wakifuatilia kwa makini taarifa hiyo wakati wa kikao cha Menejimenti
Kanda ya Musoma.
Mkaguzi wa Ndani wa
Mahakama Kuu Musoma Bw. Andala Odock (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya
ukaguzi katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.
Afisa TEHAMA wa
Mahakama Kuu Musoma Bw. Japhet Mnyetta (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya
hali ya miundombinu na matumizi ya TEHAMA ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma
wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.
Naibu Msajili wa
Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, akiwasilisha taarifa ya hali ya
mashauri ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda
ya Musoma.
Mtendaji wa Mahakama
Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi (aliyesimama), akifafanua jambo wakati wa kikao
cha Menejimenti Kanda ya Musoma.
Mjumbe wa kamati ya
utalii (matukio ya kijamii) ambaye ni Mhasibu wa Mahakama Kuu Musoma, Bi.
Samira Nkya (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya ushiriki katika matukio ya
kijamii ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya
Musoma.
Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati),
akisisitiza jambo kwa wajumbe wa kikao cha Mnenejimenti Kanda ya Musoma wakati
wa kikao hicho.
Picha ya pamoja ya
wajumbe wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma walipotembelea mmoja ya miradi
inayoendelea ndani ya Kanda hiyo, ambayo ni ujenzi wa Jengo la Mahakama ya
Wilaya Serengeti, mara baada ya kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma
kilichofanyika Wilayani Serengeti.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni