Jumatatu, 16 Machi 2026

KAZI YA UHAKIMU NI ADILIFU NA WITO KATIKA JAMII: JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka Mahakimu Wakazi wapya wa Mahakama za Mwanzo kuzingatia utu, uadilifu na tabia njema katika kutimiza majukumu yao ya uhakimu huku wakimtanguliza Mungu mbele katika kuenenda vema.

Mhe. Rwizile alitoa wito huo tarehe 13 Marchi, 2026 mara baada ya kuwapokea Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama za Mwanzo wakati wa mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi yake.

“Ninyi ambao mmepangiwa kufanya kazi Kanda hii mmependelewa sana kwakuwa Kigoma tunafanya tofauti hivyo dhamana ya utoaji haki ni jukumu zito linalohitaji nidhamu, uaminifu, weledi na tabia njema ya kiwango cha juu na tunaamini kazi hiyo ni adilifu na wito kwenu na ndio matarajio ya jamii, kwani kazi ya uhakimu ni tofauti na kazi zingine,” alisisitiza Jaji Rwizile.

Katika hatua nyingine, Jaji Mfawidhi huyo, alimshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju kwa kuongeza nguvukazi na kuwafunda kwa kiasi cha kutosha Mahakimu hao wapya.

Mhe. Rwizile amewasisitiza Mahakimu hao kuyaishi maelekezo aliyoyatoa Jaji Mkuu tarehe 23 Februari, 2026 mara baada ya kuwaapisha.

Kadhalika Jaji Mfawidhi huyo, amewataka Mahakimu hao kutofungwa na masharti ya kiufundi, kelele za mamlaka au  maneno ya mitandaoni, msukumo wa kihisia, upendeleo wa wazi na kutoa hukumu bila kuzingatia haki itadhoofisha utendaji kazi wao huku akiwasisitiza kwamba wana wajibu wa kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujiamini.

Sambamba na hayo, Mhe. Rwizile amewaasa Mahakimu hao kutumia vizuri muda wao kusoma na kuongeza ujuzi, weledi juu ya kazi yao, huku wakifanya tafiti mbalimbali kabla ya kufanya maamuzi katika kazi zao.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, amewapongeza Mahakimu hao kupata kazi na amewasisitiza kuhusu umuhimu wa kuwa  waadilifu pamoja na kuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, kwakuwa, wananchi wanatarajia kuona mashauri yakisikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo bila ucheleweshaji usio wa lazima huku akiweka wazi kuwa kuchelewa kwa haki kunaweza kuathiri imani ya wananchi kwa Mahakama na kusababisha mlundikano wa kesi mahakamani.

kwa upande wake Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza amewataka Mahakimu hao kujenga umoja na mshikamano katika maeneo yao ya kazi na kuwahimiza kujifunza kwa watumishi watakaowakuta katika maeneo watakayopangiwa kazi, huku akisisitiza kuwa wajifunze kutoka Kanda mbalimbali kwakuwa nguvu ya Mahakama ipo katika ushirikiano, uwajibikaji na kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Ameongeza kuwa, kila Hakimu anapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii kwa matendo na maamuzi mbalimbali, huku wakitumia maarifa na uzoefu wao katika kuchambua masuala na kutoa maamuzi sahihi kwa kuzingatia sheria kwakuwa kazi ya uhakimu ni wito.

Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga ambao wote kwa nyakati tofauti wamewasisitiza Mahakimu hao kujifunza kwa haraka matumizi ya mifumo ya Mahakama ili kwenda na kasi ya Mahakama katika Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akisisitiza jambo alipokuwa akifanya mazungumzo na Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama za Mwanzo. Mazungumzo hayo yalifanyika katika ofisi yake ya Mahakama Kuu Kigoma.

Mahakimu Wakazi wa Mahakama za Mwanzo wapya wanne wakisikiliza kwa makini maelekezo mbalimbali waliyokuwa wakitoa  Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma wakati wa mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John  Nkwabi akisisitiza jambo wakati akitoa nasaha kwa Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama ya Mwanzo waliopangiwa mkoani Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza akizungumza jambo na  Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama ya Mwanzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (kulia) akifanya utambulisho wa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo wapya wanne mbele ya Majaji.  Kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)





 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni