Jumatatu, 9 Machi 2026

MAHAKAMA KUU KANDA YA MOROGORO YAWAFARIJI WANAWAKE WA GEREZA LA KINGOLWIRA

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, imeungana na wanawake wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kwa kufanya ziara ya kijamii katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Maadhimisho hayo  ambayo hufanyika tarehe 8 Machi kila mwaka yalianza kwa watumishi wa Mahakama Kuu kushiriki pamoja na wanawake wengine katika siku hiyo muhimu inayolenga kutambua mchango wa wanawake katika jamii.

Maadhimisho hayo yalibeba na kauli mbiu inayosema, “Haki kwa wanawake na wasichana msingi wa maendeleo jumuishi kufikia dirĂ¡ 2050.”

Baada ya kushiriki katika maadhimisho hayo, watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro walifanya ziara maalum ya kutembelea Gereza la Wanawake Kingolwira lililopo mkoani Morogoro.

Ziara hiyo iliongozwa na Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, ikiwa na lengo la kuwafariji wanawake waliopo gerezani hapo pamoja na kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku wakiwa gerezani.

Watumishi hao walipata fursa ya kujumuika na wanawake waliopo gerezani hapo, kushirikiana nao katika mazungumzo ya faraja pamoja na kuonesha upendo na mshikamano kama sehemu ya kuadhimisha siku hiyo ya wanawake duniani.

Ziara hiyo pia ilikuwa na lengo la kuwapa moyo na matumaini wanawake hao kuwa bado wana nafasi ya kujifunza, kujirekebisha na kuendelea na maisha baada ya kumaliza vifungo vyao.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai, aliwashukuru watumishi wa Mahakama kwa moyo wao wa kujali na kuwafikia wanawake waliopo gerezani.

Alisema kuwa ujio huo umeleta faraja kubwa kwa wafungwa hao na umeonesha mshikamano wa kijamii kwa wanawake wote bila kujali hali walizonazo.

Aidha, alitoa wito kwa watumishi wa umma pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kuheshimu sheria za nchi na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kusababisha kuvunja sheria na hatimaye kujikuta wakitumikia vifungo gerezani.

Aliongeza kuwa gereza hilo pia ni sehemu ya kujifunza na kujenga upya maisha, ambapo wanawake waliopo hapo hupatiwa mafunzo mbalimbali ya stadi za maisha kama vile kilimo, ushonaji wa cherehani pamoja na shughuli nyingine za uzalishaji ili kuwa na ujuzi utakaowasaidia wanaporejea katika jamii.

 Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Mhe. Kinyage aliwahimiza wanawake waliopo gerezani kuwa na uvumilivu, nidhamu pamoja na matumaini katika kipindi chote cha kifungo chao. Aliwaasa kutumia muda wao wakiwa gerezani kujifunza mambo yatakayowasaidia kujenga maisha mapya pindi watakapomaliza vifungo vyao.

“Msijisikie wanyonge kwa kuwa hapa, kwani kila changamoto ina mwisho wake. Muhimu ni kujifunza, kuwa na nidhamu na kujiandaa kwa maisha bora baada ya kutoka hapa,” alisema Mhe.Kinyage

Maadhimisho hayo pamoja na ziara hiyo yameonesha mshikamano, upendo na kujali kwa watumishi wa Mahakama kwa wanawake wote katika jamii, ikiwemo wale waliopo katika mazingira ya kifungo, huku yakilenga kuhamasisha matumaini, marekebisho na mshikamano wa kijamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akiwasalimia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake yakiyofanyika kimkoa Morogoro.

Watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakifanya maandamano katika serehe hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakiwa katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage akikabidhi baadhi ya vifaa kwa Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni