Jumatatu, 9 Machi 2026

WATUMISHI SUMBAWANGA WAPATIWA MAFUNZO KUHUSU MAFAO & KUSTAAFU

Na. Sharifu Mokiwa - Mahakama, Sumbawanga

Watumishi  wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wamepata mafunzo maalumu kuhusu mafao na maandalizi ya kuustaafu ambayo yalitolewa kwa njia mbili yaani uso kwa uso kwa waliokuwepo ukumbini na kwa njia ya Mtandao kwa waliokuwa  mbali.

Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 6 Machi 2026, katika ukumbi wa Mahakama Kuu  Sumbawanga na yalifunguliwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu  Sumbawanga  Bw. Machumu Essaba, kabla ya kuanza kuwasilishwa kwa mada na Afisa  kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi (PSSF) Bw. Eribariki Nsulau

Akizungumza wakati wa kuwasilisha mada Bw. Nsulau alitoa elimu kuhusu huduma na mafao yanayo tolewa na PSS, alifafanua jinsi ya kujisajili kwenye portal ya PSSF kuangalia michango, kuandikisha michango mipya, nakupata mafao mbalimbali, mafao hayo ni pamoja na fao la mishahara miwili endapo mfanyakazi atapoteza ajira ,fao la uzazi ndani ya siku 90 na malipo ya pensheni kuanzia tarehe 21- 23 au 21-25 ya mwezi, yanayolipwa pia kwa wategemezi wa mstaafu. Mafunzo hayo pia yalisisitiza umuhimu wa uhakiki wa kila mwaka kwa wastaafu na wategemezi ili malipo ya pensheni yaendelee bila usumbufu.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Sumbawanga, Mhe. Abubakari Mrisha alitoa mwongozo wa kitaalamu kuhusu maandalizi ya kustaafu na alisisitiza kuwa maandalizi ya kustaafu yanapaswa kuanza mapema mara tu mtumishi anapopata cheki namba, kwani namba hiyo inaonesha muda unaotarajiwa wa kustaafu.

Alieleza kuwa ni muhimu kwa watumishi kupanga maisha yao ya baadae  mapema ili kuepuka changamoto pindi wanapo staafu.

Aidha, watumishi walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu mafao, pensheni, mirathi, na namna ya kujiandaa kustaafu ambapo, mafunzo hayo yamewasaidia kuongeza uelewa na uwajibikaji wa watumishi katika kupanga mustakabali wao wa kifedha, huku wakiongezwa ujuzi muhimu kuhusu hifadhi ya jamii na usimamizi wa michango.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Bw. Machumu Essaba akifungua rasmi mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama tarehe 6 Machi, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Mhe. Abubakari Mrisha (aliyenyanyua mkono) akisisitiza umuhimu wa maandalizi mapema ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama Sumbawanga.

Hakimu Mkazi Mhe. Willington Rwabinyasi akiuliza swali kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu wakati wa mafunzo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Sumbawanga wakisikiliza mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu.

Afisa kutoka PSSF Bw. Elibariki Nsulau akipokea maswali kwa kuyaandika kutoka kwa watumishi wa Mahakama ya Sumbawanga kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu

Afisa kutoka PSSSF Bw. Elibariki Nsulau (aliyesimama) akieleza jinsi ya kujisajili, kuangalia michango nakufahamu mafao kupitia portal ya PSSF.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni